RAIS Mstaafu wa awamu ya tano wa Zanzibar, Dk. Salmin Amour Juma amesema umefika wakati kwa Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA), kufundisha shahada ya Udaktari wa tiba.
Dk. Salmin alieleza hayo huko nyumbani kwake
Migombani mjini Zanzibar, alipokuwa akizungumza na uongozi wa Chuo hicho
uliofika kumkabidhi shahada yake ya Uzamifu ya Heshima iliyomtunuku.
Alisema kuanzishwa kwa mafunzo ya tiba,
kutasaidia kuwaondoshea matatizo mbali mbali wananchi wa Zanzibar, ikiwa ni
pamoja na kuwapunguzia gharama za kufuata matibabu nje ya nchi.
Dk. Salmin alisema ni vyema SUZA, katika
mipango yake ikafikiria suala la kuanzisha shahada hiyo kwa lengo la kuisaidia
jamii nzima ya Afrika ambayo inakabiliwa na uhaba mkubwa wa wataalamu wa tiba,
huku wananchi wengi katika eneo hilo wakikabiliwa na matatizo mbali mbali ya
kiafya.
Alisema wananchi wengi wamekuwa wakisumbuka
kutafuta tiba za maradhi yanayowakabili nje ya nchi jambo ambalo kutokana na
umasikini wao hawalimudu kutokana na ukubwa wa gharama zake.
"Ni vyema mkaanzisha masomo ya Udaktari
wa tiba kwani Afrika bado hatuna tiba ya kutosha watu wengi, maradhi mengi
lakini matibabu bado tatizo hivyo ni vyema tukajikita katika suala hili kwa
lengo la kuisaidia jamii yetu",
alishauri Dk.Salmin.
Aidha alisema katika kufikia azma hiyo Chuo
kitafute eneo kubwa litakaloweza kujenga Chuo cha tiba kitachokua mfano kwa
Afrika nzima ambacho kitaweza kuitangaza Zanzibar kutokana na ubora wake.
Akizungumzia historia ya kuanzishwa kwa kwa
SUZA, Dk.Salmin alisema wakati akiwa Rais alitoa wazo la kuanzishwa Chuo Kikuu
cha Taifa cha Zanzibar, baada ya kuona madhila wanayoyapata wanafunzi wa
Zanzibar katika suala la elimu ya juu.
Alisema madhila hayo yalimkumbusha historia
ya maisha yake wakati akitafuta elimu miaka ya 1961 alipokwenda Dar es Salaam
kwa jahazi na kukwama siku tatu baharini huku Dar es salaam akiwa hana jamaa
wala pesa.
"Madhila waliyokuwa wakiyapata
wanafunzi wa Zanzibar yalinikumbusha maisha yangu halisi wakati nikitafuta
elimu ambapo siku ya Jumanne tarehe 23 mwaka 1961 alipopanda jahazi kuelekea
Dar es salaam ambapo walipofika katika mkondo wa kibaazi tulikubwa na dhoruba
jambo lililotufanya tukwame siku tatu baharini”,alisema Dk. Salmin.
Alifahamisha kuwa baada ya kufika Dar es
salaam, alijitambulisha kwa wazee wa Chama cha TANU, alipoamrishwa waziri wa
Mambo ya Nje kumtafutia skuli na sehemu ya kuishi ndipo alipopelekwa skuli ya
Aga ghan na gharama zote zililipwa na serikali ya wakati huo.
Dk. Salmin alisema aliamua kuunda tume ya
watu watano kukusanya mawazo kwa lengo la kuanzisha Chuo hicho, tume ambayo
wajumbe wake walikuwa ni pamoja na Marehemu Prof.Haroub Othman, Prof.Saleh
Idrisaa na wenzao watatu ambapo waliendelea na mchakato huo hadi muda wa
uongozi wake unamalizika na ulipoingia uongozi wa Amani Karume Chuo hicho
kikaanza rasmi.
"Naupongeza sana Uongozi wa SUZA kwa
kunitunuku shahada hii ya udaktari wa heshima kwa mchango wangu pia
nakupongezeni kwa kuanzisha shahada ya udaktari wa lugha ya Kiswahili hilo ni
jambo la kujivunia kwa Zanzibar", alisema Dk.Salmin.
Nae Makamu Mkuu wa Chuo hicho,Prof.Idris
Ahmada Rai alisema miaka 10 ya Chuo wamejipanga kupanua wigo kwa kuwa na skuli
nne kutoka moja ya awali wakati chuo kinaanzishwa, akizitaja skuli hizo kuwa ni
skuli ya Kiswahili na lugha za Kigeni, skuli ya elimu, skuli ya sayansi ya
maumbile na jamii pamoja na skuli ya elimu ya kitaalamu na endelevu.
Prof. Rai alisema kuanzia mwaka mpya wa
masomo unaoanza mwezi wa Oktoba mwaka huu Chuo kitaanzisha masomo ya Udaktari
wa lugha ya Kiswahili ambapo hatua huyo imefikiwa baada ya Maprofesa wengi wa
Kizanzibari kuamua kurudi nyumbani kuja kufundisha Wazanzibari wenzao.
Akitoa shukrani mjumbe wa Baraza la Chuo
hicho, Mohammed Said Dimwa alisema SUZA inathamini mchango wa Dk.Salmin na
haitosita kuendelea kumtumia kwa ushauri maelekezo pale itapoona inafaa kwa
maendeleo ya chuo.
Chuo cha Taifa cha Zanzibar (SUZA)
kimeanzishwa mwaka 2002 kwa sheria namba nane ya mwaka 1999 ya Baraza la
Wawakilishi kilianza na wanafunzi 55 ambapo hivi sasa kina wanafunzi wapatao
2000.
No comments:
Post a Comment