Habari za Punde

Serikali itahakikisha inawapatia huduma zote muhimu waathirika wa mvua za masika


 
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                     20.4.2016
---
SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar itahakikisha inawapelekea huduma zote muhimu wananchi waliaothirika na mvua za masika na hakuna hata mwananchi mmoja miongoni mwao atakae kaa na njaa kwa kukosa chakula.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein aliyasema hayo leo mara baada ya kuwatembelea wananchi walioathirika na mvua za masika zinazoendelea hapa nchini ambao wanaoishi kwa muda katika kambi ya skuli ya Mwanakwerekwe C.

Dk. Shein alisema kuwa hatua hizo za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar za kuwahudumia wananchi wake ni wajibu wa Kikatiba kwa kutakiwa waishi vizuri sambamba na kupata huduma zote za msingi kwa kuenziwa wao pamoja na mali zao.

Katika mazungumzo yake na wananchi hao Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwawapa pole kwa matukio yaliowatokezea na kueleza kuwa hizo zote ni rehema za MwenyeziMungu na wanatakiwa kuzipokea kwa nguvu zote huku akiahidi kuwa Serikali yao itaendelea kuwasaidia.


“Kufanya hivyo ni wajibu wa Serikali kwani kama tungekuwa na uwezo wa kila mtu kumpa nyumba yake tungempa lakini uwezo hatuna lakini hata hivyo tutahakikisha Serikali inafanya kila iwezekanavyo kukufanyieni yale yote yanayowezekana”,alisema Dk. Shein.

Aidha, Dk. Shein alisema kuwa kuanzia leo Serikali itahakikisha kwa yale yote yaliyokuwa hayapo wanapelekewa ikiwa ni pamoja na kuwapekea TV ili waweze kupata taarifa za nchi yeo huku akiwahakikishia wananchi hao kuwa watoto wote wanaosoma skuli ambao wapo katika kambi hiyo kuanzia leo watapelekwa skuli.

Dk. Shein alisema kuwa matukio hayo yote ya mafuriko yaliosababishwa na mvua za masika ni matokeo ya mabadiliko ya mji wa Zanzibar hivi sasa ambao katika baadhi ya maeneo hayakujengwa kwa kufuata taratibu za ujenzi na ndipo zinazonyesha mvua kubwa husababisha maafa makubwa.

Alisema kuwa ujenzi uliojengwa wa kutofuata mipango miji ndio uliopelekea kuifanya Zanzibar hata kutokuwepo kwa utaratibu wa maji ya mvua kufuata mitaro ambayo kwa hivi sasa miundombinu ya kutoa maji ya mvua nayo haipo hali ambayo huchangia kutokea kwa mafuriko.

Dk. Shein alieleza kuwa athari hizo pia, husababishwa na baadhi ya watu wenye uwezo wa kifedha ambao wamezizungushia nyumba zao makuta ambayo huzuia maji na kusababisha maji kutuama na hatimae kuleta athari.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alisema kuwa makaazi hayo katika kambi hiyo ni kwa muda tu kutokana na maafa yaliowatokezea wananchi hao lakini hata hivyo Serikali itahakikisha mara baada ya maeneo yao kuanza kukalika yanakuwa katika hali nzuri na ndipo waweze kuanza tena maisha.

Kwa upande mwengine Dk. Shein alieleza kuwa mbali ya maafa yaliotokea baada ya kunyesha mvua za masika yakiwemo mafuriko pia, mvua hizo zimepelekea kuongezeka kwa maradhi ya kipindipindu na kuwataka wananchi kufuata maelekezo wanayopewa na taasisi husika katika kujikinga na maradhi hayo.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alisema kuwa maeneo yote ya Unguja na Pemba hivi sasa yana vimelea vya kipindupindu hivyo aliwataka wananchi kutofanya mzaha katika kupambana na maradhi hayo.

“Wananchi msifanye mas-hara, tukumbuke mwaka 1978 yalipoibuka kwa kasi maradhi haya...hakuna hata Wilaya moja isiyokuwa na kipindupindu hivi sasa...wananchi mfuate taratibu msiwe wakaidi mkiambiwa msiuze biashara zilizokatatwa msiuze, unadhifu upewe kipaumbele”,alisisitiza Dk. Shein.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo, kuupongeza uongozi wa Mkoa wa Mjini Magharibi pamoja na Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais kupitia Idara yake ya Maafa kwa juhudi wanazozichukua katika kuwapa huduma za lazima wananchi hao ambao nao uongozi huo kwa upande wake ulimuhakikishia Rais kuwa wamejipanga vizuri kutoa huduma stahiki kwa wahanga hao wote.

Wananchi wapatao 420 wapo kwenye kambi hiyo wakiwemo wanawake 240 na wanaume 180 ambapo watoto wadogo walio chini ya umri wa miaka mitano wapo 54 na wazee wa miaka 60 hadi 70 wapo 62, hao wote wanatoka katika Shehia za Kwahani, Welezo na Nyerere katika Wilaya ya Mjini Unguja.

Wakati huo huo, Dk. Shein alitembelea kambi ya kipindupindu iliyopo Chumbuni mjini Unguja na kuwapa pole wagonjwa waliolazwa kambini hapo na baadae kupata maelezo kutoka kwa uongozi wa Wizara ya Afya  ambapo kwa upande wake Dk. Shein aliendelea kusisitiza suala zima la usafi wa maji yanayotumiwa na wananchi sambamba na kuzingatia usafi wa mazingira.

Dk. Ramadhan Mikidadi ambae ni mkuu wa kambi hiyo, alimueleza Dk. Shein kuwa tayari wagonjwa wengi wamefikishwa katika hospitali za Unguja na Pemba tokea kuanza kipindupindu mnamo mwezi Septemba mwaka jana ambapo hivi sasa kuna wagonjwa 1788 wakiwemo 684 ambao hali zao si nzuri na tayari wagonjwa 40 wameshafariki.

Nae Dk. Mohammed Dahoma kwa upande wake alieleza juhudi zinazochukuliwa katika kuwapa elimu wananchi kupitia njia mbali mbali zikiwemo vyombo vya habari, magari  ya sinema  pamoja na kua na azma ya kutoa elimu kwenye simu za mkononi kupitia mtandao wa ZANTEL pamoja na makundi ya WASAP.

Dk. Dahoma alieleza kuwa kuwepo kwa vyanzo mbali mbali vya maji kunachangia kuongezeka kwa maradhi hayo pamoja na baadhi ya wananchi kutotumia dawa za kutia kwenye maji “water guard” kwa kisingizo kuwa zina harufu mbaya sambamba na kupunguza makali na kuwasihi wananchi kuachana na dhana hizo.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.