Habari za Punde

Wazee Vitongji: “Tukipewa Mashine ya Nafaka Umaskini Kwaheri”

Na.Haji Nassor - Pemba.

BARAZA la wazee shehia ya Vitongoji wilaya ya Chakechake mkoa wa kusini Pemba, wamesema kama wakipatiwa mashine ya kusagia nafaka, wana uhakika wataondokana na utegemezi, ndani familia zao, kama ilivyo sasa.

Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi, walisema mkombozi wa kweli wanaemfikiria ndani ya baraza lao, sio jambo jengine, bali ni kupatiwa mashine hiyo, ambayo wanaamini haina msimu.

Walisema kutokana na kuanza kupoteza nguvu za kuendeleza kilimo, inakuwa ni vigumu kuwa na miradi inayohitajika kutumia nguvu, bali miradi ya aina hiyo, ndio wanayoimudu.

Katibu wa baraza hilo Ali Juma Khamis, alisema wanaamini kuanzishwa kwa mabaraza hayo, yanayolelewa na JUWAZA na Help Age International Tanzania, kunaweza kuwakomboa, hasa wakiwa na miradi.

Alisema jamii imekuwa ikiwapa kisogo wazee kwa kutowapatia huduma kamili, kama walivyobinadamu wengine, na ndio maana baada ya kujikusanya pamoja ndani ya mabaraza hayo, yanaweza kuwanawirisha.

“Sisi kulima hatuna nguvu tena, lakini kama wafadhili au hata serikali yetu itatupatia mashine kama ya kusagia nafaka, basi tutajiongezea kipato na kuondokana na utegemezi ndani ya familia zetu”,alisema.

Nae mshika fedha wa baraza hilo Jine Ali Abeid, alisema aina yoyote ya miradi, ambayo haihitaji kutumia nguvu sana, inaweza kuwasaidia kujikomboa.

“Hata kama tukipata miradi kama ya ufugaji, biashara ndogo ndogo kwa mujibu mazingira yetu, sisi tunaamini kwa umoja wetu, basi tutafikia pahala pazuri”,alisema.

Kwa upande wake mjumbe wa baraza hilo la wazee shehia ya Vitongoji Ali Omar Abdalla, alisema waliamua ,kujikusanya pamoja ili wawe na sauti moja, ya kutetea haki zao.

Alisema, wazee wanamahitaji kadhaa ikiwa ni pamoja na matibabu kuwa na dirisha pekee la dawa, kwenye vyombo vya usafiri kutokaa foleni, haki ambazo wasipokaa pamoja ni vigumu kutekelezwa.

“Wazee wa shehia hii ambao bado hawajajiunga, muda ndio huu, maana wakikaa pembeni na kisha kudai haki zao inakuwa vigumu kuzipata”,alisema.

Kwa upande wake mlezi wa bara hilo, ambae ni sheha wa shehia hiyo Salim Ayoub Suleima, alisema kutokana na idadi ya wazee 180 walio na umri wa kuanzia miaka 6o na kundelea bado baraza hilo ni dogo.

Alisema wazee wa shehia yake, wanakabiliwa na changamoto kadhaa ikiwa ni pamoja na waliofika umri wa miaka 70 kutopata pencheni jamii, kwa vile hukosa msimazi wa ndani ya shehia yake.

“Naamini wazee hawa wa Vitongoji, sasa kama wakikaa pamoja hakutakuwa na mzee ambae anastahiki kupewa pencheni jamii kukosa, maana itakuwa wanamfuatiliaji”,alieleza.

Mapema Mratibu wa mabaraza ya wazee kisiwani Pemba kutoka JUWAZA, Sifuni Ali Haji, alisema waliamua kuwashawisha wazee, kuanzisha mabaraza hayo, ili wapate kutetea haki zao wakiwa pamoja.

Alifafanua kuwa, wazee wa Zanzibar kama walivyowazee wengine duniani kote, wanazo haki zao mbali mbali ikiwemo wa matibabu, mitaji na kutoa maoni yao katika kuendesha nchi, hivyo kupitia mabaraza hayo itakuwa rahisi.

“Mabaraza haya ya wazee yana malengo mbali mbali, na kama wenyewe  wakiyaendelea yanaweza kupiga hatua kubwa, huku na sisi JUWAZA tukiwa bega kwa bega nayo”,alifafanua.

Shehia ya Vitongoji wilaya ya Chakechake kisiwani Pemba, ina wazee 173 wenye umri wa miaka 70, na wazee 180 wenye umri wa kuwanzia miaka 60 hadi 69, ambapo baraza hilo la wazee lililoanzishwa mwaka jana linawanachama 15.


Katika ziara hiyo ilioratibiwa na Jumuia ya wazee Zanzibar JUWAZA, ilianzia shehia ya Wingwi mapofu na kumalizia shehia ya Vitongoji.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.