Habari za Punde

Zanzibar Yaadhimisha Siku ya Malaria Duniani katika Viwanja vya Maisara.

Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi (katikati) akiongoza Matembezi ya hiari ya kuadhimisha Siku ya Malaria Duniani yalioazia katika eneo la Mazizini na kumalizikia katika viwanja vya Maisara Mjini Unguja.kulia yake ni Waziri wa Afya Zanzibar Mahmoud Thabit Kombo na kushoto yake ni katibu Mkuu Wizara ya Afya Dkt  Juma Malik Akili.
Vikundi vya mazoezi vikiwa katika matembezi ya hiari ya kuadhimisha Siku ya Malaria Duniani ambayo yamefanyika kuanzia Mazizini Wilaya ya Magharibi B na kumalizikia Maisara Mjini Unguja.
Vikundi mbalimbali vya Mazoezi vikifanya mazoezi baada ya kuwasili katika Uwanja wa Maisara katika maadhimisho ya Siku ya malaria Duniani ambayo yamefanyika  Mjini Unguja.

Waziri wa Afya Mahmoud Thabit Kombo (wa mwanzo ) akishiriki katika mchezo wa kuvuta  kamba kwenye maadhimisho hayo ambapo timu ya Baraza la Wawakilishi ilipambana na Wizara ya Afya ambapo  Afya ilipata ushindi. 


Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idi akitoa hotuba ya Maadhimisho ya siku ya Malaria Duniani ambayo yamefanyika Maisara Mjini Unguja.kulia yake ni Waziri wa Afya Zanzibar Mahmoud Thabit Kombo na Kushoto yake ni Katibu Mkuu Wizara ya Afya Dkt Juma Malik Akili.(Picha na Yussuf Simai -Maelezo Zanzibar)

Na Mwandishi Wetu.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi amewataka wananchi wa wanaosafiri mara kwa mara  kwa ajili ya harakati zao za maisha kuchukua vyandarua na kuvitumia wanapokuwa safarini ili kujikinga na maradhi ya Malaria.

Akizungumza katika Maadhimisho ya siku ya Malaria Duniani katika viwanja vya Maisara, Mjini Zanzibar, Balozi Seif alisema licha ya Zanzibar kuwa na kiwango cha chini ya asilimia moja cha Malaria, utafiti unaonyesha watu wanaogunduliwa kuugua maradhi hayo hivi sasa ni wale wenye utaratibu wa kusafiri nje ya Zanzibar.

Amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imedhamiria kwa dhati kuimarisha afya za wananchi na itaendelea kuboresha huduma za afya sehemu zote na kuwataka wananchi kuunga mkono juhudi hizo.

Hata hivyo alisema wakati Zanzibar inajivunia mafanikio katika vita dhidi ya Malaria bado maradhi ya Kipindupindu yanaendelea kuwa tishio  kwa wananchi na kuwataka kufuata maelekezo yanayotolewa na wataalamu wa afya.

Mapema Katibu Mkuu Wizara ya Afya Juma Malik Akili alisema katika kumaliza Malaria kuanzia tarehe 25 mwezi huu watatoa vyandarua  760,000 vilivyotiwa dawa bure kwa wananchi katika Wilaya zote za Zanzibar.

Amewashauri wananchi kuvitumia vyandarua hivyo kikamilifu kwani inaonekana kuwa ndio njia kubwa inayosaidia kukinga Malaria.

Katika maadhimisho hayo, wananchi na vikundi vya mazoezi wakiongozwa na Makamu wa Pili wa Rais walifanya matembezi ya hiari yaliyoanza Mazizini, Wilaya ya Magharibi B na kumalizia viwanja vya Maisara, Mjini Zanzibar.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.