Habari za Punde

CCM Itaendelea Kuwajali na Kuwathamini Wazee Kwani Wazee Walitambuliwa Tangu Wakati wa Kudai Uhuru .


Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Wazee wa CCM Wilaya ya Kati Unguja katika ziara yake, mkutano huo umefanyika katika ukumbi wa Kituo cha Walimu Dunga Mkoa wa Kusini Unguja.  
MAKAMO Mwenyekiti wa CCM Zanzibar na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, amesema kuwa ndani ya Chama Cha Mapinduzi ( CCM) Wazee bado hawajapitwa na wakati.
Dk. Shein aliyasema hayo leo wakati alipofanya mazungumzo na Wazee wa CCM wa Wilaya ya Kati Unguja huko katika Ukumbi wa Kituo cha Walimu Dunga, Wilaya ya Kati Mkoa wa Kusini Unguja akiwa anahitimisha ziara zake za kukutana na Wazee wa Unguja na Pemba.
Makamo huyo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar alisema kuwa CCM inaendelea kuwajali, na kuwathamini Wazee kwani wazee walitambuliwa tokea wakati wa kudai uhuru chini ya chama cha ASP na waliweza kushirikia bega kwa bega hadi kupatikana uhuru huo.
Alieleza kuwa kwa kawaida ndani ya chama hicho wanaowaandaa vijana na viongozi ni Wazee hivyo kuna kila sababu ya kuwaenzi kuwatunza na kuwathamini wazee kutokana na umuhimu wao mkubwa walionao katika jamii.
Rais Dk. Shein aliahidi kuendelea kufanya kazi na wazee sambamba na kushirikiana na viongozi wote wa chama hicho wakiwemo wa Jumuiya zote za chama hicho, Wawakilishi na Wabunge ambao wananguvu kubwa katika jamii.
Alisema kuwa kila Wilaya katika Wilaya za Zanzibar zina historia yake lakini Wilaya ya Kati ina historia kubwa tokea ASP kwani ilikuwa ndio ngome ya chama hicho na hivi sasa CCM.
Rais Dk. Shein alieleza historia ya akina mama jinsi walivyopambana katika kudai uhuru wa Zanzibar na hatimae kuruhusiwa kupiga kura kwani walikuwa hawakupata fursa hiyo.
Rais Dk. Shein pia, alitumia fursa hiyo kuahidi kukutana na Jumuiya zote za CCM za Wilaya zote za Unguja na Pemba kama alivyofanya kwa Wazee.
Aliwapongeza wazee kwa kushirikiana na Serikali yao sambamba na kusimamia amani, utulivu, mshikamano na mapenzi kwa wananchi na wanaCCM wengine jambo ambalo limepelekea Zanzibar kuwa salama.
Makamo mwenyekiti huyo wa CCM alisisitiza haja ya kuyaenzi, kuyalinda na kuyaheshimu Mapinduzi ya Januari 12, 1964 kwani ndio yaliyoikomboa Zanzibar pamoja na kuulinda na kuudumisha Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.
Nae Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Abdalla Juma Mabodi alisema kuwa alama anayowaachia Chama ni kuwepo kwa Baraza la Wazee la Makao Makuu ya CCM Kisiwandui.
Alitoa pongezi kwa wazee wa Wilaya ya Kati kwa mashirikiano makubwa wanayoyatoa huku akitoa pongezi kwa ushirikiano wa viongozi wa chama uliopo katika Wilaya ya Kati.
Rais Dk. Shein aliahidi kwamba kwa muda mfupi ujao changamoto ya ukosefu wa walimu wa Sayansi  hapa nchini itaondoka kutokana na mikakati maalum iliyowekwa na Serikali ya kuwasomesha walimu ndani na nje ya nchi.
Nao Wazee wa Wilaya ya Kati Unguja kupitia Baraza lao la Wilaya ya Kati kwa namna ya kipekee waliipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya Awamu ya Saba  anayoiongoza Rais Dk. Shein kwa uwamuzi wake wa kizalendo wa kuwapelekea huduma mbali mbali za kijamii.
Wazee hao wa Wilaya ya Kati walieleza kuwa suala zima la Pencheni Jamii ya kila mwezi wanayoipata wazee wapatao 1977 wa Wilaya ya Kati jambo ambalo kwao ni faraja   ambayo hawakuitegemea.
Walieleza kwamba fedha hizo zinawasaidia kufanya shughuli ambazo zinawainua kiuchumi na kuachana na utegemezi kwani hayo ndio madhumuni ya ASP chini ya uongozi wa Rais wa Kwanza wa Zanzibar Hayati Mzee Abeid Amani Karume.
Kwa upande wa sekta ya afya, wazee hao walieleza kuwa wanafaidika na ujenzi wa vituo vipya vya mama na mtoto katika Shehia ya Umbuji, Mwera, Kiboje Mkwajuni, Bambi na Tunguu.
Aidha, kwa upande wa sekta ya elimu wazee hao walieleza kuwa wamefaidika kwa kiasi kikubwa kupitia sekta hiyo kutokana na kujengewa skuli za Sekondari za kisasa   katika Shehia ya Uroa skuli ya ghorofa, skuli ya Uzini, Tunguu pamoja na maabara kubwa katika skuli ya Unguja Ukuu kaepwani.
Wazee hao wa Wilaya ya Kati walitoa shukurani zao kwa wakulima kuendelea kusaidiwa ambapo Serikali imebeba asilimia 70 ya gharama za pembejeo na wakulima kulipia asilimia 30 tu.
Pamoja na hayo, wazee hao walitumia fursa hiyo kumpongeza Rais Dk. Shein kwa kuitekeleza kwa vitendo Ilani ya Uchaguzii ya CCM kwa kuyabadilisha Mabonde yao ya mpunga kwenda na teknolojia ya Kisasa kwa kuyafanya ya umwagiliaji maji na kupata eka 2095 katika mabonde ya Wilaya hiyo. 
Kwa upande wa mifugo wazee hao walieleza jinsi walivyofaidika na mradi wa “Kopa ngombe lipa ngombe” kwa kuwaongezea kipato wafugaji na kuifanya Wilaya hiyo kuwa ni moja ya watoaji wa maziwa kwa wingi ambapo kwa mwezi wanakusanya lita 31068.
Wazee hao walitoa pongeza kwa Rais Dk.Shein kwa kuwarahisishia harakati zao za maisha kuwa nyepesi kutokana na kuwajengea barabara kila upande katika Wilaya yao ikiwemo barabara ya Jendele hadi Unguja Ukuu, Koani hadi Jumbi inaendelea kujengwa, Umbuji hadi Uroa, Ukongoroni, Charawe hadi Bwejuu inaendelea kujengwa.
Kwa upande wa huduma ya maji, wazee hao walieleza kufurahishwa na ukarabati wa Matangi ya maji Unguja Ukuu kwani hatua hiyo itawafanya watu wa kisiwa cha Uzi na Ng’ambwa kuwa na matumaini ya kupata maji safi na salama.
Nae Mwenyekiti  wa CCM Wilaya ya Kati Aboud Said Mpate alieleza kuwa Wazee wa Wilaya ya Kati wamekuwa na mchango mkubwa kwa viongozi wa Serikali na Chama kutokana na ushauri, maelekezo na mashirikiano makubwa wanayotoa.
Wanampongeza sana katika kazi nzuri anayoifanya katika kuioingoza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na watu wake na kueleza kwua wamekuwa na mashrikiano mazuri.
Wanampongeza jinsi anavyotoa elimu na maelekezo kwa viongozi anapokutana nao na jinsi ya kazi nzuri ya kusimamia Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) hatua ambayo impelekea kupatikana kwa maendeleo na mafaniko makunbwa chini na uongozi wake.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.