Habari za Punde

Dk.Shein: Balozi za Tanzania Nje Ongezeni Kasi ya Utekelezaji wa Sera ya Diplomasia ya Kiuchumi.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
    Zanzibar                                                                                                                                                     20 Mei, 2016
---
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la 

Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema Balozi za 

Tanzania nchi za nje zinapaswa kuongeza kasi ya 

utekelezji wa sera ya diplomasia ya kiuchumi ili 

Tanzania izidi kuendelea kuimarisha uchumi wake.

Dk. Shein alimueleza Balozi mpya wa Tanzania nchini 

Uingereza Mheshimiwa Asha-Rose Migiro ambaye 

alifika ofisi kwake Ikulu kumuaga kuwa Balozi za 

Tanzania nchi za nje zimekuwa zikifanya kazi nzuri 

kuitangaza Tanzania na hivyo kuchangia katika 

kuimarisha uchumi na biashara ikiwemo ya utalii 

nchini.

Katika mazungumzo hayo, Dk. Shein alisema 

uhusiano kati ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania 

na Uingereza una historia kubwa na ni wenye 

mafanikio ya kuridhisha kwa pande zote.

“urafiki wetu na Uingereza una historia ndefu na ndio 

umetuweka katika familia moja ya nchi za Jumuiya ya 

Madola hivyo kuuendeleza na kuuimarisha ni wajibu 

wetu” alisema Dk. Shein.

Alifafanua kuwa nchi hiyo ina ushawishi mkubwa 

ulimwenguni hivyo kuendelea kuwa rafiki wa nchi 

yetu ni jambo la kujivunia na la umuhimu mkubwa 

ambalo tunapaswa kulienzi.

Rais wa Zanzibar alimwambia Balozi Migiro kuwa kwa 

mwaka jana Uingereza ilikuwa nchi ya tatu kwa idadi 

kubwa ya watalii walioitembelea Zanzibar hivyo nchi 

muhimu katika biashara ya utalii kwa Tanzania.

“watalii wakifika Zanzibar wanamaliza shughuli zao 

katika mbuga za wanyama Tanzania Bara 

halikadhalika kwa watalii wanaoanza safari zao 

mbugani Tanzania Bara wengi humalizia Zanzibar” 

Dk.Shein alisema na kubainisha kuwa sekta hiyo ni 

muhimu kwa uchumi wa Zanzibar na Tanzania Bara 

pia.

Alifafanua kuwa sekta ya utalii hivi sasa inachangia 

asilimia 27 ya pato la taifa la Zanzibar huku sekta 

hiyo ikichangia asilimia 80 ya fedha za kigeni.

Aidha alisema kuimarika kwa sekta hiyo inatokana na 

jitihada mbalimbali zikiwemo za balozi za Tanzania 

nchi za nje kuitangaza Zanzibar na kuongeza kuwa 

Zanzibar hivi sasa inapokea wastani wa watalii 

300,000 kwa mwaka kutoka watalii 170,000 mwaka 

2010.

Kwa mwelekeo huo, Dk Shein alibainisha kuwa 

Zanzibar inatarajia kulifikia lengo la kupokea watalii 

500,000 kwa mwaka ifikapo mwaka 2020 kama dira 

ya Zanzibar ya 2020 inavyoelekeza.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kumpongeza Balozi 

Migiro kwa kuteuliwa na Mheshimiwa Rais John 

Pombe Magufuli kushika wadhifa huo ambao alieleza 

kuwa ni heshima kubwa na kwa mtu mwenye uwezo 

kama yeye Dk Migiro.

“Nilipokea kwa furaha uteuzi wako kwa sababu ya 

utendaji wako ambao wakati wote umekuwa wa 

mafanikio” Dk. Shein alimueleza Balozi Migiro.

Kwa upande wake Balozi Asha-

Rose Migiro aliishukuru serikali na uongozi wa 

serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa 

kuendelea kumuamini kwa kumkabidhi majukumu 

hayo muhimu.

“Ahsante kwa Serikali na viongozi wangu kwa 

kuendelea kuniamini na kunipa heshima hii kubwa 

kuiwakilisha nchi yetu nje”Balozi Migiro alieleza.        

Postal Address: 2422 Tel.+255 776 613 015, Fax: 024 2231822 
                                                

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.