Habari za Punde

RC NCHIMBI ATAJA SABABU TATU MUHIMU ZA MAONESHO YA NANENANE 2021 KITAIFA KUFANYIKA KANDA YA KATI DODOMA

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dk. Rehema Nchimbi akihutubia katika kilele cha Maonesho ya Wakulima ya Nanenane Kanda ya Kati  kwenye viwanja vya Nzuguni jijini Dodoma.
Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Stella Ikupa akihutubia wakati wa kilele cha maonesho hayo. Kulia kwake ni Mkuu wa Mkoa wa Singida, Dk. Nchimbi.


Na Richard Mwaikenda, Dodoma
VIONGOZI wa mikoa ya Singida na Dodoma wameiomba Serikali kulikubali ombi lao la Maonesho ya Wakulima ya Nanenane Kitaifa mwaka 2021, yafanyike Kanda ya Kati kwenye viwanja vya Nzuguni jijini Dodoma.
Kauli hiyo aliitoa Mkuu wa Mkoa wa Singida, Dk Rehema Nchimbi wakati wa hafla ya kufunga rasmi Maonesho ya Wakulima ya Nanenane yaliyofanywa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Ulemavu), Stella Ikupa kwenya viwanja hivyo.
Akihutubia katika kilele cha maonesho hayo, mbele ya mgeni rasmi, Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya  Waziri Mkuu (Ulemavu) Stella Ikupa, Dk. Nchimbi alisema  kuwa tayari ombi hilo lilishatumwa serikalini. Waziri Ikupa alijibu kuwa watalifanyia kazi ombi hilo.
Dk. Nchimbi alitaja sababu tatu za kuomba maonesho hayo kufanyika kwenye kanda hiyo kuwa ni; Kuwashukuru wananchi kuchagua viongozi bora kama kauli mbiu ya maonesho hayo wakulima, wafugaji na wavuvi inavyosema kuwa Chagua Viongozi Bora.
Alisema kuwa anaamini bila wasiwasi wowote kuwa Mgombea urais  wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), John Magufuli atashinda kwa kishindo katika Uchaguzi Mkuu mwaka huu kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hivyo itakuwa ni sherehe kubwa kufanyika Dodoma na kutimiza kauli mbiu ya Maonesho Nanenane ya mwaka huu. Maonesho ya Kanda Kati yanashirikisha  mikoa ya Singida na Dodoma.
Sababu nyingine ni kumshukuru Mungu kutuondolea nchini ugonjwa hatari wa Corona hasa baada ya Rais John Magufuli kuwaomba viongozi wa dini zote, wasio na dini pamoja na wananchi kwa ujumla kumuomba Mungu kwa siku awaepushe na ugonjwa huo, tamko ambalo lilitolewa mkoani Dodoma.
Tatu ni kusherehekea Makao Makuu ya Nchi kuwa Dodoma ambayo ipo Kanda ya Kati, kwani hadi sasa ni miaka mitatu imepita tangu Rais John Magufuli atangaze rasmi mwaka 2017,  haijawahi fanyika sherehe ya shukrani kwa jambo hilo muhimu.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.