Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, akisisitiza jambo wakati wa mazungumzo yake na Waandishi wa Habari wa Vyombo mbalimbali vioko Zanzibar,kuhusiana na Safari yake Nchini Kenya kuhudhuria Mkutano wa Kimataifa wa Uchumi Endelevu (Blue Economy) mazungumzo hayo yamefanyika Ukumbi wa VIP Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume Zanzibar.
Na.Abdi Shamnah.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa
Braza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amesema Serikali ina azma ya kuandaa
mikakati madhubuti ili kufanikisha dhamira ya kuwa na uchumi endelevu wa bahari
(Blue economy).
Hatua hiyo inakwenda sambamba na
uimarishaji wa miundombinu ikiwemo
ujenzi wa bandari kubwa ya kisasa, pamoja na kuwaelimisha wakulima hususan wale
wa kilimo cha mwani.
Dk. Shein amesema hayo leo katika
Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume, wakati alipowasili akitokea
nchini Kenya, alikohudhuria mkutano wa
siku tatu wa Uchumi wa Bhari, akimuwakilisha Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa
Tanzania, Dk. John Pombe Magufuli.
Alipowasili uwanjani hapo, Dk. Shein
na ujumbe wake walipokelewa na Viongozi mbali mbali wa chama na Serikali,
akiwemo Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Idd.
Akizungumza na waandishi wa habari katika
ukumbi wa VIP, Dk. Shein alisema hatua hiyo ni kutekeleza kwa vitendo, miongoni
mwa yale yaliofikiwa na nchi wanachama katika mkutano huo uliomalizika hivi
punde.
Akijibu maswali ya waandishi wa
habari Dk. Shein alisema suala la mafuta na gesi asilia ni miongoni mwa neema
za uchumi wa bahari, na kubainisha kuwa utafutaji wa nishati hiyo umeingia katika awamu ya pili ya utafiti katika eneo
la maji madogo kisiwani Pemba.
Katika hatua nyengine, Dk. Shein
aliwataka waandishi wa habari kuchukuwa nafasi yao katika kuwaelimisha
wananchi juu ya kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi
na athari za kiuchumi zinazojitokeza katika eneo la bahari ili kufanikisha
dhamira ya kufikia uchumi wa viwanda.
No comments:
Post a Comment