STATE HOUSE
ZANZIBAR
OFFICE OF THE
PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 20.4.2016
SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar itahakikisha inawapelekea huduma zote
muhimu wananchi waliaothirika na mvua za masika na hakuna hata mwananchi mmoja miongoni
mwao atakae kaa na njaa kwa kukosa chakula.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza
la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein aliyasema hayo leo mara baada ya
kuwatembelea wananchi walioathirika na mvua za masika zinazoendelea hapa nchini
ambao wanaoishi kwa muda katika kambi ya skuli ya Mwanakwerekwe C.
Dk. Shein alisema kuwa hatua hizo za
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar za kuwahudumia wananchi wake ni wajibu wa
Kikatiba kwa kutakiwa waishi vizuri sambamba na kupata huduma zote za msingi
kwa kuenziwa wao pamoja na mali zao.
Katika mazungumzo yake na wananchi hao
Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwawapa pole kwa matukio yaliowatokezea na
kueleza kuwa hizo zote ni rehema za MwenyeziMungu na wanatakiwa kuzipokea kwa
nguvu zote huku akiahidi kuwa Serikali yao itaendelea kuwasaidia.
“Kufanya hivyo ni wajibu wa Serikali
kwani kama tungekuwa na uwezo wa kila mtu kumpa nyumba yake tungempa lakini
uwezo hatuna lakini hata hivyo tutahakikisha Serikali inafanya kila
iwezekanavyo kukufanyieni yale yote yanayowezekana”,alisema Dk. Shein.
Aidha, Dk. Shein alisema kuwa kuanzia leo
Serikali itahakikisha kwa yale yote yaliyokuwa hayapo wanapelekewa ikiwa ni
pamoja na kuwapekea TV ili waweze kupata taarifa za nchi yeo huku
akiwahakikishia wananchi hao kuwa watoto wote wanaosoma skuli ambao wapo katika
kambi hiyo kuanzia leo watapelekwa skuli.
Dk. Shein alisema kuwa matukio hayo yote
ya mafuriko yaliosababishwa na mvua za masika ni matokeo ya mabadiliko ya mji
wa Zanzibar hivi sasa ambao katika baadhi ya maeneo hayakujengwa kwa kufuata
taratibu za ujenzi na ndipo zinazonyesha mvua kubwa husababisha maafa makubwa.
Alisema kuwa ujenzi uliojengwa wa
kutofuata mipango miji ndio uliopelekea kuifanya Zanzibar hata kutokuwepo kwa
utaratibu wa maji ya mvua kufuata mitaro ambayo kwa hivi sasa miundombinu ya
kutoa maji ya mvua nayo haipo hali ambayo huchangia kutokea kwa mafuriko.
Dk. Shein alieleza kuwa athari hizo pia, husababishwa
na baadhi ya watu wenye uwezo wa kifedha ambao wamezizungushia nyumba zao
makuta ambayo huzuia maji na kusababisha maji kutuama na hatimae kuleta athari.
Sambamba na hayo, Dk. Shein alisema kuwa
makaazi hayo katika kambi hiyo ni kwa muda tu kutokana na maafa yaliowatokezea
wananchi hao lakini hata hivyo Serikali itahakikisha mara baada ya maeneo yao
kuanza kukalika yanakuwa katika hali nzuri na ndipo waweze kuanza tena maisha.
Kwa upande mwengine Dk. Shein alieleza
kuwa mbali ya maafa yaliotokea baada ya kunyesha mvua za masika yakiwemo
mafuriko pia, mvua hizo zimepelekea kuongezeka kwa maradhi ya kipindipindu na
kuwataka wananchi kufuata maelekezo wanayopewa na taasisi husika katika
kujikinga na maradhi hayo.
Pamoja na hayo, Dk. Shein alisema kuwa
maeneo yote ya Unguja na Pemba hivi sasa yana vimelea vya kipindupindu hivyo aliwataka
wananchi kutofanya mzaha katika kupambana na maradhi hayo.
“Wananchi msifanye mas-hara, tukumbuke
mwaka 1978 yalipoibuka kwa kasi maradhi haya...hakuna hata Wilaya moja isiyokuwa
na kipindupindu hivi sasa...wananchi mfuate taratibu msiwe wakaidi mkiambiwa msiuze
biashara zilizokatatwa msiuze, unadhifu upewe kipaumbele”,alisisitiza Dk.
Shein.
Dk. Shein alitumia fursa hiyo, kuupongeza
uongozi wa Mkoa wa Mjini Magharibi pamoja na Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais
kupitia Idara yake ya Maafa kwa juhudi wanazozichukua katika kuwapa huduma za
lazima wananchi hao ambao nao uongozi huo kwa upande wake ulimuhakikishia Rais
kuwa wamejipanga vizuri kutoa huduma stahiki kwa wahanga hao wote.
Wananchi wapatao 420 wapo kwenye kambi
hiyo wakiwemo wanawake 240 na wanaume 180 ambapo watoto wadogo walio chini ya
umri wa miaka mitano wapo 54 na wazee wa miaka 60 hadi 70 wapo 62, hao wote
wanatoka katika Shehia za Kwahani, Welezo na Nyerere katika Wilaya ya Mjini
Unguja.
Wakati huo huo, Dk. Shein alitembelea kambi ya kipindupindu iliyopo
Chumbuni mjini Unguja na kuwapa pole wagonjwa waliolazwa kambini hapo na baadae
kupata maelezo kutoka kwa uongozi wa Wizara ya Afya ambapo kwa upande wake Dk. Shein aliendelea
kusisitiza suala zima la usafi wa maji yanayotumiwa na wananchi sambamba na kuzingatia
usafi wa mazingira.
Dk. Ramadhan Mikidadi ambae ni mkuu wa
kambi hiyo, alimueleza Dk. Shein kuwa tayari wagonjwa wengi wamefikishwa katika
hospitali za Unguja na Pemba tokea kuanza kipindupindu mnamo mwezi Septemba
mwaka jana ambapo hivi sasa kuna wagonjwa 1788 wakiwemo 684 ambao hali zao si
nzuri na tayari wagonjwa 40 wameshafariki.
Nae
Dk. Mohammed Dahoma kwa upande wake alieleza juhudi zinazochukuliwa katika
kuwapa elimu wananchi kupitia njia mbali mbali zikiwemo vyombo vya habari,
magari ya sinema pamoja na kua na azma ya kutoa elimu kwenye
simu za mkononi kupitia mtandao wa ZANTEL pamoja na makundi ya WASAP.
Dk.
Dahoma alieleza kuwa kuwepo kwa vyanzo mbali mbali vya maji kunachangia
kuongezeka kwa maradhi hayo pamoja na baadhi ya wananchi kutotumia dawa za
kutia kwenye maji “water guard” kwa kisingizo kuwa zina harufu mbaya sambamba
na kupunguza makali na kuwasihi wananchi kuachana na dhana hizo.
Rajab Mkasaba,
Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024
2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment