Habari za Punde

Vipi tuwe tutakapojaaliwa kukutana na Ramadhaan





Assalamu'alaykum Warahmatu Llahi Wabarakatuh,

Shukrani zote ni zake Muumba wa mbingu na aradhina, Muumba aliyezitukuza siku chache za mgeni wetu Ramadhaan kwa kujaaliya mambo mengi ndani yake, Muumba aliyemtunuku Ramadhaan zawadi tukufu ya kuwa ndio wakati aliouchagua wa kuyaleta/kuyashusha maneno yake matukufu, ambayo ni uongozi na uongofu kwa viumbe wote, Qur-an inasema:

Mwezi wa Ramadhaan ambao imeteremshwa humo Qur'ani kuwa ni uwongofu kwa watu, na hoja zilizo wazi za uwongofu na upambanuzi..” Al-Baqarah  aya ya 185.

Rehma na Amani za Allah zimfikie Al-Habibi Musttafa (Salla Llahu 'Alayhi Wa'ala Alihi Wasallam) na kila aliyejaaliwa kufuata na kushikamana na mafunzo yake sahihah, yeye al-Habibu Musttafa (Salla Allahu 'Alayhi Wa’ala Alihi Wasallam) amepokelewa –Hadithi Qudsy- akisema kuwa: Allah amesema:
“Kila ‘amali anayoifanya mwanadam huengezewa, jema moja kwa kumi mpaka mia saba, na halafu huengezwa kwa atakavyo Allah, isipokuwa sawm (funga), hiyo (sawm/funga) ni Yangu Mimi, na Mimi ndiye Mlipaji wake ….” Imepokelewa na Muslim, kitabu cha sawm, mlango wa fadhila za sawm.

Ndugu zangu wapenzi katika imani, napenda kujiusia nafsi yangu kwanza na nasfi zenu kumcha Allah na kumtii, kwa kutekeleza kila aliloliamrisha kadiri ya uwezo wetu, na kujikataza na kila alichokikataza mara moja.


Ndugu zangu katika imani, Ramadhaan ni mgeni aliyejenga uhusiano mzuri na wenye nguvu na Waislamu wa kila zama, kwa njia ya kuwatembelea katika nyumba zao kwa kukaa na kuiishi nao kwa wakati wote wa kipindi cha mwezi mzima.  Mgeni huyu ndiye yule yule aliyewahi kuwatembelea na kukutana uso kwa uso mara karibu tisa na al-Habibi Musttafa (Salla Llahu ‘Alayhi Wa’ala Alihi Wasallam), kipenzi chetu na kipenzi cha wote wenye kumtarajia Allah na Siku ya Mwisho na wakamkumbuka Allah sana, mgeni huyu aliwahi pia kuwatembelea Sahaba (Radhiya Llahu ‘Anhum) na waislamu wote wa karne zilizopita, na ni huyu huyu ataewatembelea insha Allah kwa uwezo wake Mola waislamu wa karne zitakazokuja baada yetu tutakapokuwa chini ya tani za udongo.

Twamuomba al Hayyu al Qayyuum atusamehe makosa yetu na madhambi yetu makubwa na madogo, ya mwanzo na ya mwisho, tuliyoyafanya kwa dhahiri na kwa siri, na aturuzukuku maghfirah na tawbah kabla ya kuiaga dunia hii yenye kutushughulisha karibu wengi wetu, na tukutane naye hali ya kuwa ni waislamu waliosamehewa na waliokubalia tawbah zao insha Allah, Amin Amin Amin.
Ndugu zangu katika iman, ni miongoni mwa mambo yaliyozoeleka kuwaona Waislamu wa kila nchi, miji, vijiji na mitaa kujiwekea wakati wa kukumbushana na kuelezana namna ya kumpokea mgeni huyu mtukufu kama ni matayarisho na mapokezi yake. Hivyo utaona kwa mfano mihadhara kama sisi hapa leo kwa fadhila, rehma na uwezo wa Jabbaar tumekutana kwa hilo, au maandishi kwa wenye kutumia mtandao yenye kubeba anuani kama zifuatazo:

            Namna ya kuikaribisha Ramadhaan
            Vipi Tuikaribishe Ramdhan
            Mambo ya kuikaribisha Ramadhaan
            Njia kumi za kuukaribisha vizuri Ramadhaan

Ndugu zangu katika iman, yote haya na mengine kama haya huwa na lengo la kuwataka waislamu kujiandaa na kujitayarisha kwa kujiweka tayari kumpokea mgeni wao mtukufu kwa namna au njia inayokubaliwa na Allah na Mtume wake (Salla Llahu 'Alayhi Wa'ala Alihi Wasallam).

Ndugu zangu katika imani, matayarisho ya kumpokea mgeni ni ya namna nyingi, hasa hasa kwa kuwa mgeni wenyewe ni ‘adhimu na ni mwenye ku’adhimishwa na kila mwenye kuamini Allah na Siku ya Mwisho, kwani wao pekee ndio waliotajwa na kuainishwa katika Qur-an, kuwa wamependekezewa mgeni afikie makwao, wakae nae na kuishi nae kwa kuchunga na kuhifadhi mipaka yake, wametajwa na kuainishwa kwa jina au sifa wanayoipenda wanasibishwe nayo bali ndio identity yao katika uhai wao huu na ujao insha Allah, kinachojitokeza hapa ni vipi sisi tutamkaribisha/tumkaribishe Mgeni huyu, mgeni ambae wenyeji wake ni watu maalum, kama inavyothibitisha Qur-an, Allah anasema:

Enyi mlio amini! Mmeandikiwa Saumu, kama waliyo andikiwa walio kuwa kabla yenu ili mpate kumcha Mungu “ al-Baqarah aya ya 183,

Ndugu zangu katika imani, muhadhara wenye anuani kama hii huwa na lengo la kutupelekea kuwa na hamu na shauku ya kujiweka tayari kwa tawfiq na uwezo wa Mola wa Ramadhaan kumpokea mgeni, lakini kwa kuwa wenyeji wake ni wale wenyekupenda kunasibishwa na sifa au kuainishwa kwa jina maalum (walioamini), jambo hili hupelekea tukawa na makundi ya watu yenye fikra na mawazo tofauti katika kumpokea mgeni Ramadhaan, hivyo kuwasili kwake kunawagawa waislamu (sio waumini) katika makundi mengi yakiwemo yafuatayo:
1) Wanaompokea mgeni kwa moyo uliojaa furaha kwa kuwa Allah amewapendekezea mgeni na akawafiqisha kuweza kukutana na mgeni wao Ramadhaan baada ya wengi miongoni mwao kuiaga dunia.
2) Wanaompokea mgeni kwa manung’uniko na masikitiko kwa kuwa mgeni huyu atawanyima starehe zao na atapekelea baadhi ya matamanio yao kutopatikanwa, bali ni maudhi na mateso tu hakuna jipya, kwanini watu wafunge/tufunge na kujizuilia kula na kunywa! Bali hata hufikia kusema kuwa hivyo kweli Allah ameipendekeza Sawm kwa watu, jambo ambalo linapelekea kuingiliana katika mambo binafsi na uhuru na matakwa ya mtu.
3) Wanaompokea mgeni kwa michezo na kila lenye kupoteza wakati, (kupitisha masaa) kwao wao kuja kwa Ramadhaan ni jambo la kawaida na ni katika mila na desturi za jamii wanazoishi, lililo muhimu kwao ni kuonekanwa umefunga (huli, hunywi, waweza kufanya uyatakayo kama kawaida yako jihadhari asikuonwe na maustadhi na wapika majungu) hakuna jipya isipokuwa kushinda na njaa, kwani majumba mengi huwa hawapiki, kwa ufupi ni mwezi wa kushinda na njaa.
4)  Wanaompokea mgeni kwa wasi wasi na shaka, huku wakijaribu kujitetea na kutaka kuonekanwa kuwa moderate, kwani wanachokifanya (funga) si jambo geni, wala hakuna tofauti na wengine, kwa kuwa linafanywa pia na wengine wenye dini (Manasara, Mayahudu, na kila mwenye kujidai kuwa ana siku katika dini yake za kufunga), hivyo hakuna jipya.
Je mimi na wewe tumo katika kundi lipi? Tujipime kulingana na Ramadhaan tulizokutana nazo na yakaribu kabisa ni ya mwaka jana.  Je mwaka huu mgeni ndio huyo yuko kizingitini, tunapenda tuwemo au kuingia/kujiingiza katika kundi lipi? Lenye kupenda kunasibishwa na jina la waliotakiwa waishughulikie Ramadha kwa kuchunga, kuheshimu na kuhifadhi mipaka yake kulingana  na mafundisho ya al-Habibi Musttafa (Salla Llahu 'Alayhi Wa'ala Alihi Wasallam) au makundi yasiyopenda kuainishwa na kunasibishwa na jina/sifa waliyonasibishwa nayo waliopendekezewa Ramadhaan?
Ndugu zangu katika imani, mgeni yo yote yule utaelewa hadhi yake na umuhimu wake kwa mwenyeji/wenyeji wake kutokana na matayarisho/maandalizi na mapokezi yake, ndio sisi tukawa na anuani kama hii Vipi tumkaribishe Ramadhaan,  na ili tuelewa namna gani anahitaji kupokewa na kukaribishwa huyo mgeni wetu Ramadhaan, ni vyema kwanza umuelewe/tumuelewe Ramadhaan wenyewe ni nani? na baada ya hapo ndio upange, wewe na sio mimi, namna ya kumpokea na kumkaribisha, kwani si jambo la kawaida kuwa mgeni wako na atakuwa nyumbani kwako, bali atakuwa na wewe muda wa mwezi mzima katika masaa ishirini na nne (24) yako ya kila siku yako, aje atokea mtu mwengine nje, akupangie namna ya kumkaribisha!, labda awe mtu wako wa karibu sana kama vile rafiki/shoga yako na kadhalika.
Ndugu zangu katika imani, hata hivyo sisi leo hapa tuko katika kukushauri/kushauriana kuwaidhiana kupeana fikra na mawazo kupendekezeana juu ya jinsi ya kumkaribisha Ramadhaan, na mwisho wa hayo wewe ndie muamuzi wa mwisho, hivyo suala ni hili, unamuelewa vyema mgeni wako? Kama kweli unamuelewa, basi vipi umepanga kumpokea? kama umejipangia, na kama bado, je uko tayari kusikiliza mapendekezo yangu? Mapendekezo ambayo kwa kweli hayana uzuri wo wote kuliko yale utakayojiwekea wewe mwenyewe kwa hiari yako.
Ndugu zangu katika imani, Ramadhaan au mgeni wako (wetu) mpenzi yuko hivi kama alivyoelezwa na Mola wake, Allah anasema:
Mwezi wa Ramadhaan ambao imeteremshwa humo Qur-aan kuwa ni uongofu kwa watu, na hoja zilizo wazi za uongofu na upambanuzi. Basi ataye kuwa mjini katika mwezi huu na afunge. Na mwenye kuwa mgonjwa au safarini, basi atimize hisabu katika siku nyengine. Mwenyezi Mungu Anakutakieni yaliyo mepesi wala Hakutakieni yaliyo mazito, na mtimize hiyo hisabu, na mumtukuze Mwenyezi Mungu kwa kuwa Amekuongoeni ili mpate kushukuru” Al-Baqarah: aya ya 185, pia al-Habibu Musttafa (Salla Allahu 'Alayhi Wa’ala Alihi Wasallam) amesema:
“Mwenye kufunga Ramadhaan (kama inavyotakiwa na sio kukaa na njaa) kwa iman na kutaraji malipo, atasamehewa madhambi yake yote yaliyotangulia” Imepokelewa na Bukhar, kitabu cha saum, mlango wa mwenye kufunga Ramadhaan kwa iman, pia al-Habibu Musttafa (Salla Allahu 'Alayhi Wa’ala Alihi Wasallam) amesema:
"Inapoingia Ramadhaan, milango ya Pepo hufunguliwa na milango ya Moto hufungwa, na mashetani hufungwa …" Imepokelewa na Muslim, kitabu cha saum, mlango wa fadhila za mwezi wa Ramadhaan,
Ndugu zangu katika imani, miongoni mwa mambo yanayotupelekea kuwa na mihadhara kama hii itakayoweza kwa tawfiq ya Mola kutupelekea kujiandaa vizuri, ni ile hadithi iliyothibiti ya al-Habibi Musttafa (Salla Llahu 'Alayhi Wa'ala Alihi Wasallam) kuwa alisikiwa akisema Amin Amin Amin mara tatu (3) huku alipanda minbar, alipomaliza Sahaba (Radhiya Llahu ‘Anhum) walimuuliza kwa mshangao mkubwa, mbona umeitikia Amin Amin Amin, mara tatu huku ukipanda vidaraja vya minbar, jambo ambalo si kawaida yako, hukuomba dua, je kuna liilojiri?! al-Habibi Musttafa (Salla Llahu 'Alayhi Wa'ala Alihi Wasallam) aliwajibu kwa kusema:
“Amenijia Jibril –‘Alayhis Slaam- na kuniambia kuwa: yuko mbali na Rehma za Allah yule ambae ametembelewa na Ramadhaan na akashindwa kutekeleza kitachopelekea kufutiwa madhambi yake, -nilinyamaza kimya, Jibril akanitaka niitikie kwa kusema: Amin, nikasema: Amin -akaendelea kusema:yuko mbali na Rehma za Allah yule ambae atasikia jina lako linatajwa, na akawa hana nafasi ya kukusalia, -nilinyamaza kimya, Jibril akanitaka niitikie kwa kusema: Amin, nikasema: Amin-,akaendelea kusema: kuwa yuko mbali na Rehma za Allah yule ambae amejaaliwa kuwakuta wazazi wake wawili na akashindwa kuingia peponi!, -nilinyamaza kimya, Jibril akanitaka niitikie kwa kusema Amin nikasema Amin
Ndugu zangu katika imani, tujaribu kuwa na tabia ya kujiwekea mipango, malengo, njia na mbinu za kutekeleza mambo yetu, njia za kujitayarisha katika kuyatekeleza na kadhalika, tena tuwe wakweli na wawazi katika mipango yetu, kwa mfano na haya ndio hasa tunayoyapendekeza na kuyataka tuwe nayo katika kumpokea mgeni:
Azimia kuwa mgeni utampokea kwa kila aina ya ‘amali njema na utajitahidi kiasi cha kumthibitishia mgeni kuwa katika wageni wako wote wanaokutembelea nyumbani kwako na kuishi na wewe ni yeye Ramadhaan ndiye unaempenda na kumthamini, kwa sababu kubwa moja, ni mgeni aliyependekezwa na Mlinzi wa Waumini ni Mlinzi Mwema na Msaidizi Mwema, kuwa awe mgeni wako ili kwa tawfiq yake upate yale aliyoyaandaa na kuyatunuku ndani yake. Tafadhali angalia nini uliwafiqishwa mwaka jana na kile ulichoshindwa kukitekeleza ukiwekee mikakati ya kukitekeleza mwaka huu, azimia kuwa mwezi wako huu uwe ndio mwezi bora utaoishi nao na kutekeleza utachojaaliwa na kuwafiqishwa kutekeleza ukijilinganisha na miezi yote iliyopita ikiwemo Ramadhaan yako ya mwaka jana.
Weka mikakati na mipango yenye uhakika itakayo kupelekea kuweza kuitekeleza tena kwa ufanisi na bila uzito, wakati wote mgeni akiwa na wewe; kwa mfano:
Fufuwa au imarisha uhusiano wako na Mola wa Ramadhaan, kwa kumsikiliza na kumuitika, kwa kujizowesha kuwa karibu na maneno yake ambayo aliyachagulia mwezi wa Ramadhaan kuwa ndio wakati wa kuyateremsha. Jipangie wakati maalumu wa kuzungumza na As Samiy’ul Bassiyr, shauriana na ahli zako, rafiki zako, jirani, mnaofanya kazi pamoja, mnaocheza mpira pamoja, au wenzako mnaosali pamoja, shauriana nao kuchagua wakati na pahala muwafaqa pasipohitaji taklifah, ambapo mutaweza kwa tawfiq yake Mola kukaa pamoja na kuzungumza na Rahmaan, kwa mfano: kila baada ya sala fulani, nyumbani kwa fulani au msikiti fulani au klabu fulani.  Pia jiwekeeni wakati wa kuhifadhi maneno yake matukufu na kusikilizana hifdh yenu, jipangieni wakati wa kujielimisha na kuweza kufahamu maana yake, ili uweze kwa tawfiq yake Mola wa Ramadhaan kujiengezea na kujizidishia iman yenu na yaqini itakayo kupelekea/kupelekeeni kuweza kutekeleza maamrisho yake na kuwacha makatazo yake kama atakavyo Al-Wahiyd al Qahhar.
Fufuwa au imarisha uhusiano wako na sala tano, tumia diplomasia yako katika kisimamo chako cha sala tano kiijumuishe mahusiano na sala za usiku, fufuwa, imarisha sala zako kwa kuzipa uhai mpya, jaribu kurefusha visimamo, rukuu na sijdah za sala zako, fufuwa, imarisha au huisha sala za sunnah zote zikiwemo zile za kabla hujalala witr au kabla salatul fajiri au zile za usiku tahjjud.
Imarisha uhusiano wako na  jamaa zako, kwa kuwatembelea wazee wako au kuwasiliana nao, pia kwa kuwapa au kuwatengea sehemu katika kile alichokuruzuku Mola wa Ramadhaan kabla hujaiaga dunia.
Imarisha, fufuwa au anza kujifunza namna ya kuthamini wakati wako, chunga wakati wako katika shindano hili kubwa la mwaka lenye kushirikisha kila mwenye kuamini Allah na Siku ya mwisho. Imarisha, fufuwa au jizoeshe na uzoeshe ulimu wako na moyo wako na ahli zako na wenzako katika baraza zako kumkumbuka na kumtaja kwa wingi Mola wa Ramadhaan na kumsalia/kumtakia Rehmah na Amani al-Habibi Musttafa (Salla Llahu 'Alayhi Wa'ala Alihi Wasallam) aliyetufunza yote tunayoyahitaji katika uhai huu, yakiwemo tunayohitajia tuyafanye na kuyaomba wakati mgeni akiwa katika nyumba zetu, alikuwa al-Habibi Musttafa (Salla Llahu 'Alayhi Wa'ala Alihi Wasallam ) yakimhuzunisha sana yanayo tutaabisha; aliyekuwa akituhangaikia sana na kwa waliopendekezewa mgeni mtukufu.-Waumini- alikuwa al-Habibi Musttafa (Salla Llahu 'Alayhi Wa'ala Alihi Wasallam) ni mpole na mwenye huruma sana, kama ilivyothibisha hayo Qur-an tukufu, Allah anasema:
Hakika amekwisha kujieni Mtume kutokana na nyinyi wenyewe; yanamhuzunisha yanayo kutaabisheni; anakuhangaikieni sana. Kwa Waumini ni mpole na mwenye hurumaat-Tawbah aya ya 128.
Imarisha, fufuwa au anzisha uhusiano mkubwa na wenye nguvu wa kumuomba mwenye kupenda kuombwa na aliyekupendekezea namna ya kumuomba, Allah anasema:
Na Allah ana majina mazuri kabisa, basi muombeni kwa hayo “al-A’raaf aya ya 180; na wakati wa kumuomba pia, Allah anasema:
Na waja wangu watakapo kuuliza khabari zangu, waambie kuwa Mimi nipo karibu. Naitikia maombi ya mwombaji anapo niomba. Basi na waniitikie Mimi, na waniamini Mimi, ili wapate kuongoka  “ al-Baqarah aya ya 186; pia al-Habibi Musttafa (Salla Llahu 'Alayhi Wa'ala Alihi Wasallam) katika kutuhangaikia ametupendekezea wakati wa kupeleke maombi yenu kwa kusema:
Allah anashuka katika mbingu za dunia kila usiku katika thuluthi ya mwisho na kusema; "Yuko mwenye kuniomba nimkubalie maombi yake?, Nani aniulizae nimpe?, Nani aniombae msamaha (Maghfirah) nimsamehe?." Imepokelewa na Bukhar, milango ya Tahajjud (kisimamo cha usiku), mlango wa dua na sala katika sehemu ya mwisho wa usiku.
Ndugu yangu katika iman, huisha na sisitiza kumtaka na kumuomba msamaha kwani Yeye ni Ghaffar, sisitiza kumuomba rehma zake kwani Yeye ni Arhamur Raahimiyn, sisitiza na shikilia kumuomba akuepusha na akute katika moto kwani Yeye ni Qaadir wa kila kitu na ni Mwenye kufanya alitakalo na wewe ni mja wake dhalili, muhitaji na ni mwenye kukiri madhambi na taqssiyr .zako, na Yeye ni Msamehevu na Mwenye Rehma, Qur-an inasema:
Na wengine walikiri dhambi zao, wakachanganya vitendo vyema na vingine viovu. Asaa Allah akapokea toba zao. Hakika Allah ni Mwenye kusamehe Mwenye kurehemu  at-Tawbah aya ya 102.
Imarisha, fufuwa au huisha darasa yako, kama hakuna, basi pendekeza na shajiisha kuwepo kwa darasa, mihadhara, kufutarishana, kuwaidhiana, kukutana kwa ajili ya Allah,  ambapo wewe na ahli zako utakuwa muhusika wa kwanza, mhudhuriaji wake na mtangazaji wake, na mhakikishaji kuwa haitapata pingamizi ya aina yo yote ile katika kuwepo kwake, iwe pingamizi ya pahala au malipo ya pahala, au hata vifuturishaji kama vitahitajika.  Darsa/mawaidha na mikusanyiko kama hii yenye kutajwa Allah na Mtume wake al-Habibi Musttafa (Salla Llahu 'Alayhi Wa'ala Alihi Wasallam) na waja wema ni pahala patakapo kupelekea kuwa karibu na Allah, kwani ni pahala unapokumbushwa na kushajiishwa kila lenye kukupelekea kuweza kwa tawfiq yake Mola kukufikisha kwenye lengo kuu lililosababisha Ramadhaan ipendekezwe na Mola wake kuwa iwe mgeni wako katika masiku yake machache na matukufu, na hayo ni miongoni mwa vyakula unavyovitajia, vyakula vya moyo wako, mwili wako unahitaji vyakula vya namna mbili; kimoja cha kukuza mwili na chengine cha kukuza iman yako ambacho utakipata tu ukiwa karibu na wenye kupenda kunasibishwa na imaan.
Fufuwa, imarisha au anzisha uhusiano wa kuwalingania watu kwa hikmah na mawaidha mema na mazuri kabisa na ujadiliane nao kwa namna iliyo bora na  iliyozuri zaidi, kama inavyotupendekezea Qur-ani, Allah anasema:
Waite waelekee kwenye Njia ya Mola wako Mlezi kwa hikima na mawaidha mema, na ujadiliane nao kwa namna iliyo bora. Hakika Mola wako Mlezi ndiye anaye mjua zaidi aliye ipotea Njia yake, na Yeye ndiye anaye wajua zaidi walio ongoka.  “an Nahl aya ya 125, tumia diplomasia yako katika da’wah, wewe uko tayari kumkinaisha kila mtu kwa ulitakalo, kwa nini usitumie uwezo wako huo aliokupa Mola wa Ramadhaan kuwakinaisha angalau Ahli zako, jamaa zako, rafiki zako, waswahili wenzako, kufikia kutekeleza maarisho ya Mola wako na hasa yatakayowapelekea kunufaika na kufaidika na Ramadhaan ambayo unaielewa vyema umuhimu wake katika maisha yako ya hapa duniani na kesho Akhea utakapokuwa chini ya udongo.
Orodhesha a’maali njema ambazo utapenda kwa tawfiq ya Mola wa Ramadhaan uzitekeleze katika mwezi huu, kwa mfano jipangie na jiwekee kusoma kitabu fulani; katika ‘aqidah – ‘aqida ya Twahaawiyyah-, katika sala – Sala kama alivyoisali al-Habibi Musttafa (Salla Llahu 'Alayhi Wa'ala Alihi Wasallam), Sawm na kadhalika.
Ndugu zangu katika iman, haya yote yanawezekana, na wewe na mimi tutayaweza kama tutaamuwa na kuchukuwa hatua moja muhimu; kabla ya kuichukuwa hatua hiyo, ni vyema tuelewe (mimi na wewe wenye kutaka kununuwa bidhaa ya Allah), ni vyema tuelewe kuwa bidhaa tuitakayo imezungukwa na kila lisilo pendwa na kuvutiwa na nyoyo zetu, na moto ambao hufungwa milango yake katika mwezi huu, umezungukwa na kila linalo pendwa na kufurahiwa na nyoyo na nafsi zetu; hivyo basi simamisha bali vunja mawasiliano na uhusiano wako mzuri na wenye nguvu na wa karibu sana na shayttaan, mwenye nafasi kubwa na ya pekee katika kila nyumba, tuliyemnunuwa kwa fedha alizoturuzuku Mola wa Ramadhaan, TV; chakufanya au mapendekezo:Itumie kwa kuangalia yatakayo kuletea kheri kama kuangalia mihadhara, mawaidha, iwe ndani ya mwezi wa Ramadgan au miezi mengine kama huwezi kumkosa. Jaribu kumsilimisha Shayttaan wako ili ufaidike na ugeni wa Ramadhaan katika nyumba yako.
.
Ndugu yangu katika iman, tukipata ushauri kwa wenzetu ushauri ulio mzuri basi tuwe tayari kuusikiliza na kuufikiria kuutekeleza kama tutauona unamuelekeo mzuri na wenye kushikamana na mwenendo wa Al-Habibi Musttafa (Salla Llahu 'Alayhi Wa'ala Alihi Wasallam) na watu wema waliotutangulia ambao katika uhai wao walishikamana na mwenendo wa Al-Habibi Musttafa (Salla Llahu 'Alayhi Wa'ala Alihi Wasallam) bila ya kutia mawazo au fikra zao katika waliyoshikamana nayo.
Ndugu zangu katika iman, tujaribu kuishi wakati wetu huu na al-Habibi Musttafa (Salla Llahu 'Alayhi Wa'ala Alihi Wasallam) ili tuangalie vipi yeye Al-Habibi Musttafa (Salla Llahu 'Alayhi Wa'ala Alihi Wasallam) alikuwa akijitayarisha kumkaribisha na kumpokea Ramadhaan, na vipi alikuwa akiishi na Ramadhaan, yote haya kwa kuwa Yeye Al-Habibi Musttafa (Salla Llahu 'Alayhi Wa'ala Alihi Wasallam) ni Ma’asuum, ambaye kwa maneno yake hupimwa maneno, na kwa matendo yake hupimwa vitendo, na kwa hali yake husahihishwa hali. 
Ndugu zangu katika iman, ni hakika isiyopingika kuwa mwenye kumfuata, na kuigiza mwenendo wake, na kuongoka kwa sira yake al-Habibi Musttafa (Salla Llahu 'Alayhi Wa'ala Alihi Wasallam) ndie mwenye kheri nyingi na insha Allah ndiye atae faulu na kufanikiwa katika hii dunia na kesho Akhera, na ni hasara kubwa isiyopimika na kuharibikiwa kusiko elezeka kwa yule asiye mfuata al-Habibi Musttafa (Salla Llahu 'Alayhi Wa'ala Alihi Wasallam) katika kila nyaja ya maisha yake ya kila siku hapa duniani na huko twendako kwa uhakika.
Ndugu zangu katika iman, al--Habibu Musttafa (Salla Llahu 'Alayhi Wa’ala Alihi Wasallam) alikuwa akimpokea Ramadhaan kwa mapokezi yaliyojaa na kila aina ya furaha na maandalizi yenye kuonyesha na kuthibitisha kuwa mja yuko tayari kuingia kwa tawfiq ya Allah katika masiku yanye fadhila na kila lenye kupendwa na Rahmaan, mja yu tayari kuingia katika mwezi ambao kwa tawfiq yake Rahmaan ukimalizika, awe katika walioghufuriliwa na kutolewa katika moto wa Jahannam, mja yu tayari kukutana na kuishi msimu wa mavuno, mavuno atayoyahitajia bila ya shaka wala wasi wasi wa aina yo yote ile atakapokuwa chini ya udongo, mja yu tayari kukutana na msimu wa kheri, msimu wa Rahmah, msimu wa Maghfirah, msimu wa kutolewa watu katika moto wa Jahannam.
 Imethibiti katika hadithi kuwa al--Habibu Musttafa (Salla Llahu 'Alayhi Wa’ala Alihi Wasallam) akiuona mwezi muandamo wa Ramadhaan alikuwa akisema:
Allahu Akbar, Ewe Mola Uanzishe kwetu –mwezi muandamo- kwa aman na iman, na usalama na Uislam, na tawfiq ya kutekeleza kila ukipendacho na ukiridhiacho, -pia alikuwa akiuthibitishia mwezi kwa kuusemeza na kuuambia kuwa- Mola wangu na Mola wako ni Allah”.  Imepokelewa na  …………………….
Ndugu zangu katika iman, al--Habibu Musttafa (Salla Llahu 'Alayhi Wa’ala Alihi Wasalla) alipokuwa akisema maneno haya (akiomba dua hii) ilikuwa Ramadhaan ndio ishaingia kwani kuandama kwa mwezi ndio kuanza kwake, hivyo kahuwa akiukaribisha kwa hayo, kwani mwezi ushaingia, bali alikuwa akiomba awafikishwe ndani yake kwa yale aliyoyaona ni muhimu, nasi leo tunashauriana juu ya namna ya kuukaribisha Ramadhaan, ningependelea mara nyengine kama tutajaaliwa kuwa hai na uzima kuelekea kuwa na tamaa ya kukutana tena na Ramadhaan, tuweke wiki ya mwanzo ya Shaaban kuwa ndio wakati wa kushauriana namna ya kumpokea Ramadhaan, kwa kuwa matayarisho ya kumpokea mgeni mwenye nafasi kubwa katika nafsi za waumini hayawezi yakawa ya siku tatu au tano kabla ya kuwasili mgeni, hasa tukielewa kuwa bidhaa yake Mola wa Ramadhaan ambayo tunaitarajia kuinunua –kama tunacho cha kununulia- au kutunukiwa –kama tunazosababu za kuthibitisha kuwa tunastahiki kutunukiwa- au kuiomba - kama maombi yetu yanatimiza masharti ya kukubaliwa- tunaiomba tena kwa wingi katika masiku haya machache, bidhaa yake Mola wa Ramadhaan si rahisi, bidhaa yake anayoiuza ni ghali sana, bidhaa yake ni Jannah. 
Kisha tujipangie kuwa wiki ya mwisho ya Shaaban kama leo, tuiweke au tuitumie kwa kutathmini maandalizi yetu tuliyojiwekea katika kuikaribisha Ramadhaan na kujiandaa kwa kukutana naye mgeni kwa kujikumbusha na kurejea sharia na hukumu za Sawm na yote yenye kufungamana na Sawm, nini cha kufanya ndani ya mwezi mzima wa Ramadhaan na kadhalika.
Ndugu zangu katika iman, hata hivyo tutashauriana na kujitahidi kutekeleza tutakayowafiqishwa, kwani kila kitu ni kwa tawfiq yake Mola wa Ramadhaan.  Ushauri au pendekezo langu ni kuwa kwa kuwa siku zilizobakia ni chache, basi tujitayarishe na tujiandae kwa kumpokea mgeni wetu kwa mambo yafuatayo, mambo ambayo tutajaribu kuyachukuwa kutoka kwa  al--Habibu Musttafa (Salla Llahu 'Alayhi Wa’ala Alihi Wasalla) kwani kama ilivyothibitisha Qur-an kuwa yeye ndie wa kufuatwa na kuigwa kama tunataka kuongoka na kutengenewa mambo yetu, Allah anasema:
Hakika nyinyi mnayo ruwaza njema kwa Mtume wa Allah kwa anaye mtaraji Allah na Siku ya Mwisho, na akamkumbuka Allah sanaal-Ahzaab  aya ya 21
Ndugu zangu katika iman, imethibiti kuwa al--Habibu Musttafa (Salla Llahu 'Alayhi Wa’ala Alihi Wasalla) katika kujiandaa kwake kumpokea Ramadhaan, alikuwa akifunga sana katika mwezi wa Shaaban, mpaka ikafika wakati Sahaba (Radhiya Allahu ‘Anhum) wakawa hawaelewi lini al--Habibu Musttafa (Salla Llahu 'Alayhi Wa’ala Alihi Wasalla) ameamka amefunga na lini ameamka hajafunga,:
Mtume Salla Llahu 'Alayhi Wa’ala Alihi Wasallam alikuwa akifunga hadi tukadhani kuwa hatofungua kamwe, na alikuwa akiacha kufunga hadi tukadhani hatofunga tena. Sijamuona Mtume Salla Llahu 'Alayhi Wa’ala Alihi Wasallam akifunga mwezi mzima kama isipokuwa Ramadhaan, na sijamuona akifunga sana –katika siku alizokuwa akifunga- kama alivyokuwa akifunga katika mwezi wa Shabaan” Imepokelewa na Bukhar, kitabu cha Sawm, mlango wa Sawm za Shaaban
Ndugu zangu katika iman, al-Habibu Musttafa (Salla Llahu 'Alayhi Wa’ala Alihi Wasalla) alikuwa akifunga sana katika mwezi wa Shabaan kama ilivyothibiti, na sisi leo tumebakiwa na siku chache sana za mwezi, hivyo hilo hatukufanikiwa kulipata kwa baadhi yetu. 
Ndugu zangu katika iman, al--Habibu Musttafa (Salla Llahu 'Alayhi Wa’ala Alihi Wasalla) alikuwa akifanya yote haya kama ni matayarisho ya kukutana na mgeni mtukufu Ramadhaan, ili iwe wepesi kwake kutekeleza kwa tawfiq ya Rabbu wa Ramadhaan haya mambo atakapokutana na mgeni mtukufu, na haya kikweli yanatuhusu sisi (mimi na wewe), kwani yeye hana tatizo katika kutekeleza a’maali njema, haoni uzito, na vipi ataona uzito hali amejaaliwa kuwa kipoza macho yake ni katika Sala, lakini kwa kuwa ameletwa awe kigezo kwa viumbe ndio akawa anafanya ayafanyayo kwa kuwa tupate kumuiga na sio vyengivyo Allahu a’lam.
Ndugu zangu katika imani, Mgeni wetu ndio yuko milangoni mwetu (anahodisha), na baada ya siku chache ataingia ndani na kuwa nasi, suala la kujiuuliza ni vipi tutaisha naye katika kipindi hicho cha mwezi mmoja?

Hili (namna ya kuishi na Ramadhaan) ni somo lenye kujitegea, na wengi wetu kwa uhaba wa elimu zetu, na shindikizo la tamaduni zetu zisizokubalika katika Uislamu tunahitaji kuelewa jambo hili, hivyo tukipata wasaa tutawaomba maustadhi wetu - Allah awape kila la kheri - watuandalie na kutueleza namna ya kuishi na Mgenu mtukufu, kwani Mgeni huyu aliyewahi kuwa Mgeni wa al-Habibi Musttafa (Salla Llahu ‘Alayhi Wa’ala Alihi Wasallam) na Sahaba zake (Radhiya Llahu ‘Anhum), bila shaka atakuwa anakuja na mbinu na namna ya kuishi nasi, nini anapenda sisi tukipate kutoka kwake, nini hapendi sisi tufanye, nini afanyiwe ili tufaidike na ugeni wake, vipi asemezwe ili tupate fadhila zake, na kadhalika

Ndugu Waislamu, mgeni wetu anakuja kwa lengo la kututayarisha sisi kuweza kufikia lengo lililowekwa na Muumba wetu, lengo ambalo bila ya kuelewa namna ya kuishi nae itakuwa ni vigumu kulifikia.

Ndugu Waislamu, Ramadhaan inakuja kwa lengo la kutusafisha, kutufunza heshima, utii na kadhalika, tuwe wavumilivu katika kupata mafundisho yake na tuwe wastahalimivu katika kukabiliana na mitihani inayotukuta kila siku. 

Ndugu Waislamu, Ramadhaan haiwi Ramadhaan kama hatutokuwa tayari kusameheyana, kukumbushana, kuwaidhiana, kuusiana na kuamrishana mema na kukatazana maovu katika shughuli zetu zote za kila siku, kurekebishana kwa namna itayoheshimu kila mmoja utu wake.
Ndugu yangu katika iman, ningependa kwa tawfiq yake Mola wa Ramadhaan kuhitimisha kwa kujaaliya miongoni mwa ya kumkaribisha mgeni Ramadhaan ni kubainisha/kuainisha au kutaja baadhi ya habarí (hadithi dha’ifu au si sahihah) zilizo mashuhuri katika ndimi zetu ukiwemo wangu, haya ni kwa kuwa tunatakiwa kumpokea mgeni kwa kutumia hadithi sio habari, miongoni mwa hizo habari ni:
  • “Lau wangeelewa waja yaliyomo katika Ramadhaan wangelitamani umma wangu iwe Ramadhaan mwaka mzima, hakika pepo hupambwa kwa ajili ya Ramadhaan ....... “ ni hadithi ndefu.
  • “Enyi watu, umekufikieni/umekufunikeni mwezi mtukufu, mwezi ndani yake umo usiku ambao ni bora kuliko miezi alfu, amejaalia Allah funga yake ni fardh na kisimamo cha usiku wake kuwa ni tattawu’ –sunnah sio faradh-,  mwenye kujikurubisha ndani ya mwezi huu kwa (kutenda) jambo lolote la kheri, huwa ni kama aliyetekeleza fardh katika mwezi usiokuwa Ramadhaan, ...  na ni mwezi ambao mwanzo wake ni rehmah, katikati yake ni maghfirah, na mwisho wake ni kuachwa huru na Moto .....” ni hadithi ndefu pia.
  • “Fungeni mtapata afya “
  • “Mwenye kula siku moja katika Ramadhaan bila ya udhuru wo wote ule wala maradhi, haitalipika siku aliyoiwacha kwa kufunga dahri kama atafunga“
  • “Kila kitu kila mlango, na mlango wa Ibadah ni sawm
  • “Usingizi wa mwenye kufunga ni ibadah “
  • “Mambo matano humfunguza mwenye kufunga: kusema uongo; kusengenya; kuchochea/kutia fitina; kula yamini ya uongo; na kutazama kwa matamanio “
  • “Wanawake wawili walifunga wakati wa  al-Habibi Musttafa (Salla Llahu ‘Alayhi Wa’ala Alihi Wasallam), wakawa kazi yao ni kuwasengenya watu ....................................... alisema al-Habibi Musttafa(Salla Llahu ‘Alayhi Wa’ala Alihi Wasallam) hawa wawili wamefunga/wamejizuia na waliyohalalishiwa na Allah, na wamefungua na yale waliyoharamishiwa na Allah
Ndugu zangu katika iman, habari hizi (na sio hadithi) ni zenye kueleweka kwa wahusika wake, na sio hadithi, hivyo ni vyema kutozitumia kwani sio hadithi sahihi, na kutumia kama ni hadithi baada ya kuthibiti kuwa sio ni kumzulia uongo al-Habibu Mustafa (Salla Llahu ‘Alayhi Wa’ala Alihi Wasallam), na vipi utakuwa mwenye kujitayarisha kumpokea Ramadhaan! Huku unamzulia aliyekuwa  yakimuhuzunisha sana yanayo tutaabisha; aliyekuwa akituhangaikia sana na kwa mimi na wewe -na waumini wote- kama hatumzulia uongo ni mpole na mwenye huruma sana.
Ndugu zangu katika iman, kilichothibitishwa na waliotunukiwa na kuruzukiwa macho ya kuona ndani ya hadithi za al-Habibu Mustafa (Salla Llahu ‘Alayhi Wa’ala Alihi Wasallam) kuwa sio sahihi, ni vyema kwa kila anaepata nafasi ya kutuwaidhi asitumie habari kama hizi, hata kama maneno/matamshi yake yanaonekana au yanaharufu ya yote yenye muelekeo na Uislam, lakini sio hadithi za al-Habibu Mustafa (Salla Llahu ‘Alayhi Wa’ala Alihi Wasallam), na kama hadithi basi sio sahihi, na kuzitumia kama ni hadithi kwa kusema: amesema al-Habibu Mustafa (Salla Llahu ‘Alayhi Wa’ala Alihi Wasallam): hayo, baada ya kuthibiti kuwa sio sahihi, ni kumzulia uongo al-Habibu Mustafa (Salla Llahu ‘Alayhi Wa’ala Alihi Wasallam), na makemeo ya kuzua uongo tunayaelewa vyema, wachilia mbali kumzulia uongo aliyeletwa kwa lengo la kuigwa nae ni al-Habibu Mustafa (Salla Llahu ‘Alayhi Wa’ala Alihi Wasallam).

Ndugu Waislamu, tumuombe Rahman atuwafikishe katika kuikaribisha na kumpokea mgeni wetu Ramadhaan, tumuombe atuwafikishe katika kuishi na kukaa na Ramadhaan kwa kuifunga, kutekeleza ayatakayo Muumba, na kuachana na makatazo yake, pia twamuomba Muumba atupe uwezo wa kufikisha amana kama alivyoifikisha al-Habibu Mustafa (Salla Llahu ‘Alayhi Wa’ala Alihi Wasallam), atutie mapenzi baina yetu, mapenzi yatayotupelekea kuwa tayari kusameheyana, kuhurumiana, kuvumiliana, kuheshimiana na kukosoana na kurekebishana kwa njia na namna alivyokuwa akiwarekebisha al-Habibu Mustafa (Salla Llahu ‘Alayhi Wa’ala Alihi Wasallam) Sahaba zake (Radhuya Llahu ‘Anhum).

Wassalamu'alaykum Warahmatu Llahi Wabarakatuh

Imekusanywa na
Ndugu yenu katika imani
Abu Faatimah

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.