Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Ali Mohamed Shein.Aipokeza Kamati ya (ANOCA)


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Rais wa Umoja wa Kamati za Olimpiki za Afrika,(ANOCA) Bw.Mustapha Berraf kulia akiwa na Ujumbe wake walipofika Ikulu Jijini Zanzibar kwa mazungumzo leo,17-11-2019,

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amepongeza uwamuzi wa Umoja wa Kamati za Olympiki kwa kuichagua Zanzibar kuwa mwenyeji wa mkutano wa Makatibu Wakuu wa Kamati za Olympiki za Afrika (ANOCA).

Rais Dk. Shein aliyasema hayo leo Ikulu mjini Zanzibar wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Rais wa Umoja wa Kamati za Olympiki za Afrika Mustapha Berraf akiwa amefuatana na Ujumbe wake.

Katika maelezo yake Rais Dk. Shein alimueleza kiongozi huyo kuwa uwamuzi wa Kamati hiyo ya Olympiki (ANOCA) kwa kushirikiana na Kamati ya Olympiki ya Tanzania (TOC) ni uwamuzi wa busara kwani unaendeleza mahusiano na mashirikiano mazuri yaliopo katika sekta ya michezo kwenye nchi za Bara la Afrika.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kumpongeza Rais huyo wa Umoja wa Kamati za Olympiki za Afrika Mustapha Berraf kwa kuchaguliwa kushika wadhifa huo na kueleza imani yake kwamba mafanikio zaidi yatapatikana katika Bara la Afrika kwenye sekta ya michezo.

Aidha, Rais Dk. Shein alieleza haja kwa Umoja huo kwa mashirikiano na Kamati ya Olympiki ya Tanzania ushirikiane na Wizara ya Vijana, Utamaduni Sanaa na Michezo  pamoja na Wizara ya Habari, Utalii na Mambo ya Kale kutayarisha michezo ya Kimataifa na mashindano mengine hapa Zanzibar kwa lengo la kuimarisha sekta ya utalii, ajira kwa vijana, mashirikiano, amani pamoja na kujenga afya.

Rais Dk. Shein pia alieleza haja kwa Umoja wa Kamati za Olympiki za bara la Afrika (ANOCA) kwa mashirikiano ya Kamati za Olympiki Tanzania (TOC) na Kamati ya Olympiki ya Kitaifa (IOC) kutoa ufadhili wa mafunzo kwa makocha wa michezo mbali mbali ikiwemo riadha, mpira wa miguu na mengineyo.


Rais Dk. Shein pia, alimueleza kiongozi huyo mwenye asili ya nchi ya Algeria, kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ina uhusiano mzuri na wa kihistoria kati yake na Algeria hivyo hatua hiyo itajenga zaidi mashirikiano na uhusiano uliopo.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alimtaka kiongozi huyo pamoja na ujumbe wake kuitumia vizuri nafasi hiyo ya kuja kufanya mkutano wao hapa Zanzibar kwa kuvitembelea vivutio mbali mbali vya kitalii vilivyopo Zanzibar.

Rais Dk. Shein pia, alimueleza kiongozi huyo juhudi za makusudi zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha sekta ya michezo ambayo inahistoria kubwa hapa nchini.

Pia, Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kumueleza Rais huyo wa Umoja wa Kamati za Olympiki za Afrika Mustapha Berraf historia ya Zanzibar katika anga za michezo na jinsi ilivyotambuliwa ndani na nje ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Hata hivyo Rais Dk. Shein alimueleza kiongozi huyo na ujumbe wake kuwa majadiliano na maazimio yatakayofikiwa katika mkutano huo yatakuwa chachu katika kuimarisha sekta ya michezo katika Bara la Afrika.

Nae Rais wa Umoja wa Kamati za Olympiki za Afrika Mustapha Berraf alimueleza Rais Dk. Shein azma ya mkutano wao unaofanyika hapa Zanzibar katika Hoteli ya Verde na kueleza jinsi walivyopata mapokezi mazuri yeye na wajumbe wengine wa mkutano huo.

Kiongozi huyo alitumia fursa hiyo kuipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi wa Rais Dk. Shein kwa kuendeleza na kuimarisha sekta ya utalii hapa nchini na kueleza jinsi Zanzibar inavyovutia.

Hata hivyo, kiongozi huyo wa Kamati ya Olympiki ya Bara la Afrika alimueleza Rais Dk. Shein mashirikiano mazuri yaliopo kati ya Kamati anayoiongoza na ile ya Tanzania hatua ambayo imepekea kufanikisha vyema mkutano huo.

Alisema kwamba mkutano wao huo Mkuu wa 36 utakuwa wa siku mbili ulioanza leo na kuishia kesho  ambao ulitanguliwa na mikutano iliyoanzia Novemba 14 na 15 ambayo ilijumuisha nchi zinazozungumza Kiengereza na tarehe 19 na 20 mwezi huu kutakuwa na mkutano kwa nchi zinazozungumza lugha ya Kifaransa.

Alisema kuwa jumla ya mikutano minne yote itawajumuisha wajumbe hao wakiwemo wajumbe wa (ANOCA), (OS), (IOC) sambamba na matayarisho ya mashinadano ya Olympiki ya Tokyo 2020.

Kiongozi huyo ambaye pia, ni Rais wa Kamati ya Kitaifa ya Olympiki ya Algeria alieleza kuwa mkutano huo wenye wajumbe zaidi ya 150 wote wanatoka katika nchi 54 za Bara la Afrika pamoja na baadhi ya nchi za Ulaya zikiwemo Japan, Switzerland, Hungary na nyenginezo.

Kwa maelezo ya Rais wa Kamati ya Olympiki Tanzania  Gulam Abdallah alisema kuwa mkutano huo pia, umehudhuriwa na Kamati ya Maandalizi ya Olympiki 2020 Tokyo ambayo pia inashiriki katika mkutano huo ambapo pia mkutano huo mbali ya mambo yake mengine pia utajadili shughuli za michezo ya Olympiki kwa Bara la Afrika sambamba na matayarisho ya Olymki 2020 Tokyo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.