Habari za Punde

Wananchi Mikoa ya Kusini wahimizwa kuwasilisha malalamiko yao THBUB

Mwenyekiti wa THBUB, Jaji (Mst.) Mathew Mwaimu (kushoto) akiongea na Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mheshimiwa Godfrey Zambi (kulia) alipomtembelea ofisini kwake

Na Mbaraka Kambona,
Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB), Jaji (Mst.) Mathew Mwaimu ametoa rai kwa Wananchi wanaoishi katika  Mikoa ya Kusini kutokaa na malalamiko na badala yake yawasilishwe  katika ofisi za Tume ili yaweze kushughulikiwa.
Jaji Mwaimu aliyasema hayo Mei 18, 2020 katika ziara aliyoifanya ya kutembelea ofisi ya THBUB iliyopo Mkoani Lindi ambayo inahudumia mikoa yote ya kanda ya kusini ikiwemo Lindi, Mtwara na Songea.
Katika ziara hiyo Jaji Mwaimu alisema kipindi cha miaka miwili iliyopita Tume haikuwa na uongozi kwa maana ya Makamishna jambo ambalo lilichangia baadhi ya kazi kusimama lakini kwa sasa Tume imekamilika hivyo wananchi waendelea kuwasilisha malalamiko yao ili waweze kusaidiwa.
“Niwaeleze Wananchi kwamba Tume ipo, na ipo imara kuwasaidia, walete malalamiko yao yanayohusu ukiukwaji wa haki za binadamu na utawala bora na sisi tunawaahidi yatafanyiwa kazi kwa haraka”, alisema Jaji Mwaimu
Awali akiongea na Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mheshimiwa Godfrey Zambi alipomtembelea ofisini kwake alisema kuwa kimsingi tume ni taasisi iliyoundwa kuisaidia serikali kutatua kero za wananchi zinazohusiana na uvunjifu wa haki za binadamu na misingi ya utawala bora nchini.
“Tume ni jicho la serikali ambalo inalitumia kumulika na kubaini changamoto zinazojitokeza hususani za masuala ya ukiukwaji wa haki za binadamu na misingi ya utawala bora ili kuiepusha serikali kuingia katika migogoro isiyo ya lazima na wananchi wake”, alieleza Jaji Mwaimu
Naye Mkuu wa Mkoa wa Lindi alimueleza Jaji Mwaimu kuwa Mkoa wa Lindi unaendelea kufunguka na kuna miradi mbalimbali inayoendelea kutekelezwa mkoani humo hivyo sio vibaya wakaweka utaratibu wa kufuatilia miradi hiyo ili kujiridhisha kama inatekelezwa kwa kuzingatia misingi ya haki za binadamu.
Aidha, Jaji Mwaimu aliwapongeza Watumishi wa THBUB wa Kanda ya Kusini kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuendelea kuhakikisha kuwa wananchi wa kanda hiyo wanapata huduma nzuri na kwa wakati.
“Kwanza mimi niwapongeze kwa kazi nzuri ambayo mmeendelea kuifanya pamoja na changamoto mbalimbali mnazokabiliana nazo lakini mmeendelea kutoa huduma stahiki kwa wananchi”, aliongeza Jaji Mwaimu
Wananchi wa Mikoa ya Kusini wamehimizwa kutumia ofisi za Tume zilizopo katika Kanda hiyo ili iwe rahisi kwao kupata huduma, na kwa msaada zaidi THBUB imetoa anuani na mawasiliano kama ifuatavyo; S.L.P. 1050, LINDI; Simu: (023) 2202734/2202744, na kwa wale watakaotaka kuwasiliana na ofisi za Makao Makuu Dodoma wanaweza kutumia S.L.P. 1049, DODOMA; Simu: 0734 047 775/0734 119 978; Barua pepe: info@chragg.go.tz
Jaji Mwaimu alikutana na Mkuu wa Mkoa wa Lindi ikiwa ni sehemu ya ziara yake katika Mikoa ya Kusini ambayo lengo lake kubwa ni kutembelea ofisi ya Tume iliyopo Mkoani Lindi ili kushughulikia malalamiko ya muda mrefu  yaliyowasilishwa  na wananchi katika ofisi hizo.
Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mheshimiwa Godfrey Zambi (kushoto) akimtambulisha Katibu Tawala wa Mkoa wa Lindi, Bi. Rehema Madenge (wa pili kushoto) kwa Mwenyekiti wa THBUB, Jaji (Mst.) Mathew Mwaimu (kulia) na ujumbe wake walipotembelea ofisi za Mkuu wa Mkoa huo

Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mheshimiwa Godfrey Zambi (katikati) akiagana na  Mwenyekiti wa THBUB, Jaji (Mst.) Mathew Mwaimu na ujumbe wake muda mfupi baada ya kumaliza mazungumzo yao Mei 18,2020. Kushoto ni Kaimu Katibu Mtendaji wa THBUB, Hajjat Fatuma Muya.
Afisa Mfawidhi wa THBUB Kanda ya Kusini, Bwana Noel Chiponde (kushoto) akimkaribisha Mwenyekiti wa THBUB, Jaji (Mst.) Mathew Mwaimu (katikati) katika ofisi ya Tume ilizopo Mkoani Lindi alipoitembelea Mei 18,2020 . Kulia ni Kaimu Katibu Mtendaji wa THBUB, Hajjat Fatuma Muya.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.