Mkurugenzi
Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Bw. Bernard Konga akiongea na
watumishi wa mfuko huo wakati wa ufunguzi wa mkutano wa nne wa Baraza la
wafanyakazi
Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Bw. Mohamed
Utaly akiwa katika picha ya pamoja na Wajumbe wa Baraza la wafanyakazi wa Mfuko
wa Taifa wa Bima ya Afya.
NA MPIGA PICHA WETU-MOROGORO
Na MWANDISHI WETU- Morogoro
KAIMU Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Bw. Mohamed
Utaly amewataka Watumishi wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya kuwa wazalendo,
waadilifu na kufanya kazi bila kuchoka ili kuhakikisha Mfuko unabaki na uhai
wake na unahudumia vizazi na vizazi.
Amesema kuwa kutokana na Mfuko kwa sasa
kuwa nyenzo na nguzo muhimu katika Sekta ya afya hakuna namna ambayo mwananchi
yoyote anaweza kuwa na amani bila kuwa na bima ya afya ambayo inamuwezesha kuwa
na uhakika wa kupata huduma za matibabu wakati wowote.
Bw. Utaly ameyasema hayo wakati akifungua
mkutano wa nne wa Baraza la Wafanyakazi la NHIF mjini Morogoro ambapo aliutaka
Mfuko kuhakikisha unaendelea na mikakati ya kuwafikia wananchi katika maeneo
yao ili wawaelimishe na kuwahamasisha kujiunga na bima ya afya.
“Jambo muhimu ambalo mnatakiwa kuzingatia
ni kwamba Serikali ya Awamu ya tano imedhamiria kumpa kila mtanzania maisha
bora. Hivyo Mfuko unatakiwa kuwa katika mstari wa mbele kuhakikisha wananchi
wanakuwa na afya bora kwa kuhakikisha wanajiunga na bima ya afya na wanapata
huduma za matibabu kupitia mfumo wa bima,” alisema Bw. Utaly.
Alisema kuwa kwa sasa wananchi wameelewa
dhana ya bima ya afya ikilinganishwa na hapo awali wakati NHIF inaanzishwa
ambapo kulikuwa na upinzani mkubwa ndani ya jamii hususan kwa vyama vya
wafanyakazi hivyo kazi kubwa iliyopo katika Mfuko ni Watumishi kuendelea na
mikakati ya kuwafikia wananchi.
“Mfuko huu una historia kubwa, mimi
nilikuwepo wakati mjadala wa uanzishwaji wake unapita katika vyama vya
wafanyakazi, ni kazi kubwa iliyofanyika mpaka hapa, watumishi wa umma ndio
walikuwa mstari wa mbele kupinga lakini kwa nyakati hizi watumishi hawa hawa
ndio watetezi wa huduma za Mfuko huu kutokana na umuhimu wake katika maisha ya
kila siku,” alisema Bw. Utaly.
Akitoa maelezo ya awali Mkurugenzi Mkuu wa
Mfuko Bw. Bernard Konga alisema kuwa kikao hicho kina agenda za kuweka mipango
thabiti ya uboreshaji wa huduma katika maeneo yote kupitia mipango ya mwaka wa fedha
2020/2021 na mpango mkakati wa miaka mitano ijayo.
Alisema kuwa Mfuko umetekeleza maagizo ya
Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa kuanzisha mpango unaowawezesha kila mwananchi
kujiunga na huduma za bima ya afya.
“Katika hili tumejipanga katika maeneo yote
yakiwemo ya huduma kwa wanachama wetu, kwa sasa tunaendelea na kampeni
mbalimbali za uhamasishaji wananchi katika maeneo yote ili wananchi wengi zaidi
waweze kuwa ndani ya utaratibu wa bima ya afya,” alisema Bw. Konga.
Kutokana na hayo, ametoa wito kwa wananchi
kuchukua hatua haraka za kujiunga na NHIF kupitia mpango wa vifurushi ambavyo
vimezingatia hali halisi ya mahitaji ya huduma na uwezo wa wananchi katika
kuchagia huduma hizo.
No comments:
Post a Comment