Habari za Punde

Dk Shein akutana na Waziri wa Nchi,Maendeleo,Biashara na Ushirikiano wa Ireland

 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiri wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akisalimiana na Waziri wa Nchi Maendeleo,Biashara na Ushirikiano wa Ireland Bw.Sean Sherlock wakati alipofika Ikulu Mjini Zanzibar akiwa na Ujumbe aliofuatana nao.[Picha na Ikulu.]
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiri wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akizungumza na Waziri wa Nchi Maendeleo,Biashara na Ushirikiano wa Ireland Bw.Sean Sherlock wakati alipofika Ikulu Mjini Zanzibar akiwa na Ujumbe aliofuatana nao.[Picha na Ikulu.]


  
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                                                         19.3.2015
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amefanya mazungumzo na Waziri wa Nchi, Maendeleo, Biashara na Ushirikiano wa Ireland Mhe. Sean Sherlock na kumueleza mikakati iliyowekwa na Serikali anayoiongoza katika kuimarisha sekta za maendeleo sambamba na kusimamia na kuendeleza amani na utulivu uliopo.

Dk. Shein aliyasema hayo leo huko Ikulu mjini Zanzibar wakati alipofanya mazungumzo na Waziri wa Nchi, Maendeleo, Biashara na Ushirikiano wa Ireland Mhe. Sean Sherlock akiwa amefuatana na Balozi wa Ireland nchini Tanzania Mhe. Fionnuala Gilsenan.

Katika maelezo yake Dk. Shein alimueleza Balozi huyo pamoja na ujumbe aliofuatana nao hatua mbali mbali zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuhakikisha sekta za maendeleo zinaimarika hapa nchini.

Dk. Shein alieleza kuwa miongoni mwa hatua zinazochukuliwa na Serikali ni kuhakikisha inaimarisha Vyuo vyake vya Amali kwa lengo la kutoa mafunzo ya kuwatayarisha vijana wanaomaliza masomo katika vyuo hivyo kujiajiri wenyewe.


Alisema kuwa tayari Serikali imeshajenga vyuo vya Amali kwa upande wa Unguja na Pemba na juhudi zinaendelea kuviimarisha sambamba na azma ya kuviongeza vyengine ili viweze kukidhi haja ya kutoa mafunzo kwa vijana huku serikali ikijitahidi katika kutatua changamoto ya upatikanaji wa vifaa kwa ajili ya masomo vyuoni humo.

Akieleza kuhusu sekta ya afya, Dk. Shein alieleza juhudi za makusudi zinazochukuliwa na Serikali katika kuhakikisha sekta hiyo inaimarika ikiwa ni pamoja na kupunguza vifo vya akina mama na watoto hatua ambayo inaonesha mafanikio kila kukicha.

Aidha, Dk. Shein alieleza juhudi za Serikali katika kuhakikisha uchumi wake unazidi kuimarika pamoja na kupiga hatua katika kutekeleza malengo yake ya Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umasikini (MKUZA).

Kwa upande wa Serikali anayoiongoza chini ya muundo wa Umoja wa Kitaifa, Dk. Shein alisema kuwa Serikali hiyo, inaendelea vizuri na mafanikio makubwa yameweza kupatikana tokea kuanzishwa kwake hadi hii leo.
Alisisitiza kwamba kubwa kuliko yote ni kuhakikisha amani na utulivu inaendelea kuwepo hapa nchini kwa wakati wote huku akisisitiza hatua hiyo kuendelezwa na kusimamiwa na Serikali anayoiongoza hasa katika wakati huu wa kuelekea upigaji kura za maoni juu ya Katiba inayoopendekezwa sambamba na uchaguzi mkuu ujao.

Katika hatua za kuendeleza amani na utulivu hapa nchini, Pia, Dk. Shein alimueleza Balozi Sherlock juhudi zinazochukuliwa na Serikali katika kuhakikisha suala zima la ulinzi na usalama kwa ajili ya watalii linaimarishwa ili kuufanya utalii wa Zanzibar uzidi kupata sifa na kuwa kivutio kwa  watalii kutoka kila pembe ya dunia.

Aidha, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi zake kwa Ireland kwa kuendeleza ushirikiano na uhusiano kati yake na Zanzibar na kusisitiza haja ya kuimarishwa zaidi ushirikiano huo ili kuleta manufaa kwa pande zote mbili.

Dk. Shein alieleza haja ya kuendeleza ushirikiano katika sekta mbali mbali za maendeleo ikiwemo sekta ya kilimo na sekta nyenginezo huku akitoa pongezi zake kwa nchi hiyo kwa kuiunga mkono Zanzibar katika kusaidia katika sekta ya afya, miundombinu na mawasiliano, huduma za zimamoto, ufugaji na sekta nyenginezo.

Nae Waziri wa Nchi, Maendeleo, Biashara na Ushirikiano wa Ireland Mhe. Sean Sherlock alimueleza Dk. Shein kuwa Ireland inathamini sana uhusiano na ushirikiano wake na Zanzibar hasa kwa kutambua kuwa Ireland na Zanzibar zote ni  visiwa.

Waziri Sherlock alisema kuwa Ireland itaendelea kutoa ushirikiano wake na kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika uimarishaji wa miradi mbali mbali ya maendeleo huku akiahidi Serikali yake kuunga mkono uimarishaji wa Vyuo vya Amali hapa Zanzibar.

Alisema kuwa tokea mwaka 1979 Ireland imekuwa na mahusiano mema na Tanzania ikiwemo Zanzibar hatua ambayo inaendelezwa hadi hivi leo.

Aidha, Waziri Sherlock alieleza kuwa mafanikio yaliofikiwa hapa nchini katika kuimarisha sekta za maendeleo ni ya kupigiwa mfano na kuna kila sababu ya kuendelea kuyaunga mkono. Waziri huyo alieleza  azma ya Serikali yake ya kuendeleza uhusiano na ushirikiano na Zanzibar hasa katika maeneo mapya ya kimaendeleo.

Mnamo mwezi Disemba mwaka jana Wabunge wa Bunge la Ireland walitembelea Zanzibar na kufanya mazungumzo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapindyuzi Dk. Ali Mohamed Shein ambapo katika mazungumzo hayo suala la kuimarisha uhusiano na ushirikiano baina ya opande mbili hizo lilisisitizwa.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.