Habari za Punde

Dk. Shein:SMZ imedhamiria kidhati kuimarisha utalii. Ataka jamii ishiriki ifaidike nao


Said Ameir, Ikulu

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amesisitiza dhamira ya dhati ya serikali kuendeleza na kuimarisha sekta ya utalii kwa kushirikiana na washirika wa sekta hiyo ikiwemo sekta binafsi.
Dk. Shein alitoa kauli hiyo jana Ikulu wakati wa mazungumzo na Bodi ya Wakurugenzi wa Jumuiya ya Wawekezaji katika sekta ya utalii Zanzibar (ZATI) na Jumuiya ya Makampuni ya Watembeza Watalii Zanzibar (ZATO).
“Dira yetu ya maendeleo ya mwaka 2020 inatuelekeza kuwa utalii ndio sekta mama na halikadhalika mpango wetu wa kupunguza umasikini Zanzibar (MKUZA II) umetilia mkazo sio tu nafasi ya sekta ya utalii katika kupambana na umasikini bali pia maendeleo yetu kwa ujumla,” alisema Dk. Shein.

Dk. Shein alizipongeza bodi na viongozi wa ZATI na ZATO kwa ushirikiano wao na serikali na taasisi zake kama vile Mamlaka ya Ukuzaji Vitega Uchumi Zanzibar (ZIPA), Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA)  na Bodi ya Mapato Zanzibar (ZRB) ushirikiano ambao aliueleza kuwa umesaidia kukuza sekta hiyo Zanzibar. 
 Alibainisha kuwa madhumuni ya kuleta dhana ya utalii kwa wote ni kuhakikisha kuwa kila mmoja anashiriki kwa nafasi yake na mahala alipo kwa namna moja au nyingine katika kukuza na kuimarisha utalii Zanzibar.



“Tunataka kila mtu ashiriki kukuza na kuimarisha utalii kwa sababu ndio sekta yetu kuu ya uchumi na inatufaidisha sote kwa namna moja au nyingine,” alifafanua Dk. Shein.



Katika mazungumzo hayo ambayo yalihudhuriwa pia na Mshauri wa Rais masuala ya Utalii,Issa Ahmed, ujumbe wa ZATO na ZATI walibadilishana mawazo na Rais kuhusu masuala ya huduma katika sekta ya utalii, usalama wa watalii, kuitangaza Zanzibar nje kuvutia uwekezaji na kuongeza idadi ya watalii pamoja na haja ya kuimarisha mafunzo kwa wananchi wa Zanzibar ili kuongeza ajira kwa Wazanzibari katika sekta hiyo.  



Kwa hiyo alitoa wito kwa wadau wote katika sekta ya utalii na zile ambazo zinahusiana na sekta hiyo pamoja na wananchi kushirikiana kwa hali na mali kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazoikabili sekta hiyo muhimu kwa maendeleo ya Zanzibar.



Aliwahakikishia washirika wa sekta ya utalii kuwa milango ya serikali yake iko wazi kwa majadiliano ya mara kwa mara kuhusu namna bora ya kuimarisha sekta ya utalii nchini.



Katika mazungumzo hayo ujumbe wa ZATI uliongozwa na Mwenyekiti wake, Abdulswamad Said Ahmed na ule wa ZATO uliongozwa na Mwenyekiti wake, Khalifa Mohamed Makame.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.