Habari za Punde

Waziri ataka vishoka wa maji wadhibitiwe

Na Abdi Shamnah

WAZIRI wa Makaazi, Maji, Nishati na Adhi, Ramadhan Abdulla Shaaban, ameitaka Bodi ya Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA), kusimamia ipasavyo sheria ya uungaji maji, ili kudhibiti wimbi la uungaji wa maji kiholela, unaosababisha upungufu mkubwa wa huduma hiyo.
Waziri huyo alitoa changamoto hiyo jana  katika ukumbi wa Mamlaka ya Maji Gulioni, katika uzinduzi wa bodi ya tatu ya Wakurugenzi ya Mamlaka hiyo.
Alisema Mamlaka hiyo inakabiliwa na jukumu kubwa la kutatua tatizo sugu la uungaji maji kiholela, unaofanywa na baadhi ya mafundi wa mamlaka kwa kushirikiana na wananchi, kinyume na taratibu na miongozo ya utumishi.


Alisema hatua hiyo isiozingatia sheria wala  utaalamu inapelekea uharibifu wa mfumo wa miundombinu na kuwa chimbuko la upungufu wa maji, hususan katika maeneo ya mjini.
“Mafundi wa ZAWA kamwe wasihusike na uungaji wa maji katika miradi ilio nje ya mamlaka hii,” alionya.
Aidha alisema pia kuna tatizo kubwa la uchimbaji holela wa visima, ambao huwanufaisha wananchi wachache wenye uwezo na kupelekea wananchi wengi kukosa huduma hiyo muhimu.
Waziri huyo aliwataka wajumbe wa Bodi hiyo kusimamia utoaji wa elimu kwa wananchi ili waweze kufahamu matumizi bora ya maji, pamoja na uhifadhi wa mazingira na vianzio vyake.
Katika hatua nyingine Waziri Shaaban, aliwataka wajumbe wa Bodi hiyo pamoja na wataalamu wa ZAWA kufanya kazi kwa mashirkiano ilii kuleta ufanisi na upatikanaji wa uhakika wa huduma hiyo.
Nae, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Mustafa Aboud Jumbe alisema hivi sasa dunia inakabiliwa na changamoto kubwa ya mabadiliko ya hali ya hewa, hatua inayopelekea upungufu mkubwa wa maji, hivyo kuitaka Mamlaka ya Maji kuwaelimisha wananchi juu ya umuhimu wa kutunza vianzio vya maji.
Mapema Mwenyekiti  wa Bodi hiyo, Mtumwa Khatibu Ameir, alisema suala la upatikanaji wa maji safi na salama  ni tete kwa kuzingatia kuwa linakabiliwa na changamoto nyingi, ikiwemo uchakavu wa miundo mbinu.
Aliitaka mamlaka hiyo kuwashajiisha wananchi kuchangia huduma hiyo kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizopo.  

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.