Mwenyekiti
wa THBUB, Jaji (Mst.) Mathew Mwaimu (kushoto) akiongea na Mkuu wa Mkoa wa
Lindi, Mheshimiwa Godfrey Zambi (kulia) alipomtembelea ofisini kwake
Na
Mbaraka Kambona,
Mwenyekiti
wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB), Jaji (Mst.) Mathew Mwaimu
ametoa rai kwa Wananchi wanaoishi katika Mikoa ya Kusini kutokaa na malalamiko na
badala yake yawasilishwe katika ofisi za
Tume ili yaweze kushughulikiwa.
Jaji
Mwaimu aliyasema hayo Mei 18, 2020 katika ziara aliyoifanya ya kutembelea ofisi
ya THBUB iliyopo Mkoani Lindi ambayo inahudumia mikoa yote ya kanda ya kusini
ikiwemo Lindi, Mtwara na Songea.
Katika
ziara hiyo Jaji Mwaimu alisema kipindi cha miaka miwili iliyopita Tume haikuwa
na uongozi kwa maana ya Makamishna jambo ambalo lilichangia baadhi ya kazi
kusimama lakini kwa sasa Tume imekamilika hivyo wananchi waendelea kuwasilisha
malalamiko yao ili waweze kusaidiwa.
“Niwaeleze
Wananchi kwamba Tume ipo, na ipo imara kuwasaidia, walete malalamiko yao
yanayohusu ukiukwaji wa haki za binadamu na utawala bora na sisi tunawaahidi
yatafanyiwa kazi kwa haraka”, alisema Jaji Mwaimu
Awali
akiongea na Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Mheshimiwa Godfrey Zambi alipomtembelea
ofisini kwake alisema kuwa kimsingi tume ni taasisi iliyoundwa kuisaidia
serikali kutatua kero za wananchi zinazohusiana na uvunjifu wa haki za binadamu
na misingi ya utawala bora nchini.
“Tume
ni jicho la serikali ambalo inalitumia kumulika na kubaini changamoto
zinazojitokeza hususani za masuala ya ukiukwaji wa haki za binadamu na misingi
ya utawala bora ili kuiepusha serikali kuingia katika migogoro isiyo ya lazima
na wananchi wake”, alieleza Jaji Mwaimu
Naye
Mkuu wa Mkoa wa Lindi alimueleza Jaji Mwaimu kuwa Mkoa wa Lindi unaendelea
kufunguka na kuna miradi mbalimbali inayoendelea kutekelezwa mkoani humo hivyo
sio vibaya wakaweka utaratibu wa kufuatilia miradi hiyo ili kujiridhisha kama
inatekelezwa kwa kuzingatia misingi ya haki za binadamu.
Aidha,
Jaji Mwaimu aliwapongeza Watumishi wa THBUB wa Kanda ya Kusini kwa kazi nzuri
wanayoifanya ya kuendelea kuhakikisha kuwa wananchi wa kanda hiyo wanapata
huduma nzuri na kwa wakati.
“Kwanza
mimi niwapongeze kwa kazi nzuri ambayo mmeendelea kuifanya pamoja na changamoto
mbalimbali mnazokabiliana nazo lakini mmeendelea kutoa huduma stahiki kwa
wananchi”, aliongeza Jaji Mwaimu
Wananchi wa Mikoa ya Kusini wamehimizwa kutumia ofisi za Tume zilizopo
katika Kanda hiyo ili iwe rahisi kwao kupata huduma, na kwa msaada zaidi THBUB
imetoa anuani na mawasiliano kama ifuatavyo; S.L.P. 1050, LINDI; Simu: (023)
2202734/2202744, na kwa wale watakaotaka kuwasiliana na ofisi za Makao Makuu
Dodoma wanaweza kutumia S.L.P. 1049, DODOMA; Simu: 0734 047 775/0734 119 978;
Barua pepe: info@chragg.go.tz
Jaji
Mwaimu alikutana na Mkuu wa Mkoa wa Lindi ikiwa ni sehemu ya ziara yake katika Mikoa
ya Kusini ambayo lengo lake kubwa ni kutembelea ofisi ya Tume iliyopo Mkoani
Lindi ili kushughulikia malalamiko ya muda mrefu yaliyowasilishwa na wananchi katika ofisi hizo.
Mkuu
wa Mkoa wa Lindi, Mheshimiwa Godfrey Zambi (kushoto) akimtambulisha Katibu
Tawala wa Mkoa wa Lindi, Bi. Rehema Madenge (wa pili kushoto) kwa Mwenyekiti wa
THBUB, Jaji (Mst.) Mathew Mwaimu (kulia) na ujumbe wake walipotembelea ofisi za
Mkuu wa Mkoa huo
Mkuu
wa Mkoa wa Lindi, Mheshimiwa Godfrey Zambi (katikati) akiagana na Mwenyekiti wa THBUB, Jaji (Mst.) Mathew
Mwaimu na ujumbe wake muda mfupi baada ya kumaliza mazungumzo yao Mei 18,2020.
Kushoto ni Kaimu Katibu Mtendaji wa THBUB, Hajjat Fatuma Muya.
Afisa
Mfawidhi wa THBUB Kanda ya Kusini, Bwana Noel Chiponde (kushoto) akimkaribisha Mwenyekiti
wa THBUB, Jaji (Mst.) Mathew Mwaimu (katikati) katika ofisi ya Tume ilizopo
Mkoani Lindi alipoitembelea Mei 18,2020 . Kulia ni Kaimu Katibu Mtendaji wa
THBUB, Hajjat Fatuma Muya.
No comments:
Post a Comment