Na Mwajuma Juma
CHAMA Cha Waalimu wa Soka Zanzibar (ZAFCA), kimefanya uchaguzi mdogo na kuwachagua viongozi wa muda watakaokiongoza hadi pale utakapofanyika uchaguzi mkuu.
Katika uchaguzi huo uliofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita, wajumbe wa chama hicho walimchagua Salum Bausi kuwa Mwenyekiti mpya wa mpito.
Naye Juma Awadh alichaguliwa kuwa Makamu Mwenyekiti, wakati wakati Ali Abdallah amepewa wadhifa wa Katibu Mkuu na msaidizi wake anakuwa Nassor Salim.
Wengine waliochaguliwa kushika nyadhifa mbalimbali ni Said Omar Kwimbi aliyekabidhiwa jukumu la kuwa Mshika Fedha, akisaidiwa na Ali Msabah, na Hababuu Ali Omar amevishwa kofia ya Katibu Mwenenzi. Kwa upande wa wajumbe wa kamati Tendaji ya chama hicho, waliobahatika ni Iddi Mohammed na Seif Bausi.
Akizungumza mara baada ya kumalizika kwa uchaguzi huo, Katibu wa chama hicho Ali Abdallah, alisema lengo la uchaguzi huo ni kukiendeleza chama, kwa vile kwa muda mrefu kimeonekana kuzorota kiutendaji.
WAKATI huohuo, katika ligi ya soka jimbo la Amani, timu ya Ziwatue imerekebisha makosa yake kwa kuichapa Guzoni bao 1-0, mchezo uliofanyika uwanja wa Dynamo Kibandamaiti.
Nayo Sebleni ikalazimishwa sare isiyo na magoli uwanjani kwake dhidi ya Muungano.
No comments:
Post a Comment