STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar
10.9.2015

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa India na Zanzibar zina uhusiano na ushirikiano wa
kihistoria hivyo hatua za nchi hiyo za kuendelea kuiunga mkono Zanzibar zimeweza
kuleta manufaa kwa pande zote mbili.
Dk. Shein aliyasema
hayo leo wakati wa mazungumzo kati yake na Balozi mpya wa India katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.
Sandeep Arya, aliefika Ikulu mjini Zanzibar kwa ajili ya kujitambulisha.
Katika mazungumzo
hayo, Dk.Shein alisema kuwa Tanzania ikiwemo Zanzibar zina uhusiano na ushirikiano
wa kihistoria na India ambao umeanzishwa na
waasisi wa nchi hizo akiwemo marehemu Julius Kambarage Nyerere na marehemu
Mzee Abeid Amani Karume kwa mashirikiano
na waasisi wa nchi hiyo akiwemo marehemu Indira Gandhi.
Akielezea juu ya
ushirikiano na uhusiano kati ya India na Zanzibar, Dk. Shein alimueleza Balozi Arya
kuwa Zanzibar inathamini sana ushirikiano uliopo hatua ambao umesaidia kwa
kiasi kikubwa kuongeza ushirikiano katika sekta mbali mbali za maendeleo
ikiwemo elimu, afya, biashara, miundombinu, huduma za kijamii na nyenginezo.
Kwa upande
wa ushirikiano uliopo katika sekta ya
elimu, Dk. Shein aliipongeza India kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika sekta
ya elimu ikiwa ni pamoja na kutoa nafasi kadhaa za masomo kwa Zanzibar ikiwa ni
pamoja na kuwapatia nafasi hizo watendaji wa Serikali kwa lengo la kuongeza
ufanisi na kusisitiza haja ya kuongezwa kwa nafasi hizo.
Pia, alipongeza
hatua za mashirikiano zilizofanyika kati ya Zanzibar na India katika
uanzishwaji wa Chuo cha amali cha “Barefoot college” katika kijiji cha
Kinyasini Mkoa wa Kaskazini Unguja ambacho alikizindua hivi karibuni ikiwa ni
matunda ya ziara yake aliyoifanya nchini India Februari mwaka 2014.
Dk. Shein alitumia
fursa hiyo kumueleza Balozi Arya, mafanikio yaliofikiwa hapa Zanzibar katika
sekta za maendeleo ikiwemo sekta ya utalii hatua ambayo imepelekea kufungua
afisi nchini humo katika mji wa Mumbai. Pia, alimueleza kuimarika kwa mahusiano kati ya wananchi wa India na
Zanzibar yaliopelekea kukuza ushirikiano wa kijamii na kiutamaduni.
Sambamba na hayo,
Dk. Shein aliendelea kuipongeza India kwa kuendeleza ushirikiano wake na kuunga
mkono miradi ya maji, elimu na mengineyo huku akipongeza hatua zinazoendelea za
kutekeleza makubaliano yaliofika katika ziara yake nchini India.
Nae Balozi mpya wa
India katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Sandeep Arya alipongeza uhusiano na ushirikiano wa muda
mrefu uliopo kati ya India na Zanzibar na kuadi kuuendeleza.
Balozi Arya alisema
kuwa India itahakikisha inakamilisha miradi yote ya maendeleo ilioanzishwa kwa
mashirikiano kati yake na Zanzibar sambamba na kuongeza nafasi za masomo kwa Zanzibar
huku akiahidi juhudi maalum zitaendelea kuchukuliwa katika kuutangaza utalii wa
Zanzibar nchini India.
Aidha, Balozi Arya,
alisema kuwa juhudi za makusudi zitachukuliwa katika kuhakikisha sekta ya
uwekezaji na biashara zinaimarika kati ya nchi mbili hizo sambamba na kuongeza
nafasi za masomo nchini humo.
Wakati huo huo, Dk. Shein alifanya mazungumzo na Mhe. Hemed Idd
Mgaza, Balozi Mteule wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Saud Arabia
aliyefika Ikulu mjini Zanzibar kwa ajili ya kusalimia na kuaga rasmi.
Katika mazungumzo
hayo, Dk. Shein alimueleza Balozi Mgaza kuwa Tanzania imekuwa na uhusiano mwema
na Saud Arabia ambapo nchi hiyo imeweza kutoa misaada kadhaa ya kuendeleza
sekta za maendeleo na ni nchi yenye mahusiano makubwa na nchi nyengine duniani
hivyo ipo haja ya kukuza uhusiano na ushirikiano uliopo.
Kwa upande wa Zanzibar,
Dk. Shein alisema Saud Arabia imeweza kusaidia sekta ya elimu na kutolea mfano
Chuo Kikuu cha mwanzo cha Zanzibar kiliopo Tunguu ambacho kimejengwa na Darul
Imaan kutoka Saudia, miundombinu zikiwemo barabara za Kaskazini Pemba ambazo
amezizindua hivi karibuni zenye km 35 ikiwemo Wete-Konde na Wete-Gando, sekta
ya maji, umeme na nyenginezo.
Pamoja na hayo,
Dk. Shein alimueleza Balozi huyo kuwa hivi sasa Tanzania imekuwa ikichukua
juhudi za makususdi katika kuimarisha uhusiano na ushirikiano wa uchumi wa
kidiplomasia na nchi rafiki duniani hivyo, ipo haja kwa Tanzania kukuza
uhusiano wake na Saudia katika nyanja hiyo.
Nae Balozi
Magaza, alimueleza Dk. Shein shukurani zake kwa viongozi wa kitaifa kwa uteuzi
wake huo huku akiahidi kutekeleza kazi zake kwa ufanisi na mashirikiano makubwa
kwa lengo la kuimarisha uhusiano na ushirikiano uliopo kati ya Tanzania na Saud
Arabia.
Rajab Mkasaba, Ikulu
Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024
2231822
E-mail:
rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment