Habari za Punde

Waziri Mhe.Mhagama Azindua Bodi ya Wadhamini wa Mfuko wa Fidia Kwa Wafanyakazi wa (WCF)

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu) Mhe. Jenista Joachim Mhagama (MB)  (kulia) akimkabidhi mkoba wenye Nyaraka mbalimbali, Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF). Bw. Emmanuel Humba, mara baada ya kuzindua Bodi hiyo mkoani Morogoro Oktoba 4, 2021

NA MWANDISHI WETU, MOROGORO                                                                                      

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu) Mhe. Jenista Joachim Mhagama (MB), amezindua Bodi ya Wadhamini ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) leo Tarehe 4/10/2021 Mjini Morogoro.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mhe. Jenista Mhagama amempongeza Mwenyekiti Mpya wa Bodi hiyo Bw. Emmanuel Humba kwa kuaminiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kuteuliwa kushika wadhifa huo na pia amewapongeza Wajumbe wa Bodi aliowateua na kuwataka waende kuusimamia Mfuko kwa kushirikiana na Menejimenti ili kufikia matarajio ya Serikali.

Wajumbe wapya wa Bodi walioteuliwa na Mhe. Waziri Jenista Mhagama ni pamoja na Ornorius John Njole, Perfect Raphael Kilenzi, Ibrahim Barnabas Mahuni, Abdulaziz Alladin Shambe, Rifai A. Mkumba, Raymond Kaseko, Julian C.N. Mpanduji, Rehema Rashid Ludanga na Felix Kagisa Rugarabamu.

Mhe. Jenista Mhagama amewataka wajumbe hao kuyaelewa vema majukumu yao kama yalivyoanishwa kisheria katika kifungu cha 13, 14, 15 na 16, na sehemu ya majukumu hayo ni pamoja na kusimamia maslahi ya wafanyakazi yanayotokana na kuanzishwa kwa sheria ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi.

 “ Kumekuwa na Mafanikio makubwa ya Mfuko katika kipindi hiki cha miaka sita na mnatakiwa kuyalinda kwa wivu na kwa nguvu zenu zote.” Alifafanua na kutoa mfano………katika kipindi ambacho bodi haikuwepo, thamani ya Mfuko imekuwa hadi kufikia shilingi za Kitanzania bilioni 445.49 kutoka thamani ya Mfuko  ya shilingi bilioni 112.83 mwaka 2016/2017,  huu ni ukuaji mkubwa sana na tunaona kuna kazi kubwa imefanyika, lindeni mafanikio haya.” Alisisitiza.

 Akizungumzia ulipaji wa Mafao, Mhe. Waziri Mhagama alisema kufikia mwaka 2020/2021 Mfuko ulilipa Mafao ya Wafanyakazi waliopata ajali kazini shilingi bilioni 12.43 ikilinganishwa na mwaka 2016/2017 ambapo zililipwa shilingi bilioni 1.55 tu.

Aidha aliwaasa Wajumbe wa Bodi kuelewa vema lengo la uwepo wa Mfuko ambapo ni kuhakikisha Wafanyakazi wanaoumia, Kuugua ama Kufariki kutokana na Kazi zao kwa mujibu wa Mikataba ya Ajira zao basi Serikali kupitia WCF iwalipe fidia au iwatibu na wakipona warejee kazini kuendelea na majukumu yao.

“Kubwa ni kuendelea kuweka mkazo kwenye utoaji elimu kwa waajiri na wafanyakazi ili waujue Mfuko na majukumu yake sambamba na kutoa mafunzo kwa madaktari wengi zaidi iwezekanavyo ili waweze kutoa huduma kwenye maeneo mengi ya nchi yetu, " alisema Mhe. Mhagama na kuongeza ......hivi sasa tunasema tuko kwenye uchumi wa viwanda, viashiria vingi vya uwepo wa ajali kazini na eneo mojawapo ni kwenye sekta ya Viwanda na Usafirishaj kwahiyo huduma za WCF zinahitajika sana katika kutoa hakikisho kwa wafanyakazi kuwa wachape kazi na hivyo kuongeza uzalishaji.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Bw. Emmanuael Humba alimuhakikishia Mheshimiwa Waziri Mhagama kuwa watahakikisha Mfuko unaendelea kutekeleza majukumu yake kulingana na malengo ya Mfuko na matarajio ya Serikali.

“Mashirika mengi yanakufa kutokana na kujisahau kwa waliopewa dhamana ya kusimamiwa mashirika haya, sisi ni wadhamini tu, na kwahiyo udhamini wetu lazima tuulinde kwa hali na mali kwa kutenda haki.” Alisema Bw. Humba.

Bw. Humba alimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kumuamini kuongoza Bodi hiyo na kutoa hakikisho ya kufanya kazi kwa uwezo wake wote.

“Naomba wajumbe wenzangu tuutendee haki uaminifu ambao Mheshimiwa Rais na Mheshimiwa Rais wametupatia kwa kufanya kazi kwa Weledi na bidii kwa hiyo nawaombeni tutende haki.” Alibainisha.

Awali Mkurugenzi Mkuu wa WCF Dkt. John Mduma alimpongeza Mwenyekiti wa Bodi Bw. Emmanuel Humba kwa kuaminiwa kupewa dhamana hiyo kwa kipindi cha pili lakini pia kuwapongeza wajumbe wote walioteuliwa na Mheshimiwa Waziri katika kuendesha gurudumu la Mfuko.

Alimpongeza Mhe. Waziri kwa kuteua wajumbe kwa kuzingatia kubakia kumbukumbu ya Taasisi kwa kuwabakisha wachache waliokuwepo na kuteua wengine wapya hali itakayosaidia kuufikisha Mfuko mahala panapostahili.

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu) Mhe. Jenista Joachim Mhagama
Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Bw. Emmanuael Humba 
Mkurugenzi Mkuu wa WCF Dkt. John Mduma, akitoa hotuba yake
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu) Mhe. Jenista Joachim Mhagama akimkabidhi nyaraka, Mjumbe wa Bodi Bi. Julian C.N. Mpanduji
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu) Mhe. Jenista Joachim Mhagama akimkabidhi nyaraka, Mjumbe wa Bodi Bi. Rehema Rashid Ludanga
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu) Mhe. Jenista Joachim Mhagama akimkabidhi nyaraka, Mjumbe wa Bodi Bw. Abdulaziz Alladin Shambe
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu) Mhe. Jenista Joachim Mhagama akimkabidhi nyaraka, Mjumbe wa Bodi Bw. Perfect Raphael Kilenzi
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu) Mhe. Jenista Joachim Mhagama akimkabidhi nyaraka, Mjumbe wa Bodi 
Bw. Raymond Kaseko
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu) Mhe. Jenista Joachim Mhagama akimkabidhi nyaraka, Mjumbe wa Bodi Bw.Ibrahim Barnabas Mahuni
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu) Mhe. Jenista Joachim Mhagama akimkabidhi nyaraka, Mjumbe wa Bodi Bw.Felix Kagisa Rugarabamu.
Meza Kuu na Wajumbe wa Bodi ya Wadhamini ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) baada ya kuzinduliwa mjini Morogoro Oktoba 4, 2021
Picha ya pamoja Meza Kuu na baadhi ya wafanyakazi wa WCF,

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.