Habari za Punde

UNDP laipatia Baraza la Wawakilishi magari matatu

Na Himid Choko,BLW            

SHIRIKA la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) limekabidhi msaada wa gari tatu kwa ajili ya matumizi ya Kamati za Kudumu za Baraza la Wawakilishi.
Gari hizo zilizogharimu kiasi ya shilingi milioni 152 ni miongoni mwa misaada ya shirika hilo chini ya mradi wa kusaidia mabunge.
Akikabidhi msaada huo kwa Spika wa Baraza la Wawakilishi, Pandu Ameir Kificho, Mkuu wa Ofisi ya UNDP Zanzibar, Anna Segan alisema  shirika lake limetoa msaada huo ili kuzijengea uwezo zaidi kamati hizo.
Alisema kamati za kudumu za mabunge ni vyombo vinavyopaswa kujitegemea ili kutekeleza kazi zake kwa ufanisi zaidi.

Alisema  kazi  ya  kusimamia  na kuchunguza serikali na taasisi zake ni muhimu na ngumu hivyo  Kamati za Kudumu za Mabunge  pamoja na mabunge yenyewe yanapaswa kuwa na vitendea kazi vya kutosha  ili ziweze kuheshimika kwa  wanaowachunguza na kuwasimamia.
Aidha alisema kwamba serikali nyingi ulimwenguni zimefanikiwa kiutendaji na uwajibikaji kutokana na usimamizi mzuri na madhubuti unaotokana na kamati za mabunge.

Akipokea msaada huo Spika wa Baraza la Wawakilishi, Pandu Ameir Kificho alisema  Baraza la Wawakilishi na serikali inaridhishwa na juhudi za UNDP  kwa misaada yake mbali mbali nchini.
Alisema shirika hilo limekuwa mstari wa mbele katika kusaidia maendeleo ya wananchi na kuendelea kutoa wito kwa mashirika mengine kuiga mfano huo.
Alisema  kupatikana kwa gari hizo kutasaidia  kurahisisha  usafiri kwa kamati za kudumu na hivyo kuwawezesha kuwa huru zaidi katika kutekeleza majukumu yao ambapo awali mara nyingi walikuwa wakitegemea usafiri  kutoka taasisi wanazozifanyia kazi.
Nae Katibu wa Baraza la Wawakilishi, Yahya Khamis Hamad ameahidi kwamba ofisi yake itazitunza gari hizo na zitatumika kama ilivyokusudiwa.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.