Habari za Punde

SHINA INC Yatowa Mafunzo kwa Wanavikundi vya Wanawake Makunduzi Zanzibar.

Rais wa Shirika Lisilo la Kiserekali la SHINA INC Bi Jessica Kamala Mushala, akizungumza na wanawake wa Wilaya ya Kusini Unguja baada ya kumaliza mafunzo yao ya kuweza kuibua miradi kumkomboa mwanamke na mtoto katika kupata kipato, wakati wa hafla ya kukabidhi Vyeti kwa Wanavikundi hivyo Vinne vya Shehia ya Nganani Makunduchi. 

Rais wa Jumuiya ya SHINA INC Tanzania, Jesica Kamala, ametowa wito kwa akinamama nchini kushirikiana na kuimarisha huduma za ulezi kwa watoto, ili waweze kuwa na maisha bora na kupiga hatua ya kielimu.
Rais huyo ametowa changamoto hiyo leo katika hafla ya kukabidhi vyeti kwa vikundi vya ujasiriamali vya shehiya ya Kijini, iliofanyika katika ukumbi wa skuli ya Sekondari Makunduchi.
Jumla ya wanachama 40  kutoka vikundi  vya ‘Mkorofi sio mwenzetu’, ‘Siri Moyoni mwako’, ‘Dhulma sio njema’ na ‘Manufaa yetu’, wamepatiwa vyeti baada ya kumaliza masomo ya miezi mitatu kuhusiana na uendeleezaji wa kilimo cha mboga mboga pamoja na uanzishaji wa biashara ndogo ndogo.
Akizungumza na wanachama hao, Kamala alisema kuna haja kwa akinababa kutoa nafasi na kuwawezesha akinamama ili waweze kuwa wazalishaji na kujiendeleza kimaisha.
Alisema sio lengo la mradi huo kubadilisha tamaduni za asili za wananchi, bali una azma ya kuwawezesha akinamama kiuchumi, na kuondokana na umasikini.
Aliwataka akinamama hao kila mmoja kutoa mchango kwa mwenzake kwa kile anachokifahamu, ili waweze kupiga hatua  za kimaendeleo kwa pamoja.
Aidha aliahidi kuzichukuwa changamoto zinazowakabili na kuwaomba ndugu na marafiki nchini Marekani kusaidia katika kuzipatia ufumbuzi wake.
Mapema katika risala ya wanachama wa vikundi hivyo, iliyosomwa na mwanafunzi Rukia Abdalla, wajasiriamali hao walisema pamoja na mafanikio waliyofikia, wanakabiliwa na changamoto kadhaa, ikiwemo uhaba wa vifaa vya kufanyia kazi na uelewa duni kwa wanachama wake.
Wamesema katika uendeshaji wa vikundi vyao, wanakabiliwa na na mahitaji makubwa, huku uwezo wao kifedha ukiwa duni.   
Hata hivyo risala hiyo imebainisha kuwa vikundi hivyo tayari vimefanikiwa kuzalisha bidhaa mbali mbali zenye thamani ya zaidi ya shilingi Milioni 1.6, ndani ya kipindi cha 2016.
Aidha wameiomba Serikali kuunga mkono na kusaidia shughuli za wajasiriamali hao ili waweze kupiga hatua na kujikwamua katika lindi la umasikini.
Mmoja wa wajasiriamali waliokabidhiwa vyeti hivyo, Vatima Ali, alisema kutokana na mafunzo aliyopata, ameweza kujenga uwezo mkubwa katika uendeshaji wa biashara pamoja na kuongeza uzalishaji wa bidhaa za kilimo.
Alisema hivi sasa anaweza kujiendesha na kumudu kugharamia mambo kadhaa, ambapo kabla ya mafunzo hayo alishindwa kuyamudu.
Jumuiya ya SHINA INC mbali na kujishughulisha na utoaji wa vifaa na misaada mbali mbali ya kijamii, kwa wajane, yatima na watoto/watu wanaoishi katika mazingira magumu, pia hujihusisha na kuwawezesha akinamama katika kuendeleza miradi midogo midogo ya kilimo na biashara, kwa lengo la kujikwamua katika umasikini.

Katika hafla hiyo, mbali na wanachama wote wa vikundi hivyo kupatiwa vyeti, pia walipatiwa mablanket maalum ya kujikinga na wadudu wanaofyonza damu ya binadamu, ikiwemo mbu, kwa lengo la kujikinga na malaria.     

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.