Habari za Punde

LAAC yabaini madudu halmashauri Arusha

Na Joseph Ngilisho, ARUSHA
KAMATI ya Bunge ya hesabu za serikali ya mtaa (LAAC), imebaini upotevu mkubwa wa fedha za maendeleo katika halmashauri ya jiji la Arusha, huku ikiituhumu kamati ya fedha kushindwa kusimamia fedha zinazotengwa kwa ajili ya miradi ya wananchi.
Aidha kamati hiyo imemshutumu Meya wa jiji la Arusha, Gaudence Lyimo, ambaye ni Mwenyekiti wa kamati ya fedha kwa kuhusika na wizi wa mamilioni ya fedha.
Mwenyekiti wa kamati hiyo, Rajab Mohamed, alisema kamati imebaini wizi wa kutisha kupitia fedha za miradi ya maendeleo ya jamii, ambapo sekta hiyo hutengewa asilimia 10 ya bajeti ya kila mwaka ya halmashauri hiyo.
Alisema bajeti ya mwaka 2011/12 jumla ya shilingi milioni 391 zilitengwa huku fedha zilizotumika zikionyesha ni shilingi milioni 30 pekee na fedha nyengine hazijulikani zilipo.
Pia alisema taarifa ya fedha ya mwaka 2012/13 sekta hiyo ilitengewa shilingi milioni 518 lakini fedha zilizotumika ni shilingi milioni 75, tu huku fedha nyengine zikiishia matumboni mwa wajanja.
Baadhi ya wajumbe wa kamati hiyo walionesha kusikitishwa na ubadhirifu wa fedha hizo na kumtaka mwanasheria wa jiji hilo, Kiomoni Kibamba awafungulie mashtaka wahusika.

Mmoja wa wajumbe wa kamati hiyo, Ezekiel Maige, alisema baadhi ya watendaji wamekuwa na tabia ya kukopeshana fedha za miradi, ambapo kwenye taarifa zao hubainisha kwamba fedha zimekopwa na wananchi na makundi ya vijana na wanawake.
Naye Mbunge wa Karatu, Israel Natse, alitaka halmashauri hiyo ifutwe kwani inaongoza kwa hati na matumizi mabaya ya fedha.
Aidha alimtaka Meya wa jiji la Arusha, aeleze kwanini amekuwa akipitisha fedha za miradi wakati akijua haziendi kwa wananchi.
Kamati hiyo pia ilifichua upotevu wa shilingi milioni 225 fedha ambazo zilitengwa kwa ajili ya maendeleo ya vijiji lakini zilipitishwa na hazikuwafikia walengwa ambao ni wenyeviti wa vijiji kwa ajili ya maendeleo ya vijiji vyao.
Pia kamati imebaini halmashauri hiyo imekuwa ikiidhinisha malipo hewa kwa wakala pindi anapofikia ukomo wa mkataba.
Akijibu shutuma hizo, Meya Lyimo, alisema hafahamu chochote juu ya upotevu wa fedha hizo na kuahidi kufuatilia.

Hata hivyo, alisema kuhusu shutuma za jiji kutofikia malengo ya makusanyo ya ndani inatokana na sababu za kisiasa inayolikumba jiji la Arusha.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.