Habari za Punde

Dk. Mwinyi - Kuongezeka kwa idadi kubwa ya Wahitimu wa masomo ya fani mbalimbali chuoni hapo ni hatua za maendeleo zilizofikiwa na chuo hicho.

 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi ambae pia ni Mkuu wa Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA) Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akihutubia katika hafla ya Mahafali ya 18 ya Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA) mahafali hayo yaliyofanyika katika ukumbi wa Dk.Ali Mohamed Shein Tunguu Wilaya ya Kati Unguja leo 28-12-2022

SERIKALI  ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema inaongeza jitihada za kukiendeleza Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA), kuwa chuo bora zaidi katika kuwaandaa vijana wenye umahiri na weledi kitaaluma na ubunifu wa kuzitambua fursa na kuzitumia ipasavyo.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, ambae ni Mkuu wa Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA), Dkt. Hussein Ali Mwinyi aliyasema hayo kwenye mahafali ya 18 ya chuo hicho yaliyofanyika katika ukumbi wa Dkt. Ali Mohamed Shein Tunguu, Mkoa wa kusini Unguja, leo Disemba 28, 2022.

Dkt. Mwinyi alisema kuongezeka kwa idadi kubwa ya wahitimu waliofaulu masomo ya fani mbalimbali chuoni hapo ni hatua za maendeleo zilizofikiwa na chuo hicho.

Alisema kwa mwaka huu  2022 idadi ya wahitimu imeongezeka kufikia 1913 ikilinganioshwa na 1894 waliohitimu mwaka jana hatua aliyoipongeza kwa tasisi ya elimu ya juu SUZA kwa mafanikio ya kuzalisha wasomi wa fani mbalimbali ambazo alizitaja kuwa ni nguvu kazi na chachu ya kusukuma mbele maendeleo ya Zanzibar.

Wakati huo huo, Dkt. Mwinyi alitumia fursa hiyo kuwapongeza wahitimu kwa hatua waliyofikia sambamba na kuwasahauri kuitumia vyema elimu waliyoipata hapo kwa munufaa yao na taifa kwa ujumla.

“Nachukua fursa hii kukupongezeni kwa mafanikio hayo ya kitaalima ambayo chuo chetu  kinaendelea kuyapata” alipongeza Dkt. Mwinnyi.

Akizungumzia suala la ushirikiano baina ya Chuo Kikuu cha taifa cha Zanzibar (SUZA) taasisi nyengine za elimu ya juu za ndani na nje, ikiwemo Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali pamoja na wadau wengine wa Elimu, Dkt. Mwinyi alieleza hatua hiyo itafanikisha azma ya kuleta mageuzi katika sekta ya elimu kuanzia elimu ya awali hadi elimu ya juu.

“Tutoe wahitimu wenye uwezo wa kuhimili ushindani uliopo kwenye soko la ajira  kwa kutumia elimu walioyoipata” alisema Dkt. Mwinyi.

Aidha, alikishauri chuo hicho kuzipatia ufumbuzi wa haraka changamoto zinazopitia ili kutekeleza majukumu yake ipasavyo.

Hata hivyo, Dkt. Mwinyi alieleza kuwa serikali inaendelea kuunga mkono jitihada zinazochukuliwa na chuo hicho kwa kuwapatia misaada ya hali na mali kwa kadri hali inavyoruhusu.

“Hata hivyo, bado naendelea kusisitiza haja ya kutafuta njia mbadala za kupata fedha ikiwemo kuchukua mikopo na kuanzisha miradi ya maendeleo itakayoleta faida kwa chuo” alieleza Dkt. Mwinyi.

Kuhusu suala la uhaba wa rasilimali watu unaokikabili chuo hivyo, Rais Dkt. Mwinyi alieleza haja ya serikali kuajiri watumishi ili kuongeza nguvu katika taasisi za elimu za elimu ya juu wakiwemo wahadhiri, wakutubi na wataalamu wa maabara na watumishi wa fani ili kukidhi viwango vya ubora wa elimu ya juu nchini sambamba na kuimarisha mazingira bora ya kufanyia kazi.

Akizungumza kwenye Mahafali hayo, Waziri wa Elimu na  Mafunzo ya Amali, Lela Mohamed Mussa, alisema juhudi za serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni kutoa vijana wasomi watakaokuwa na uwezo wa kujiajiri na kuzikimbilia fursa ili kupunguza msongo mkubwa kwa seikali na wazazi.

Alisema jitihada za Chuo Kikuu cha taifa SUZA ni kuzaliwa wasomi watakaochochea maendeleo chanya nchini.

Nae Makamu mkuu wa chuo hicho Prof. Moh’d Makame Haji alisema chuo kinampango wa kujenga jengo la sayansi ya bahari lenye nia ya kuendeleza dhana ya Uchumi wa Bluu nchini ambalo alilieleza kwamba fedha zake tayari zimeidhinishwa na serikali.

Imetayarishwa na Idara ya Mawasiliano

Ikulu Zanzibar.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.