Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais
inasimamia maeneo manne ya utekelezaji ambayo ni uratibu na udhibiti wa dawa za
kulevya, usimamizi wa mazingira na mabadiliko ya tabianchi, uratibu wa masuala
ya watu wenye ulemavu pamoja na uratibu wa juhudi za kupambana na ukimwi.
Ofisi ya Makamu ya Makamu wa Kwanza wa
Rais, inasimamia taasisi zifuatazo:-
i)
Ofisi ya Faragha ya Mhe. Makamo wa Kwanza wa Rais;
ii)
Idara ya Mipango, Sera na Utafiti;
iii)
Idara ya Uendeshaji na Utumishi;
iv)
Idara ya Mazingira;
v)
Baraza la Taifa la Watu Wenye Ulemavu;
vi)
Tume ya Kitaifa ya Uratibu na Udhibiti wa Dawa za
Kulevya;
vii) Tume
ya Ukimwi; na
viii) Mamlaka
ya Usimamizi wa Mazingira.
2.0
UTEKELEZAJI
WA MAJUKUMU
2.1
Usimamizi
wa Mazingira na Mabadaliko ya Tabianchi
i. Ofisi
imeendelea kudhibiti uchimbaji holela wa maliasili zisizorejesheka kwa kutenga
maeneo maalum kwa ajili ya shughuli za uchimbaji wa mchanga na kifusi. Jumla ya
maeneo 5 ya mchanga na 2 ya kifusi yamekaguliwa na kupewa ruhusa za kimazingira
za kuchimbwa rasilimali hiyo. Maeneo ya mchanga ni Donge Kipange, Donge
Mchangani, Pangatupu, Zingwezingwe na Matetema. Maeneo ya kifusi ni Jendele na
Fumba. Operesheni 35 za kusimamia
maliasili zisizorejesheka zimefanyika Unguja na Pemba kati ya operesheni 50
zilizopangwa kufanyika.
ii. Ofisi imeendelea kudhibiti uingizaji, biashara
na matumizi ya mifuko ya plastiki. Jumla ya tani 2.8 zimekamatwa na kuteketezwa
na watu 104 wamefikishwa katika vyombo vya kisheria. Hali hii inaonyesha kuendelea kuwepo
kwa wafanyabiashara ambao
wamekuwa wanaingiza na kuuza mifuko hiyo.
iii. Katika
kusimamia matumizi mazuri ya fukwe na bahari, maeneo 23 (13 Unguja na 10 Pemba)
yamefuatiliwa, kusafishwa na baadhi yao kupandwa mikoko. Maeneo hayo ni
Kilimani, Kisakasaka, Kibele, Nyamazi, Nungwi, Kiwengwa, Matemwe, Michamvi,
Jambiani, Kihinani, Paje, Makunduchi na Chukwani kwa upande wa Unguja na Mkoani, Ole
Kichanganazi, Mtangani, Kangani, Wambaa, Tundaua, Vumawimbi, Makangale,
Pangawatoro, na Kichanjaani kwa Pemba.
iv. Katika
kuzuia kuendelea kwa athari za mabadiliko ya tabianchi katika ukanda na ufukwe
wa pwani wa Msuka Magharibi uliopo Wilaya ya Micheweni Pemba, ukuta wenye urefu
wa mita 350 umejengwa ikiwa ni sehemu ya ukuta wa mita 500 unaokusudiwa
kujengwa. Aidha, misingi midogo ya
kupitisha maji ya mvua ndani ya ukuta huo wa mita 350 imekamilika.
v. Shughuli za kiuchumi zisizozingatia mazingira,
zimeendelea kufanyika katika mitaa na maeneo yetu hapa Zanzibar. Hali hii imepelekea kuwepo kwa kesi
32 (viwanda
vya matofali, magereji, maeneo ya kukata mbao na maeneo yanayofanya shughuli za
weldings) zinazohusiana na uharibifu na uchafuzi wa mazingira kwenye makaazi ya watu.
vi. Ofisi imeandaa Muongozo wa Kimazingira wa
uanzishaji na uendelezaji wa viwanda vya kusaga mawe, kifusi na utengenezaji wa
matofali. Kwa kushirikiana na Masheha,
tunakamilisha utaratibu wa jinsi gani shughuli hizo zifanyike bila ya kuwa na
athari za kimazingira katika maeneo ya kilimo, ufugaji, afya na makaazi kwa
ujumla.
vii. Ofisi
pia imeandaa Muongozo wa
Ufuatiliaji wa Kimazingira kwa ajili ya Hoteli za Kitalii. Muongozo huo
umelenga kuziwezesha Hoteli za kitalii kufanya ufuatiliaji binafsi katika
utunzaji wa mazingira. Kupitia Muongozo
huo Mamlaka ya Usimamizi wa Mazingira,
itaweza kuzifuatilia hoteli hizo ili kuimarisha
utunzaji wa mazingira na
kushajihisha utalii endelevu katika visiwa vya Zanzibar.
viii. Jumla
ya miradi ya kiuchumi na maendeleo 89 imefanyiwa
tathmini za kimazingira, kati ya miradi 99 iliyokuwa imepangwa. Tathmini hizo
zinahusu athari za kimazingira (miradi 40), ukaguzi wa kimazingira (miradi
tisa) na ripoti za kimazingira (miradi 40).
ix. Serikali
imenununa kifaa cha kukusanya taarifa za hali ya hewa ‘Automatic Weather
Station” na kufungwa katika eneo la Skuli ya Mohamed Juma Pindua; Mkoani Pemba
ili kuhakikisha taarifa za awali za hali ya hewa kwa ajili ya kuimarisha
uhimili wa mabadiliko ya tabianchi zinapatikana kwa wakati. Kifaa chengine kama
hicho kinategemewa kufungwa Makunduchi Unguja.
x.
Katika kuimarisha
usimamizi wa mazingira ya ukanda wa pwani ya Hifadhi ya Bahari ya Mkondo wa
Pemba (PECCA), Serikali imesafisha bwawa la maji machafu (Waste Water Treatment
Facility) lililopo eneo la Bandataka linapokea maji machafu yanayotoka katika
Shehia nne za Msingini, Chanjaani, Kichungwani na Madungu za Wilaya ya
Chakechake. Usafishaji huo ni katika hatua za awali katika kufanya marekebisho
ya mfumo wa bwawa hilo kwa ajili ya kuongeza ufanisi wa usafishaji wa maji
machafu ya bwawa hilo.
2.2
Udhibiti
na Usafirishaji wa Dawa za Kulevya
Zanzibar inakadiriwa kuwa na vijana zaidi ya 10,000 ambao wamo katika
matumizi ya dawa za kulevya. Hadi mwishoni
mwa mwaka 2020, watu ambao wako katika nyumba za upataji nafuu ni 349. Katika
kuimarisha mapambano dhidi ya uingizaji, ulimaji, usambazaji na utumiaji wa
dawa za kulevya, Serikali imetekeleza yafuatayo:-
i.
Rasimu ya sheria mpya ya Udhibiti wa Dawa za Kulevya
imeandaliwa na inatarajiwa kuwasilishwa katika kikao cha Baraza la Wawakilishi
cha mwezi wa Disemba 2021. Sheria hiyo mpya itaiwezesha Mamlaka ya Udhibiti na
Usimamizi wa Dawa za Kulevya kuwa na nguvu
kisheria za kupambana na dawa za kulevya. Kupitia sheria hiyo, tutakuwa na
maabara ya pamoja ambayo itahakikisha kwamba tunabaini uhalifu mapema zaidi,
pamoja kuwa na kikosi maalumu ambacho kitakuwa na kazi ya kusimamia udhibiti wa
uhalifu huu. Lengo letu pia ni kufupisha muda wa usikilizaji wa kesi
zinazohusiana na dawa za kulevya.
ii.
Katika kuimarisha udhibiti wa dawa za kulevya zisirudi tena
mitaani, jumla ya kilogram 94.573 zimeteketezwa. Dawa hizo ni bangi, heroini,
kokeni na mirungi. Aidha, tumepitia upya
muongozo wa uteketekezaji wa dawa hizo kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkurugenzi
wa Mashtaka na Mrajis wa Mahakama Kuu. Hatua kadhaa zinaendelea kuchukuliwa,
zikiwemo za udhibiti wa ushahidi wa dawa na usimamizi imara zaidi.
iii.
Katika kupunguza usambazaji na matumizi ya dawa za
kulevya, operesheni 52 zilifanyika katika mitaa iliyobainika kuwa ni hatarishi
zaidi kwa pindi hiki. Mitaa hiyo ni Kikwajuni, Sogea, Kidongochekundu,
Miembeni, Chuini, Jangombe, Migombani, Maeneo ya Mji Mkongwe kwa Wilaya ya
Mjini, Nungwi, Chakechake, Pujini, Wete, baadhi ya maeneo ya Makunduchi
(Kijini, Miwaleni na Mtegani) na maeneo yote yanayofanyika shughuli za utalii.
Doria za mara kwa mara zitaendelea kufanyika ili kupunguza matumizi na biashara
ya dawa za kulevya mitaani na kuimarisha mashirikiano baina ya wananchi na
Serikali katika kupunguza wimbi la usambazaji wa dawa za kulevya.
iv.
Ofisi imebaini ongezeko la matukio 52 (sawa na asilimia
15) ya ukamataji ambapo ujumla ya matukio 393 yameripotiwa kwa kipindi cha
Januari – Septemba 2021 ikilinganishwa na matukio 341 yaliyoripotiwa katika
kipindi kama hicho kwa mwaka uliyopita. Matukio hayo yamepelekea kukamatwa kwa
8.5kg za heroine na kufunguliwa kwa kesi 168, sawa na ongezeko la kesi 19
ikilinganishwa na mwaka uliopita ambapo gramu 761 za heroine zilikamatwa na
kufunguliwa kesi 149. Aidha, jumla ya kilogramu 189.3 za bangi zilikamatwa na
kufunguliwa kwa kesi 220, sawa na ongezeko la kesi 5 ikilinganishwa na mwaka
uliopita ambapo kilogramu 39 za bangi zilikamatwa na kufunguliwa kesi 189.
Vilevile, 180g za mirungi zilikamatwa na kufunguliwa kesi 5. Jumla ya gramu 191
za skanka zilikamatwa na kufunguliwa kesi 2.
v.
Ofisi, inakamilisha Ujenzi wa
Nyumba ya Kurekebisha Tabia iliyopo Kidimni kwa lengo la kuimarisha upatikanaji
wa huduma za afya kwa walioamua kuachana na dawa za kulevya na kujenga uwezo
wao wa kichumi kwa kuwapa nyenzo za elimu na mafunzo ya stadi za maisha kabla
ya kurudi kuungana na jamii katika shughuli za kiuchumi. Kwa upande wa Pemba, imefanikiwa
kupata eneo kwa ajili ya ujenzi wa Kituo kama hiki katika kijiji cha Kiembe
Raha, Kangagani. Uwepo wa vituo hivi utapunguza unyanyapaa na kuzidisha
kukubalika kwa vijana hao ambao wameamua kuachana na matumizi ya dawa za
kulevya.
vi.
Ofisi imefanikiwa kuanzisha huduma ya simu ya bure
(free line) kwa ajili ya kuripoti taarifa za uhalifu wa dawa za kulevya. Kwa
sasa, jamii inawasiliana na Tume moja kwa moja kupitia namba ya
bure ya 0774 33 33 00 au kupitia simu binafsi za viongozi na watendaji wa Tume.
Kupitia huduma hii, Ofisi tayari imeshapokea taarifa 37 na inaendelea
kuzifanyia kazi. Huduma hii inawarahisishia wananchi kutoa taarifa zao juu ya
uhalifu kwa usiri na kwa haraka jambo ambalo limerejesha imani kwa wananchi
katika kutoa taarifa.
vii.
Ofisi imeendesha mafunzo ya ulinzi na usalama wa
bandari (port security) kwa maafisa kutoka taasisi mbalimbali zinahusika na
ulinzi na usalama wa bandari zikiwemo TRA, KMKM, Jeshi la Polisi, ZMA, ZAECA,
Zimamoto na Uokozi, na Afisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka. Mafunzo hayo yalilenga
kuimarisha ulinzi na ukaguzi wa abiria na mizigo bandarini.
viii.
Jumla ya Asasi Zisizo za
Kiserikali 15 zinashirikiana na Ofisi yangu katika mapambano dhidi ya matumizi
na biashara ya dawa za kulevya na kutoa elimu kwa jamii.
2.3
Uratibu
wa masuala ya UKIMWI
Kufikia Juni 2021, Zanzibar inakadiriwa kuwa na watu 8,147
wanaoishi na virusi vya ukimwi ambapo wanawake ni 5,621 na wanaume ni 2,526.
Katika kipindi cha mwaka mmoja, Ofisi imetekeleza yafuatayo:-
i.
Upimaji wa hiari umeongezeka hususan kwa vijana ambapo
jumla ya vijana 3,098 walipima VVU (1,577 wanaume na 1,521 wanawake) na mmoja
tu kati yao aligundulika kuwa na maambukizo ya VVU. Katika kipindi kama hicho
mwaka uliopita, vijana 833 tu ndio waliweza kuhamasika kupima kwa hiyari ambapo
wanaume ni 562 na wanawake ni 271.
ii.
Zanzibar bado inakabiliwa na tatizo la unyanyapaa kwa
wanaoishi na VVU. Ofisi imeendelea kutoa elimu juu ya athari za unyanyapaa kwa
njia ya sanaa shirikishi katika shehia 9 za Wilaya ya Micheweni, Mkoa wa
Kaskazini Pemba. Aidha, tunaendelea kuhakikisha kuwa masuala ya UKIMWI
yanazingatiwa katika sekta zote kwa kuhamasisha Wizara, Taasisi za Serikali na
Binafsi pamoja na Mashirika ya Umma kuwa na programu za kupambana na maradhi ya
UKIMWI ili kudhibiti maambukizo mapya ya VVU kwa jamii yetu. Kwa sasa, tunashirikiana
na Asasi Zisizo Za Kiserikali 47 kwa ajili ya kuendelea na kazi hizo.
iii.
Asilimia kubwa ya maambukizo yapo kwa makundi maalum
yakiwemo wanawake wanaofanya baishara ya miili yao (12.1%), wanaotumia dawa za
kulevya kwa kujidunga (5.1%) na wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume wenzao
(5%). Kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na Wizara ya Afya mwaka 2018, jumla ya
wanawake 5,554 (4,854 unguja, 700 Pemba) wanakisiwa kujihusisha na biashara ya
kuuza miili yao, wanaume 3,300 (3,000 Unguja na 300 Pemba) wanajihusisha na
uhusiano wa jinsia moja na watu 2,600 (2,200 Unguja, 400 Pemba) wanakisiwa
kutumia dawa za kulevya kwa njia ya kujidunga sindano. Ofisi imeendelea na
jitihada za kuyafikia makundi hayo kwa lengo la kuyapa elimu na kupima
maambukizo ya VVU kupitia programu za masafa (outreach) Unguja na Pemba. Hadi
kufikia Septemba 2021, jumla ya watu 10,378 wa makundi maalumu wamefikiwa na
6,424 walikubali kupima VVU ambapo 69 waligundulika na maambukizo ya VVU.
iv.
Kuanzia Julai 2020 hadi Juni 2021 jumla ya mama wajawazito
56,165 wamefanyiwa uchunguzi wa VVU ambapo kati yao 104 (0.2%) waligundulika na
VVU. Aidha watoto 381 waliozaliwa na mama wajawazito walichunguzwa afya zao na
5 waligundulika na maambukizo ya VVU ikiwa ni sawa na asilimia 1.3. Katika
kudhibiti maambukizo ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto kiwango cha
maambukizo chini ya asilimia 5 kinachukuliwa kama ni ishara ya ufanisi katika
kuwalinda watoto na maambukizo kutoka kwa mama zao.
v.
Katika kuibua mbinu za kudhibiti mazingira hatarishi
yanayoweza kupelekea kuongezea kwa maambukizo ya VVU, Ofisi kwa kushirikiana na
Tawala za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa Unguja na Pemba imeweka
utaratibu kudhibiti upigaji wa ngoma na muziki; kufungia kabisa utoaji wa
vibali vya ngoma kwa baadhi ya maeneo; kufungia baa na nyumba za kulala wageni
na hoteli zinazoendeshwa kinyume na utaratibu au zinazochochea tabia hatarishi;
pamoja na kudhibiti bandari zisizorasmi kwa kusimamia uingiaji wa wageni
wasiokuwa na shughuli zinazoeleweka.
vi.
Elimu ya kuhamasisha mabadiliko ya tabia katika jamii
imeendelea kutolewa kupitia vyombo vya habari, mikutano, machapisho,
vipeperushi na mitandao ya kijamii ya Instagram, youtube na facebook.
2.4
Usimamizi
wa masuala ya Watu wenye Ulemavu
Zanzibar inakisiwa kuwa na idadi ya watu wenye Ulemavu
74,500. Hata hivyo, Mfumo wa kidigitali wa Baraza la Taifa la Watu wenye
Ulemavu (Jumuishi Database), umefanikiwa kusajili watu 8,488 wenye ulemavu
wakiwemo wanawake 4,043 na wanaume 4,445. Ili kuhakikisha kwamba haki na fusra
zinapatikana kwa Watu wenye Ulemavu, yafuatayo yametekelezwa:-
i.
Ofisi imeimarisha Jumuishi Database kwa kuanzisha
moduli ya usajili wa visaidizi (Asset Register) vinavyotolewa kwa wenye ulemavu
ili kuleta ufanisi katika utoaji wa visaidizi hivyo na kuweka kumbukumbu sahihi
za watu waliopatiwa visaidizi.
ii.
Jumla ya visaidizi 302 vya aina mbali mbali vimetolewa,
kati ya hivyo visaidizi 104 vimepelekwa Pemba ambavyo wamepewa wanawake 56 na
wanaume 48 na visaidizi 198 vimetolewa Unguja ambavyo wamepatiwa wanawake 113
na wanaume 85. Visaidizi hivyo ni viti vya magurudumu miwili 94, fimbo nyeupe 7
na kigari kimoja cha kisasa kinachotumia umeme.
iii.
Katika kupunguza wimbi la vitendo vya unyanyasaji kwa
Watu wenye Ulemavu, ofisi imepokea na kufuatilia malalamiko 6 ya udhalilishaji
Unguja na Pemba na kupelekea kesi 5 kufunguliwa mahakamani ambapo 3 zinaendelea
kusikilizwa, mtuhumiwa mmoja ametiwa hatiani na 2 zinaendelea na uchunguzi wa
polisi.
iv.
Katika kuimarisha zaidi usimamizi wa fursa na haki za
watu wenye ulemavu, Ofisi imefanya mapitio ya awali ya Sheria ya Watu wenye
Ulemavu (Haki na Fursa) No.9 2006 ambapo rasimu yake inaendelea kupata maoni ya
wadau. Ofisi inaamini kuwa marekebisho ya sheria hii yataongeza ufanisi katika
utoaji wa haki na fursa kwa Watu wenye Ulemavu pamoja na kuimarisha
ukondoishaji wa masuala ya Watu wenye Ulemavu katika sekta mbalimbali
zinazogusa maisha yao hali itakayoongeza kasi ya kuwafanya waishi maisha bora
zaidi.
v.
Ili kuhamasisha uelewa juu ya haki
na fursa za watu wenye ulemavu, Ofisi inashirikiana na Taasis Zisizo za
Kiserikali 10 kuhamasisha marekebisho ya miundombinu ya majengo hususan ya
Serikali kwa ajili ya kuweza kufikika kwa urahisi zaidi. Aidha, miundombinu ya
barabara ambayo inaendelea kurekebishwa hususan kuwekwa kwa njia za watembea
kwa miguu (walkways), kumesaidia kwa kiasi kikubwa kwa watu wenye ulemavu
kupunguza vihatarishi vilivyokuwa vikitokea hapo awali katika barabara zetu.
2.5 Usikilizaji na
utatuzi wa kero na malalamiko ya Wananchi
i.
Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais, imeanzisha utaratibu
wa kuwasikiliza wananchi mbalimbali na kupatiwa ufumbuzi wa hoja zao. Ofisi
imefanikisha kupatiwa suluhu ya mgogoro wa ardhi kati ya wananchi wa Nungwi na
Serikali ya Mkoa. Aidha, malalamiko ya wananchi wa Kendwa kuhusu kuchukuliwa
eneo la soko, yanaendelea kufanyiwa kazi. Ofisi pia ilisimamia na hatimaye
kuupatia suluhisho mgogoro baina ya mwekezaji wa kiwanda cha kusaga kokoto na
wakulima wa Shehia ya Mwambe, Pemba.
ii.
Katika kuweka mbele masuala yenye maslahi kwa umma,
Ofisi imefuatilia na kuyafanyia kazi malalamiko ya wananchi dhidi ya wamiliki
wa viwanda vinavyofanya shughuli zao katika maeneo ya makaazi ya watu na kuleta
kero kwa wananchi. Hatua zilizochukuliwa ni pamoja na kuzuia ujenzi wa kiwanda
cha kuzalisha waya za umeme cha kampuni ya ZANTEXAS LTD katika maeneo ya Bweleo
baada ya mjenzi kuthibitika kutokuwa na vibali vya mazingira na ZIPA pamoja na
kuleta athari za kiafya na kimazingira kwa wanajamii wanaoishi jirani na
kiwanda hicho.
iii.
Ili kuimarisha mawasiliano yake na umma, Ofisi inatumia
mitandao ya kijamii kwa kutoa taarifa na kupokea maoni ya wananchi kupitia
“facebook”, “instagram” na tovuti yenye anuani ya www.omkr.go.tz
.
iv.
Ofisi pia imeendelea kuyafanyia kazi malalamiko
mbalimbali yanayowasilishwa katika mfumo wa “Sema na Rais” ambapo malalamiko 13
yamepokelewa, 6 kati ya hayo yamepatiwa ufumbuzi na 7 yanaendelea kufanyiwa
kazi.
v.
Ofisi imeandaa Mkataba wa Huduma kwa Mteja (Customer
Service Charter) ikiwa ni hatua ya kuimarisha mfumo wa utoaji wa huduma za
Ofisi.
vi.
Hatua za kupunguza athari za Uviko 19 kwa watumishi wa
umma zimeendelea kuchukuliwa kwa kuwajengea uelewa watumishi 273 juu ya
kujikinga na maambukizo ya Uviko 19 kwa lengo la kupunguza na kukabiliana na
maradhi hayo kwenye maeneo ya kazi na jamii kwa ujumla. Aidha, vifaa vya
matumizi kwa ajili ya kinga ikiwemo vitakasa mikono (sanitizers) vimewekwa katika
maeneo ya ofisi.
3.0
CHANGAMOTO
1. Ukosefu wa vifaa vya kisasa vya utambuzi
wa dawa za kulevya katika viwanja vya ndege na bandari Unguja na Pemba.
2. Baadhi
ya Watu wenye Ulemavu kushindwa kupata matibabu kutokana na kutomudu gharama za
matibabu pamoja na uhaba wa dawa hospitalini kwa wenye ulemavu mchanganyiko.
3. Maradhi ya UKIMWI kuzoeleka na kuonekana
si tatizo tena katika jamii jambo linalopelekea kuongezeka kwa tabia na
mazingira hatarishi pamoja na maambukizo
ya VVU.
4. Umwagaji ovyo wa maji machafu
yanayotapishwa kwenye vyoo na makaro katika Manispaa ya Zanzibar.
5. Kuendelea kuwepo shughuli za uchimbaji
holela wa mchanga na maliasili nyengine zisizorejesheka
4.0
HITIMISHO
Ofisi itaendelea na jitihada za kusimamia
masuala ya usimaizi wa mazingira na mabadiliko ya tabianchi, udhibiti wa dawa
za kulevya, mapambano dhidi ya UKIMWI na kulinda haki na fursa kwa watu Wenye
Ulemavu ili kuinua uchumi na kuimarisha upatikanaji wa huduma mbalimbali kwa
wananchi kupitia dhana nzima ya Uchumi wa Buluu.
No comments:
Post a Comment