Habari za Punde

HOTUBA YA MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA FEDHA YA OFISI YA RAIS, FEDHA NA MIPANGO KWA MWAKA WA FEDHA 2021/2022

 



SERIKALI YA MAPINDUZI YA ZANZIBAR 

HOTUBA YA MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI  YA FEDHA YA OFISI YA RAIS, FEDHA NA MIPANGO  KWA MWAKA WA FEDHA 2021/2022 

MHE. JAMAL KASSIM ALI 

WAZIRI NCHI OFISI YA RAIS, FEDHA NA MIPANGO JUNI, 2021

YALIYOMO UKURASA 

 UTANGULIZI.........................................................................................1 MUUNDO WA OFISI YA RAIS, FEDHA NA MIPANGO ........................3 MAJUKUMU MAKUU YA OFISI YA RAIS, FEDHA NA MIPANGO ........3 UTEKELEZAJI WA MAPATO NA MATUMIZI YA OFISI YA RAIS FEDHA  

NA MIPANGO KWA MWAKA WA FEDHA 2020/2021........................4 Mapato ya Ofisi ya Rais Fedha na Mipango..................................4 Matumizi ya Ofisi ya Rais Fedha na Mipango ................................5 UTEKELEZAJI WA BAJETI ZA TAASISI ZA OFISI YA RAIS, FEDHA  

NA MIPANGO KWA JULAI 2020-MACHI 2021...................................12

Bodi Ya Mapato Zanzibar (ZRB)........................................................12

Mfuko wa Barabara(ZRF) ..................................................................13 Mamlaka ya Ununuzi na Uondoaji wa Mali za Umma(ZPPDA) ....13

Mfuko Wa Hifadhi Ya Jamii Zanzibar(ZSSF)......................................16

Benki ya Watu w a Zanzibar (PBZ)....................................................17

Shirika La Bima (ZIC)...........................................................................18 MWELEKEO WA BAJETI KWA TAASISI ZINAZOSIMAMIWA NA OFISI  

YA RAIS, FEDHA NA MIPANGO ..........................................................19 Bodi ya Mapato Zanzibar..................................................................19 Mfuko wa Barabara...........................................................................20 Mamlaka ya Ununuzi na Uondoaji wa Mali za Umma ..................20 Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar................................................21 Benki ya Watu w a Zanzibar PBZ.......................................................21 Shirika la Bima la Zanzibar.................................................................23 MWELEKEO WA BAJETI YA OFISI YA RAIS, FEDHA NA MIPANGO  

KWA MWAKA 2021-2022 ....................................................................24 Vipaumbele vya Ofisi ya Rais Fedha na Mipango ........................24 Makadirio ya Mapato ya Ofisi ya Rais Fedha na Mipango..........25 Makadirio ya Matumizi ya Ofisi ya Rais Fedha na Mipango.........25 Matumizi ya miradi ya maendeleo inayotekelezwa na Ofisi ya  

Rais, Fedha na Mipango kwa mwaka 2021/2022..........................26 SHUKRANI ............................................................................................26 HITIMISHO ............................................................................................26

OR-Fedha na Mipango

A. UTANGULIZI 

1.0 Mheshimiwa Spika, naomba nianze kwa kumshukuru  Mwenyezi Mungu Muumba mbingu na ardhi kwa  kutujaalia neema ya uhai na kutuepusha na kutuhifadhi  majanga ya kilimwengu ikiwemo maradhi, vita na maafa  yanayosababishwa na mabadiliko ya hali ya hewa  ulimwenguni.  

2.0 Mheshimiwa Spika, naomba kuchukua nafasi hii pia  kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa  Baraza la Mapinduzi Dkt. Hussein Ali Mwinyi kwa imani yake  kwangu iliyompelekea kunikabidhi jukumu la kusimamia  Ofisi yake muhimu inayoshughulikia Fedha na Mipango ya  Nchi yetu. Aidha, napenda kuchukua nafasi hii kuwashukuru  wasaidizi wakuu wa Rais wetu ambao ni Makamo wa Kwanza  wa Rais Mheshimiwa Othman Masoud Othman na Makamo  wa Pili wa Rais Mheshimiwa Hemed Suleiman Abdulla ambao  wanashirikiana nae kwa karibu katika kuimarisha umoja na  mashirikiano ambayo ni chachu kwa maendeleo ya nchi  yetu .  

3.0 Mheshimiwa Spika, naomba nikushukuru wewe binafsi, ukiwa  Spika wa Baraza hili, Naibu Spika Mheshimiwa Mgeni Hassan  Juma na Wenyeviti wa Baraza; Mheshimiwa Shaaban Ali  Othman na Mheshimiwa Mwanaasha Khamis Juma, kwa jinsi  mnavyoshirikiana kuliongoza vyema Baraza hili wakati wote.  Pia, natoa shukrani za dhati kwa Kamati ya Uchumi ya Baraza  lako tukufu inayoongozwa na Mwenyekiti wake Mheshimiwa  Shaaban Ali Othman, Makamo wake na wajumbe wote.  Ofisi yetu inafarijika kwa kupokea ushauri na mashirikiano  makubwa tunayoyapata kutoka kwao ambayo yanazidisha  ufanisi katika kutekeleza majukumu ya kazi zetu za kila siku.

OR-Fedha na Mipango

4.0 Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee nachukua nafasi  hii kuwashukuru wapiga kura wangu wa Jimbo la Magomeni  kwa kunichagua kwa imani kubwa na kunipa nafasi kuwa  muwakilishi wao katika Baraza hili. Waliniamini kuwa Mbunge  wao kwa miaka mitano na kwa sasa wameniamini tena  na kunichagua kuwa mwakilishi wao katika Baraza hili.  Nawaahidi sitawaangusha, nitakuwa nao pamoja wakati  wote kwa ajili ya maendeleo ya Jimbo letu na nchi yetu kwa  ujumla. 

5.0 Mheshimiwa Spika, Naomba kuchukua nafasi hii kuungana  na wananchi wenzangu wa Zanzibar kuwaombea dua  viongozi wetu ambao tulikuwa nao pamoja wakati tunalianza  Baraza hili la kumi (10) na leo hii wameshatutangulia mbele  ya haki. Viongozi hawa wametujengea hamasa kubwa  kutokana na weledi, umakini, uaminifu na uadilifu wao  katika kazi utumishi wao ambao umetuwezesha kupiga  hatua kubwa ya maendeleo. Kwa hakika viongozi hawa  wametufunza namna bora ya kulitumikia taifa letu. Mwenyezi  Mungu awalaze pema peponi Marehemu Mzee wetu  Maalim Seif Sharif na Mzee wetu Dkt. John Pombe Magufuli  (Ameen). 

6.0 Mheshimiwa Spika, naomba kutoa shukrani maalum  kwa watendaji wa Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango kwa  mashirikiano wanayonipa katika kutekeleza majukumu yangu  ya Uwaziri katika Ofisi hii. Sote kwa pamoja tunathamini sana  michango maoni na ushauri tunaoupata kutoka wadau  wa Sekta tunayoisimamia pamoja na wananchi wote kwa  ujumla. 

7.0 Mheshimiwa Spika, baada ya shukrani sasa naomba  uniruhusu kuwasilisha mbele ya Baraza hili Makadirio ya  Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango  kwa mwaka wa Fedha 2021/2022 kama ambavyo Katiba ya 

OR-Fedha na Mipango

Zanzibar ya mwaka 1984 imeelekeza ndani ya kifungu cha  88 kifungu kidogo (b) na (d).  

B. MUUNDO WA OFISI YA RAIS, FEDHA NA MIPANGO 

8.0 Mheshimiwa Spika, Kimuundo Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango  imeundwa na mafungu makuu matatu ambayo ni Ofisi ya  Rais, Fedha na Mipango (F01), Mfuko Mkuu wa Serikali (F02)  na Tume ya Mipango (F03). Mafungu hayo yanajumuisha  Idara kumi na tano (15), taasisi nane (8) zinazojitegemea na  ofisi mbili (2) zinazoratibu shughuli za Wizara kwa upande wa  Pemba.  

C. MAJUKUMU MAKUU YA OFISI YA RAIS, FEDHA NA MIPANGO 

9.0 Mheshimiwa Spika, Miongoni mwa majukumu ya Ofisi ya  Rais, Fedha na Mipango ni: 

a. Kusimamia mapato ya Serikali kutokana na vyanzo  mbali mbali. Mapato hayo yanajumuisha mapato ya  ndani ya kodi na yasiokuwa ya kodi, Ruzuku na Mikopo  kutoka kwa Mashirika ya Kimataifa na Nchi Wahisani; 

b. Kusimamia mali za Serikali kupitia usimamizi wa ununuzi,  utunzaji na uondoaji wa mali za Serikali pamoja na Hisa  za Serikali katika Mashirika na Kampuni binafsi ambazo  Serikali inamiliki; 

c. Kusimamia Fedha za Umma na shughuli za Uhasibu  Serikalini. Katika jukumu hili Ofisi inasimamia Bajeti ya  Serikali, usimamizi wa Hazina, huduma za Uhasibu na  ukaguzi wa ndani Serikalini; 

d. Kusimamia Deni la Taifa kwa kutoa ushauri, kujadili deni  na kufuatilia mwenendo wa Deni la Taifa (Mikopo ya  Ndani na Nje) na udhibiti wake;  

e. Ofisi inasimamia maendeleo ya Sekta ya Fedha,  inayohusisha masuala ya Benki, Bima, Hifadhi ya Jamii, 

OR-Fedha na Mipango

Soko la Hisa na Mitaji pamoja na usimamizi wa Taasisi za  huduma ndogo ndogo za fedha; na 

f. Kusimamia Teknologia ya habari na Mawasiliano  (TEHAMA) kupitia mifumo inayohusisha mapato,  matumizi na malipo ya Serikalini. 

10.0 Mheshimiwa Spika, Kwa vile muundo wa Ofisi ya Rais Fedha  na Mipango unajumuisha na Tume ya Mipango. Hivyo,  Ofisi pia inatekeleza majukumu yafuatayo kupitia Tume ya  Mipango: 

g. Kuandaa na kusimamia utekelezaji wa Dira ya  Maendeleo ya Taifa na kuitafsiri kwenye Mipango ya  kipindi cha muda wa kati kwa kuzingatia idadi ya watu  na mahitaji yake; 

h. Kuratibu na kusimamia maendeleo ya uchumi kupitia  Sekta za Kiuchumi na Kijamii; 

i. Kuratibu Sera za Kisekta na upunguzaji wa umaskini  nchini; 

j. Kusimamia upatikanaji na utoaji wa takwimu rasmi kwa  maendeleo ya nchi; na 

k. Kufuatilia na kutathmini utekelezaji wa mipango ya  kitaifa na kimataifa. 

D. UTEKELEZAJI WA MAPATO NA MATUMIZI YA OFISI YA RAIS,  FEDHA NA MIPANGO KWA MWAKA WA FEDHA 2020/2021 

D.1 Mapato ya Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango 

11.0 Mheshimiwa Spika, kabla sijawasilisha muelekeo kwa  upande wa ukusanyaji wa Mapato na Matumizi ya Ofisi  ya Rais, Fedha na Mipango, kwa ruhusa yako naomba  kuwasilisha muhtasari wa Makadirio ya Mapato na Matumizi  kwa mwaka 2020/2021 kama ifuatavyo: Ofisi hii ilipangiwa  kusimamia na kukusanya Mapato yaliyokadiriwa kufikia  jumla ya TZS 1.549 trilioni kutoka vyanzo mbali mbali. 

OR-Fedha na Mipango

12.0 Mheshimiwa Spika, Kwa kipindi cha Julai hadi Machi mwaka  wa fedha 2020/21, mapato halisi yaliyokusanywa na Ofisi ya  Rais, Fedha na Mipango yalifikia Jumla ya TZS 678.79 bilioni  sawa na asilimia 44 ya makadirio ya mwaka ya kukusanya  TZS 1.549 trilioni na pia ni sawa na asilimia 70 ya kukusanya  TZS 965.73 bilioni ndani ya kipindi cha Julai 2020- Machi 2021.  Uchambuzi wa mapato hayo ni kama ufuatavyo: 

a. Bodi ya mapato ilikusanya TZS 223.3 bilioni sawa na  asilimia 43 ya makadirio ya mwaka na pia ni sawa na  asilimia 74 ya makadirio ya kipindi cha miezi tisa; 

b. Mamlaka ya Mapato (TRA) imekusanya TZS 209.1 bilioni  sawa na asilimia 55 ya makadirio ya mwaka na pia ni  sawa na asilimia 92 ya makadirio ya kukusanya TZS 228.4  bilioni kwa kipindi cha miezi tisa;  

c. Mapato kutoka kwa Washirika wa Maendeleo ya TZS  119.6 bilioni sawa na asilimia 29 ya makadirio ya TZS 419.4  bilioni kwa mwaka na sawa na asilimia 39 ya matayajio  ya kupokea TZS 306.0 bilioni kwa kipindi cha miezi tisa.  Kati ya Fedha hizo TZS 106.4 bilioni ni Mikopo na TZS 13.23  bilioni ni Ruzuku; na 

d. Misaada ya Kibajeti (GBS) ya TZS 9.46 bilioni; 

e. Fedha za Mfuko wa pamoja wa Washirika wa Maendeleo  ni TZS 2.6 bilioni sawa na asilimia 68 ya makadirio ya  mwaka ya kupokea TZS 3.9 bilioni. 

f. Mapato yasiyokuwa ya kodi yaliyokusanywa na fungu  F01-Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango ni TZS 51.06 bilioni  sawa na asilimia 32 ya makadirio ya kukusanya TZS  159.9 bilioni, pia ni sawa na asilimia 96 ya makadirio ya  kukusanya TZS 53.44 bilioni kwa kipindi cha miezi tisa. 

D.2 Matumizi ya Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango  

13.0 Mheshimiwa Spika, kwa upande wa matumizi Ofisi ya Rais,  Fedha na Mipango ilipangiwa kutumia TZS 442.93 bilioni 

OR-Fedha na Mipango

kwa mafungu ya Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango ya F01,  F02 na F03 Kwa ujumla Mafungu haya yametumia TZS179.82  bilioni ambazo ni sawa na asilimia 41 ya makadirio ya TZS  442.43 bilioni ya mwaka. Kati ya fedha hizo, TZS 37.94 bilioni  zilitumika kwa upande wa Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango  (F01), TZS 136.47 bilioni zilitumika kwa matumizi ya Mfuko  Mkuu wa Serikali (F02) na TZS 5.40 bilioni ni matumizi ya Tume  ya Mipango (F03) . 

14.0 Mheshimiwa Spika, Mchanganuo wa matumizi ya F01 na F03  kimafungu ni kama ifuatavyo: 

i. Mshahara ni TZS 7.4 bilioni; 

ii. Ruzuku kwa Taasisi zilizo chini ya Ofisi ya Rais Fedha na  Mipango ni TZS 22.78 bilioni; 

iii. Matumizi Mengineyo (OC) ni TZS 5.26 bilioni; na iv. Matumizi ya kazi za Maendeleo ni TZS 7.29 bilioni. 

15.0 Mheshimiwa Spika, kwa upande wa matumizi program  zinazosimamiwa kwa Fungu F01, fedha zilizotumika ni kama  ifuatavyo:  

a. Programu ya bajeti na Usimamizi wa Fedha za umma  ilikadiriwa kutumia jumla ya TZS 47.48 bilioni. Hadi kufikia  Machi 2021, program hii imetumia TZS 24.91bilioni  sawa na asilimia 52 ya makadirio ya mwaka. Shughuli  zilizotekelezwa ni pamoja na: 

i. Kusimamia ukusanyaji wa mapato ya Serikali ya TZS  678.79 bilioni ambazo zimekusanywa kwa kipindi  cha tathmini; 

ii. Kuandaa na Kusimamia vikao 9 vya ukomo wa  mapato na matumizi ya Serikali (Ceiling Committee); iii. Uimarishaji wa Mfumo wa Udhibiti wa Matumizi  Serikalini – IFMlS na kuunganisha Mfumo huu katika  Ofisi za Baraza la Mji Mkoani, Kaskazini A, Wilaya ya  Kati, Manispaa za Mjini, Magharibi A na B; 

OR-Fedha na Mipango

iv. Kuhudhuria vikao 12 vya Usuluhishi wa madeni ya  nje baina ya Zanzibar na Tanzania Bara; na 

v. Kuwapeleka mafunzo wafanyakazi 25 ili waweze  kufanya mitihani ya IPSAS na CPA; 

vi. Kufuatilia utekelezaji wa Bajeti ya Serikali kwa kipindi  cha miezi tisa (9); 

vii. Kufanya Uhakiki na Ufatiliaji wa Malipo ya Mishahara  kwa Idara Maalumu za SMZ; 

viii. Kurekebisha mfumo wa malipo ya mishahara;  ix. Kuandaa majukwaa la Bajeti na Uchumi kwa Serikali  kuu na Serikali za Mitaa;  

x. Kushiriki mikutano 4 ya Benki ya Dunia na Shirika la  Fedha Duniani, kuendelea na maandalizi ya Mradi  wa Kuimarisha Ukuaji wa Uchumi (BIG-Z);  

xi. Kukamilisha kwa Ukaguzi wa Mfumo wa usimamizi  wa matumizi (IFMS); na 

xii. Kukamilisha kwa ripoti ya Ukaguzi wa ndani ya  mwaka wa Fedha 2019/2020. 

b. Pogramu ya Usimamizi na Uwekezaji wa Mali za Umma. 

16.0 Mheshimiwa Spika, Lengo la programu hii ni Kusimamia mali  za Serikali kupitia usimamizi wa ununuzi, utunzaji na uondoaji  wa mali za Serikali pamoja na Hisa za Serikali katika Mashirika  na Kampuni binafsi ambazo Serikali inamiliki. Programu hii  imetumia TZS 6.93 bilioni sawa na asilimia 27 ya makadirio ya  mwaka TZS 25.28 bilioni. Shughuli zilizotekelezwa ni pamoja  na: 

i. Ukaguzi, uhakiki na uthamini wa Mali za Serikali katika  Wizara kumi na tatu (13) na taasisi zake; 

ii. Kusimamia uondoshwaji wa mali chakavu katika Wizara  kumi na tatu (13) na taasisi zake; 

iii. Kukagua na kutathmini hesabu za mashirika ya Serikali  na kufuatilia ukusanyaji wa Gawio la TZS 8.44 bilioni; na

OR-Fedha na Mipango

iv. Kulipia fedha za ujenzi wa jengo la Ofisi za Mahkama  zinazojengwa Tunguu TZS 4.92 bilioni; 

v. Kukamilisha mapitio ya Sheria ya Usimamizi wa Mitaji  ya Umma ya mwaka 2002 na kukamilisha Mswaada  wa Sheria mpya itakayoshika nafasi ya Sheria hii iliyopo  sasa. 

c. Programu ya Mipango na Uendeshaji wa Sekta ya  Fedha.  

17.0 Mheshimiwa Spika, Lengo la Programu hii ni kuimarisha  uendeshaji wa shughuli za Sekta ya Fedha. Programu hii  ilipangiwa kutumia jumla ya TZS 56.22 bilioni. Hadi kufikia  Machi 2021, TZS 6.12 bilioni zimetumika sawa na asilimia 11  ya makadirio ya mwaka. Shughuli zilizotekelezwa ni pamoja  na:  

i. Kuratibu uendeshaji wa vikao 16 vya Kamati ya Uongozi,  Kamati Tendaji na Kamati ya Ukaguzi; 

ii. Kuratibu vikao 18 vya Bodi ya Zabuni; 

iii. Kukarabati maeneo ya Ofisi za Unguja;  

iv. Kuratibu vikao vya Uchambuzi wa takwimu za fedha za  Serikali kuu hadi kufikia mwaka wa fedha 2019/2020 ; v. Kuratibu vikao 16 vya Bodi ya Rufaa na Baraza la Rufaa  za Kodi la Zanzibar;  

vi. Kukamilisha Mswaada wa Sheria ya Usimamizi wa Taasisi  zinazotoa huduma ndogo za fedha; na 

vii. Kuratibu Shughuli za Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango  kwa upande wa Pemba. 

d. Matumizi ya Mfuko Mkuu wa Serikali 

18.0 Mheshimiwa Spika, program ya Usimamizi wa Mfuko Mkuu  lengo lake ni kusimamia huduma za Mfuko Mkuu wa Serikali.  Kwa kipindi cha Miezi tisa (Julai 2020 – Machi 2021), Programu 

OR-Fedha na Mipango

ya Usimamizi wa Mfuko Mkuu wa Serikali imetumia jumla ya  TZS 136.47 bilioni sawa na asilimia 57 ya makadirio ya kutumia  TZS 239.23 bilioni kwa mwaka. Matumizi hayo yalitumika kwa  kutekeleza shughuli zifuatazo: 

i. Malipo ya Riba na Mikopo TZS ni 13.495 bilioni; ii. Malipo ya mafao ya Kiinua mgongo kwa wastaafu 885  wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni TZS 15.864 bilioni; iii. Malipo ya Pencheni kwa wastaafu 14,084 wa Serikali ya  Mapinduzi ya Zanzibar ni TZS 22.783 bilioni; na 

iv. Kulipa matumizi Mengineyo ya Serikali ya Mapinduzi ya  Zanzibar ni TZS 84.331 bilioni. 

e. Programu ya Kuratibu Mipango ya Kitaifa na Maendeleo  ya Watendakazi 

19.0 Mheshimiwa Spika, Lengo la program hii ni kuimarisha  uratibu wa mipango ya maendeleo ya Kitaifa na kufanya  ufuatiliaji na tathmini wa mipango hiyo. Katika kipindi cha  Julai 2020 – Machi 2021 programu hii imetumia jumla ya TZS  2.5 billioni sawa na asilimia 66.8 ya makadirio ya mwaka ya  TZS 3.78 bilioni. Shughuli zilizotekelezwa ni pamoja na: 

i. Dira ya Maendeleo 2050 imekamilika na imezinduliwa na  Jumla ya nakala 600 zimechapishwa na kusambazwa  kwa wadau; 

ii. Rasimu ya Mpango wa Maendeleo wa muda wa kati  2021/25 rasimu imekamilika; 

iii. Wafanyabiashara 50 wamepatiwa mafunzo juu ya  uendeshaji biashara na utunzaji wa fedha ili kurasimisha  biashara zao katika Wilaya ya ChakeChake Pemba.  

iv. Ziara ya Ufuatiliaji na Tathmini ya Programu/Miradi  ya Maendeleo imefanyika kwa Unguja na Pemba na  kutembelea miradi jumla ya miradi sitini na tano (65) 

OR-Fedha na Mipango

pamoja na kuandaa ripoti; 

v. Kufanya Tathmini ya utekelezaji wa Dira ya Maendeleo  ya 2020 na kuiwasilisha kwa wadau mbalimbali;  

vi. Kufanya Tathmini ya utekelezaji wa Mkakati wa Kukuza  Uchumi na Kupunguza Umaskini (MKUZA III); na 

vii. Kukamilisha Mfumo wa kielektroniki wa Ufuatiliaji na  Tathmini. 

f. Programu ya Usimamizi wa Uchumi Mkuu na Takwimu 

20.0 Mheshimiwa Spika, Lengo la program hii ni kuandaa sera za  kiuchumi na kufanya tafiti za kiuchumi na kijamii kutokana na  vipaumbele vya Taifa. Hadi kufikia Machi 2021 programu hii  imetumia jumla ya TZS 1.9 bilioni ambayo ni sawa na asilimia  11.3 ya makadirio ya mwaka ya TZS 17.35 bilioni. Shughuli  zilizotekelezwa ni pamoja: 

i. Kutoa ripoti kumi na tatu za hali ya uchumi Zanzibar; ii. Kuwapatia mafunzo Wafanyakazi 30 juu ya namna ya  ukusanyaji wa taarifa za kiuchumi katika Sekta ndogo  ya mazao;  

iii. Kuwapatia mafunzo Wanahabari 20 wa vyombo  mbalimbali kisiwani Pemba juu ya namna bora ya  kuhabarisha umma kuhusu matokeo ya tafiti mbali  mbali; 

iv. Kukusanya taarifa za tafiti 320 za sekta ya uvuvi nchini  kwa lengo la kuzitambua na hapo baadae kuzichakata  na kushajiiisha matumizi ya matokeo yake katika  kutatua chamgamoto mbalimbali za sekta ya uvuvi  nchini; 

v. Utayarishaji wa vipaumbele vya tafiti vya kisekta na  kupata rasimu ya awali ya ajenda ya utafiti ya Zanzibar  ya mwaka 2021-2026;

OR-Fedha na Mipango 10 

vi. Kutayarisha maandiko kwa ajili ya kutafuta ufadhili wa  shughuli za kujenga uwezo watafiti wa kutoka taasisi  za utafiti , Taasisi za elimu ya juu pamoja na vitengo vya  utafiti vya wizara; 

vii. Ripoti mbalimbali za kitakwimu za kila mwezi, robo  mwaka na mwaka zimetolewa kama vile ripoti za kila  mwezi za Faharisi ya Bei ya Mlaji (Consumer Price Index -  CPI) na ripoti ya takwimu za robo mwaka za takwimu za  Pato la Taifa (Growth Domestic Product – GDP) ikiwa ni  pamoja na kuwasilisha na kusambaza ripoti ya matokeo  ya Utafiti wa Mapato na Matumizi ya Kaya wa mwaka  2019/2020(HBS 2019/2020). 

g. Programu ya Utawala na Uendeshaji wa Tume ya  Mipango 

21.0 Mheshimiwa Spika, lengo la programu hii ni kusimamia  shughuli za utendaji na utumishi ndani ya Tume ya Mipango  na kuhakikisha kazi zote zinatekelezwa kwa umakini na ufanisi.  Kwa mwaka 2020/2021 programu hii ilitengewa jumla ya TZS  2.55 bilioni, ambapo hadi kufikia Machi 2021, imetumia jumla  ya TZS 913.20 milioni ambayo ni sawa na asilimia 35.76 ya  makadirio. Utekelezaji kwa program ni kama ifuatavyo:  

i. Wafanyakazi kumi na saba wamepatiwa mafunzo, kati  ya hao wafanyakazi wawili mafunzo ya muda mfupi na  wafanyakazi kumi na tano mafunzo ya muda mrefu  katika fani zinazohusiana na kada zao;  

ii. Jumla ya vikao vitatu vimefanyika kwa wadau Unguja  na Pemba kwa ajili ya kukusanya maoni na kuboresha  Mkataba wa Huduma kwa Umma wa Tume ya Mipango  Zanzibar; 

iii. Wafanyakazi thamanini na tisa wa Unguja na Pemba  wamepatiwa mafunzo ya ndani (Inhouse training)  kuhusiana na miongozo mbali mbali ya kisheria pamoja  na Mfumo wa Upandishwaji Vyeo kwa Watumishi wa 

OR-Fedha na Mipango 11 

Umma;  

iv. Vikao kumi na sita vimeratibiwa; vikiwemo Kikao kimoja  cha Tume ya Mipango , kumi na nne bodi ya Zabuni na  Tathmini na viwili Ukaguzi wa Hesabu za ndani; na  

v. Kutoa huduma za kiutawala na kiuendeshaji zikiwemo  usafiri, ununuzi wa mafuta, vifaa vya kuandikia, pamoja  na ununuzi wa vitendea kazi. 

E. UTEKELEZAJI WA BAJETI ZA TAASISI ZA OFISI YA RAIS, FEDHA  NA MIPANGO KWA JULAI 2020-MACHI 2021 

E.1 Bodi Ya Mapato Zanzibar (ZRB) 

22.0 Mheshimiwa Spika, Bodi ya Mapato Zanzibar ni Wakala  Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wa kukusanya  mapato yatokanayo na kodi. Kwa mwaka wa Fedha  2020/2021, ZRB ilikadiriwa kukusanya jumla ya TZS 516.73  bilioni. Hadi kufikia Machi 2021, Bodi ya mapato imekusanya  jumla ya TZS. 223.34 bilioni sawa na asilimia 43 ya makadirio  ya mwaka.  

23.0 Mheshimiwa Spika, Kwa upande wa matumizi, Bodi ya  Mapato Zanzibar ilikadiriwa kutumia TZS 33.12 bilioni kwa  ajili ya kutekeleza kazi zake. Hadi kufikia Machi 2021 Bodi ya  Mapato Zanzibar imetumia jumla ya TZS 16.71 bilioni sawa na  asilimia 50 ya makadirio ya mwaka. Kati ya Fedha hizo TZS 5.60  bilioni zimetumika kwa kazi za maendeleo na TZS 11.10 bilioni  zimetumika kwa kazi za kawaida. Shughuli zilizotekelezwa nia  pamoja na : 

i. Kufuatilia ugomboaji wa madeni ya TZS 12.41 bilioni  yaliyokuwa hayajalipwa kutoka kwa walipa kodi  mbalimbali. Kwa kipindi cha miezi tisa jumla ya TZS 9.70  bilioni sawa na asilimia 78 ya madeni yote yalilipwa; 

ii. Kukamilisha kutengeneza Mfumo wa ZRB wa Kukadiria 

OR-Fedha na Mipango 12 

Mapato yatakayokusanywa (A Robust Zanzibar Revenue  Forecasting Model for Zanzibar Revenue Board); 

iii. Kukamilisha kazi ya kutengeneza Kituo cha Huduma  kwa Walipakodi (ZRB Contact Centre); 

iv. Kusajili walipakodi wapya 896 sawa na asilimia 108 ya  makadirio ya walipakodi 830 waliotarajiwa kusajiliwa;  na  

v. Kukamilisha na ujenzi wa jengo la Ofisi Pemba katika  maeneo ya Gombani. 

E.2 Mfuko wa Barabara (ZRF) 

24.0 Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2020/2021 Mfuko  wa Barabara umeendeleza jukumu la kuimarisha utunzaji  wa fedha zinazokusanywa kwa ajili ya matengenezo ya  barabara. Hadi kufikia Machi 2021, matumizi ya Mfuko  yamefikia TZS 5.5 bilioni sawa na asilimia 36 ya makadirio ya  mwaka ya TZS 15.14 bilioni. Kati ya matumizi hayo jumla ya  TZS 3.5 bilioni zimetumika kwa matengenezo ya barabara  kuu sawa na asilimia 44 ya makadirio ya mwaka ya TZS 8.04  bilioni, na TZS 1.1 bilioni zililipwa kwa kazi za matengenezo  ya barabara za ndani sawa na asilimia 21 ya makadirio ya  mwaka ya TZS 5.36 bilioni. 

E.3 Mamlaka ya Ununuzi na Uondoaji wa Mali za Umma (ZPPDA) 

25.0 Mheshimiwa Spika, Lengo la Mamlaka ni kusimamia  utekelezaji wa Sheria ya Ununuzi na Uondoaji wa Mali za  Umma, namba 11 ya mwaka 2016. Kwa mwaka wa fedha  2020/2021, Mamlaka ya Ununuzi na Uondoaji wa Mali za  Umma imepangiwa kukusanya jumla ya TZS 325.00 milioni  kutoka katika vianzio vyake mbali mbali vya mapato. Hadi  kufikia Machi 2021 Mamlaka imekusanya jumla ya TZS  94 milioni ambayo ni sawa na asilimia 29 ya makadirio ya  mwaka.

OR-Fedha na Mipango 13 

26.0 Mheshimiwa Spika, Kwa upande wa matumizi, hadi kufikia  mwezi Machi 2021, Mamlaka imetumia jumla ya TZS 833.00  milioni sawa na asilimia 43 ya kupokea ruzuku ya TZS 1.94  bilioni kwa ajili ya kutekeleza shughuli zake zikiwemo  zifuatazo: 

i. Kukagua taasisi 29 za ununuzi kama zifuatazo;- Wizara ya  Ardhi, Nyumba na Nishati, (OR) Tawala za Mikoa Serikali  za Mitaa na Idara maalum za SMZ, Wizara ya Ujenzi  Mawasiliano na Usafirishaji, Wizara ya Vijana Utamaduni  Sanaa na Michezo, Tume ya Utumishi Serikalini, Tume  ya Maadili ya Viongozi wa Umma, Wizara ya Kilimo  Maliasili Mifugo na Uvuvi, Tume ya Kurekebisha Sheria,  Tume ya Uchaguzi na Baraza la manispaa magharibi.  Aidha, Mamlaka kwa upande wa Mashirika imekagua  Shirika la Magazeti, Shirika la huduma za Maktaba,  Baraza la Manispaa Magharib “B”, Shirika la nyumba  Zanzibar, Shirika la Biashara (ZSTC), Shirika la Bandari  Zanzibar, Bodi ya Uhaulishaji, Wizara ya fedha na  Mipango (ujenzi wa nyumba za Kwahani), Halmashauri  ya wilaya ya Micheweni pamoja na mapitio ya ripoti  za tathmini, Baraza la manispaa mjini, Wakala wa  Serikali wa uchapaji Unguja, Kamisheni ya Utalii Unguja,  Ripoti za tathmini za taasisi nunuzi, Wakala wa Chakula  Dawa na Vipodozi, Mamlaka ya mafunzo ya amali  Unguja, Halmashauri ya wilaya ya Micheweni, Wakala  wa Uchapishaji Pemba, Baraza la Mji Chake Chake na  Kamisheni ya Utalii; 

ii. Kufanya uchunguzi kwa Taasisi 5 za ununuzi na Uondoaji  wa Mali za Umma. Kati ya Hizo ni Mamlaka ya Mafunzo  ya Amali juu ya ujenzi wa uzio Vitongoji Pemba, maabara  ya usindikaji chakula, ujenzi wa mji mpya wa Kwahani  Zanzibar, Halmashauri ya wilaya ya micheweni juu ya  ujenzi wa ukumbi (hall) na utekelezaji wa mikataba  katika Shirika la Biashara la Taifa (ZSTC);

OR-Fedha na Mipango 14 

iii. Kuandaa na kutoa miongozo ya ununuzi na uondoaji  wa mali za umma, Kutengeneza nyaraka za zabuni  (standard bid documents) nane (8) Nyaraka zilizo  andaliwa kama zifuatazo: 

a. Nukuu za bei kwa bidhaa (Quotation national  shopping of goods); 

b. Nukuu za bei kwa kazi (Quotation national shopping  of works); 

c. Nyaraka ya ununuzi wa bidhaa (Standard tender  document for procurement of general goods); d. Nyaraka za ununuzi wa huduma ya ushauri  

elekezi wa kitaalamu kwa kampuni na mtu binafsi  (Standard request for proposal (RFP) for selection  of consultants under competitive and individual  selection); 

e. Nyaraka za ununuzi wa kazi (Standard tender  documents for procurement of works); 

f. Nyaraka za ununuzi wa kazi zenye thamani ndogo  (Standard tender document for procurement of  smaller works);  

g. Nyaraka za ununuzi wa huduma ya ushauri elekezi  usiokuwa wa kitaalamu kwa kampuni na mtu binafsi  (Standard tender documents for procurement of  non-consultancy services);  

h. Nyaraka zinazotumika katika uondoaji wa mali za  umma (Standard bidding document for disposal of  fixed assets”). 

iv. Kutoa mafunzo kwa taasisi 118 za Serikali juu ya  miongozo ya Ununuzi na Uondoaji wa mali za Umma  kwa Wakuu wa vitengo vya manunuzi, Kati ya hizo  Unguja 86 na Pemba 32; na  

v. Kuwajengea uwezo wafanyakazi wanne (4) mafunzo  ya muda mrefu na watatu (3) muda mfupi.

OR-Fedha na Mipango 15 

E.4 Mfuko Wa Hifadhi Ya Jamii Zanzibar - ZSSF 

27.0 Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2020/2021 Mfuko  wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar umeendelea kutoa huduma  kwa wanachama wake kwa kukusanya michango yao na  kuwekeza fedha hizo katika miradi salama na yenye faida  kwa lengo la kulipa mafao kwa wanachama muda unapofika  kwa mujibu wa Sheria ya Mfuko Namba 10 ya mwaka 2016.  Kwa mwaka wa fedha 2020/2021 Mfuko ulikadiria kukusanya  mapato ya jumla ya TZS 145.20 bilioni kutoka katika vyanzo  vikuu viwili. Hadi kufikia Machi 2021 Mfuko umekusanya  jumla ya TZS 89.92 bilioni sawa na asilimia 61 ya makadirio  ya mwaka. Kati ya mapato hayo michango ya wanachama  ni TZS 57.23 bilioni sawa na asilimia 61 ya makadirio ya TZS  93.61bilioni na mapato kutoka katika uwekezaji wa Mfuko  ni TZS 32.69 bilioni sawa na asilimia 63 ya TZS 51.59 bilioni  makadirio ya mwaka. 

28.0 Mheshimiwa Spika, Kwa upande wa matumizi Mfuko  ulipanga kutumia Jumla ya TZS 145.20 bilioni. Kati ya fedha  hizo TZS 9.36 bilioni ni gharama za uendeshaji, TZS 38. 26 bilioni  kulipia Mafao ya wanachama wa Mfuko na TZS 97.58 bilioni  kwa ajili uwekezaji. Hadi kufikia Machi 2021, Mfuko umetumia  jumla ya TZS 89.92 bilioni sawa na asilimia 62 ya makadirio ya  mwaka. Kati ya fedha hizo gharama za uendeshaji zilikuwa  ni TZS 6.16 bilioni, TZS 33.32 bilioni ni malipo ya Mafao kwa  wanachama na TZS 50.45 bilioni kwa ajili ya uwekezaji wa  Mfuko.  

E.5 Benki ya Watu wa Zanzibar - PBZ 

29.0 Mheshimiwa Spika, Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ) ni Taasisi  inayomilikiwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Benki hii  inatoa huduma za benki ya Kawaida (Conventional) na 

OR-Fedha na Mipango 16 

huduma za Benki ya Kiislam (Islamic Banking). Kwa kipindi  cha Julai 2020 hadi Machi 2021 benki ilitarajia kupokea  kutoka kwenye vyanzo vyake vya riba na visivyo na riba TZS.  73.09 bilioni na kufanikiwa kupokea TZS 59.59 bilioni sawa  na asilimia 82 ya makusanyo ya kipindi hicho. Makusanyo  hayo ni upungufu wa asilimia 18 ya lengo, upungufu huu  ulisababishwa na kuzorota kwa biashara hasa ya fedha za  kigeni iliosababishwa na mripuko wa maradhi ya COVID 19. 

30.0 Mheshimiwa Spika, Kwa upande wa matumizi Benki ilitumia  TZS 38.00 bilioni sawa na asilimia 76 ya makadirio ya TZS 49.70  bilioni iliyojipangia kwa kipindi cha tathmini. Matumizi ya Benki  kwa kipindi hicho yalipungua kwa asilimia 24 ukilinganisha na  makadirio, hali hii imesababishwa na kupungua kwa baadhi  ya shughuli za kawaida za benki kutokana na kuzorota  kwa biashara katika kipindi hicho. Mbali na changamoto  za kibiashara zilizojitokeza, hadi kufikia Machi 2021 Benki  ilifanikiwa kupata faida ya TZS. 21.6 bilioni amabayo ni  upungufu kwa asilimia 8 ya lengo la TZS 23.42 bilioni. 

31.0 Mheshimiwa Spika, Hadi kufikia Machi 2021, Benki ilifanikiwa  kuongeza mikopo kutoka TZS 420.36 bilioni mpaka TZS 489.22  bilioni amabayo ni pungufu kwa asilimia 0.2 ya malengo ya  kufikia TZS 490.36 bilioni. Rasilimali (Assets) zimeendelea kukua  kutoka TZS 800.36 bilioni mpaka kufikia TZS 809.53 bilioni kwa  mwezi wa Machi 2021. Aidha, amana za wateja (deposits)  zimekua kwa asilimia 2 kwa mwezi wa Machi 2021 kutoka TZS  598.81 bilioni hadi kufikia TZS 610.27 bilioni na Mtaji wa benki  umekua kutoka TZS 95.966 bilioni Julai 2020 hadi TZS 119.53  bilioni kwa mwezi wa Machi 2021, ongezeko hilo ni sawa na  asilimia 5 ya kiwango kilichotarajiwa cha TZS. 114.14 bilioni.

OR-Fedha na Mipango 17 

E.6 Shirika La Bima - ZIC 

32.0 Mheshimiwa Spika, Shirika limeendelea na kazi ya kutoa  huduma ya bima kwa wateja pamoja na kuongeza mapato  kutoka vyanzo vyake mbalimbali. Katika kipindi cha miezi tisa  Julai 2020 - Machi 2021 pamoja na kuwepo na changamoto  mbalimbali katika soko la Bima Tanzania bado Shirika  limeweza kukusanya jumla ya TZS 17.2 bilioni sawa na asilimia  59 ya makadirio ya kukusanya TZS 29.10 bilioni. 

33.0 Mheshimiwa Spika, kwa Upande wa matumizi Shirika  limetumia jumla ya TZS 12.7 bilioni ambayo ni sawa na  asilimia 95 ya matumizi ya mwaka ya TZS 13.3 bilioni. Kati ya  Fedha hizo matumizi ya kawaida ni TZS 5.9 bilioni na matumizi  ya maendeleo ni TZS 6.8 bilioni. Shirika katika kipindi hicho  Julai 2020 - Machi 2021 limetekeleza shughuli zake zikiwemo  zifuatazo:- 

i. Kulipa madai halali yaliyowasilishwa na yaliyohakikiwa  ya TZS 5.3 bilioni kutoka kwa wateja wake walioathirika  wa majanga mbalimbali ya ajali; 

ii. Kulipa ujira wa TZS 1.5 bilioni kwa mawakala 87 na  madalali 16 wanaofanya biashara ya kuuza Bima kwa  niaba ya Shirika; 

iii. Kununua vitendea kazi vyenye thamani ya TZS 35 milioni  kwa matumizi ya watendaji wa Shirika; 

iv. Kuchangia mtaji wa TZS 450 milioni Wizara ya Biashara  na Viwanda ikiwa ni mtaji wa uanzishwaji wa kiwanda  cha mwani Zanzibar; na 

v. Utoaji wa gawio kwa Serikali lenye jumla ya TZS 400  milioni sawa na asilimia 80 ya makadirio ya TZS 500 milioni  kutokana na faida iliyopatikana mwaka wa fedha 2019.

OR-Fedha na Mipango 18 

F. MWELEKEO WA BAJETI KWA TAASISI ZINAZOSIMAMIWA NA  OFISI YA RAIS, FEDHA NA MIPANGO 

F.1 Bodi ya Mapato Zanzibar - ZRB 

34.0 Mheshimiwa Spika, Bodi ya Mapato Zanzibar inaendelea na  kazi ya uwakala wa Serikali wa kusanya mapato yatokanayo  na vianzio mbalimbali vya kodi. kwa mwaka wa fedha  2021/2022, inakadiriwa kukusanya jumla ya TZS 525.10 bilioni  kutoka katika vyanzo vilivyoainishwa katika kitabu cha  Mswada wa Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka  2021/2022. 

35.0 Mheshimiwa Spika, Kwa upande wa Matumizi ZRB  inaombewa kuidhinishiwa matumizi ya TZS 17.02 bilioni kwa  ajili ya kutekeleza Shughuli zake za kawaida na Maendeleo.  Kati ya fedha hizo TZS 15.75 bilioni ni ruzuku kutoka Serikali kuu  na TZS 1.27 bilioni kutoka katika vyanzo vyengine ikiwemo  kutoka TRA. Miongoni mwa kazi zitakazotekelezwa ni : 

i. Kukusanya mapato ya Serikali ya TZS 525.1 bilioni; ii. Kuendelea kufanya Ukaguzi wa kodi katika Hoteli kubwa  za Kitalii;  

iii. Kufanya Ukaguzi wa Kodi katika kampuni za Sekta za  Mawasiliano ya simu na Taasisi za Fedha; 

iv. Kuanzisha Matumizi ya Mashine za Kielektroniki za Utoaji  wa Risiti (EFD’s) baada ya kukamilika kwa hatua za  majaribio; 

v. Kuendelea kuwatambua na kuwasajili walipakodi  wapya wapatao 1,000; 

vi. Kuongeza ukusanyaji wa mapato kwa kuimarisha  mifumo ya kielektroniki na taratibu za utendaji kazi; vii. Kuimarisha taratibu za utendaji kazi kwa kutumia mifumo  ya kielektroniki; 

viii. Kuongeza ubunifu katika Teknolojia ya Habari na  Mawasiliano (TEHAMA); na

OR-Fedha na Mipango 19 

ix. Kuhamasisha Ulipaji Kodi kwa Hiari kwa kujenga  utamaduni wa kulipa kodi na kupunguza gharama za  uwajibikaji. 

F.2 Mfuko wa Barabara - ZRF 

36.0 Mhesimiwa Spika, Kwa mwaka wa fedha 2021/2022 Mfuko  unaombewa kuidhinishiwa jumla ya TZS 14.64 bilioni. Kati ya  fedha hizo, matengenezo ya barabara ni TZS 12.86 bilioni  na TZS 1.78 bilioni kwa ajili ya uendeshaji wa Mfuko kwa  kutekeleza shughuli zikiwemo zifuatazo: 

i. Matengenezo makubwa ya kilomita tano (5 km) za  barabara za Mjini Unguja yanayojumuisha upandishaji  wa tabaka la lami (overlaying) na mitaro.  

ii. Kukamilisha matengenezo makubwa ya barabara  zenye jumla ya kilomita (22 km) za Kipapo-Mgelema Wambaa, Micheweni-Kiuyu na ile inayoelekea eneo la  uwekezaji Micheweni. 

iii. Kuweka taa za kuongozea magari (traffic lights) kwenye  maeneo matano ya Unguja na Pemba. 

F.3 Mamlaka ya Ununuzi na Uondoaji wa Mali za Umma -  ZPPDA 

37.0 Mheshimiwa Spika, Mamlaka ya Ununuzi na Uondoaji wa  Mali za Umma itaendelea kutekeleza majukumu yake ya  kusimamia utekelezaji wa Sheria ya Ununuzi na Uondoaji  wa Mali za Umma namba 11 ya mwaka 2016. Kwa mwaka  wa fedha 2020/2021 Mamlaka hii inakadiriwa kukusanya  TZS 444.42 milioni kutoka katika vianzio vyake vya mapato  na inaombewa kuidhinishiwa matumizi ya TZS 2.15 bilioni  ambayo ni ruzuku kutoka Serikalini kwa ajili ya kutekeleza  shughuli zake zikiwemo zifuatazo: 

i. Kufanya ukaguzi na uchunguzi wa ununuzi wa mali za  umma kwa Serikali;

OR-Fedha na Mipango 20 

ii. Kuandaa na kutoa miongozo ya ununuzi wa mali za  umma; 

iii. Kupokea, kuchunguza na kuamua juu ya malalamiko  ya wazabuni katika zabuni za Umma; 

iv. Kuendelea kuimarisha mashirikiano na Taasisi  zinazojishughulisha na ununuzi na uondoaji wa mali za  umma za Tanzana Bara. 

F.4 Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar - ZSSF 

38.0 Mheshimiwa Spika, Kwa mwaka wa Fedha 2021 /2022 Mfuko  wa Hifadhi ya Jamii unatarajia kukusanya jumla ya TZS 150.24  bilioni kutokana na vyanzo vikuu wiwili, kati ya fedha hizo TZS  93.61 bilioni ni makusanyo ya michango ya wanachama wa  Serikali, Taasisi Binafsi na waliojiajiri wenyewe na TZS 56.63  bilioni kutokana na mapato ya uwekezaji wa muda mrefu  na muda mfupi wa masoko ya fedha na mitaji. 

39.0 Mheshimiwa Spika, Mfuko unategemea kutumia Jumla ya TZS  150.24 bilioni kwa matumizi yake ya mwaka 2021/2022. Kati  ya fedha hizo TZS 9.36 bilioni zinategemewa kutumika kwa  matumizi ya uendeshaji, TZS 40.13 bilioni kwa kulipia mafao  ya wanachama na TZS 100.75 bilioni kwa ajili ya uwekezaji. 

F.5 Benki ya Watu w a Zanzibar - PBZ 

40.0 Mheshimiwa Spika, Kwa kipindi cha mwaka 2021 Benki  imejipanga kufanikisha mambo yafuatayo katika kukamilisha  malengo yake. 

i. Rasilimali za benki zinatarajiwa kukua kutoka TZS 753.00  billioni hadi TZS 862.00 bilioni. Ukuwaji huu unatarajiwa  kuchangiwa na ongezeko la mikopo kwa wateja kutoka  TZS 419.00 bilioni hadi kufikia TZS 461.00 bilioni; 

ii. Kwa uapande wa amana za wateja Benki inatarajia 

OR-Fedha na Mipango 21 

kuongeza amana zake kutoka kwa wateja wake hadi  kufikia TZS 623.00 bilioni kutoka TZS 576.00 bilioni. Aidha,  Mtaji unatarajiwa kukua kwa asilimia 16, kutoka TZS  107.00 bilioni hadi TZS 131.00 bilioni; 

iii. Benki inatarajia kupata jumla ya mapato ya TZS 99.75  bilioni, na matumizi ya TZS 69.07 bilioni yanatarajiwa  kutumika kwa mwaka 2021 kwa ajili ya riba na matumizi  yasio ya riba; 

iv. Benki inatarajia kupata faida ya TZS 31.00 bilioni kwa  mwaka 2021 kulinganisha na faida ya mwaka 2020  iliopatikana TZS 18.00 bilioni ambayo ni sawa na  ongezeko la asilimia 72. 

41.0 Mheshimiwa Spika, Benki ya watu wa Zanzibar inatarajia  kutekeleza shughuli zifuatazo kwa mwaka 2021: 

i. kukamilisha tawi la Dodoma, Kigamboni, Tandika na  kituo cha kutolea huduma Tandahimba, Mtwara,  Kinyasini, Chwaka, Dunga, ZIPA na Gombani ili kupanua  wigo wa huduma za kibenki ; 

ii. Kufanya upembuzi yakinifu katika mikoa ya Mwanza,  Arusha, Mbeya, Shinyanga na Tanga ili kuweza kufungua  huduma za kibenki katika meneo hayo; 

iii. Kuimarisha huduma za mawakala kwa ajili ya kurahisisha  upatikanaji wa huduma za Benki nchi nzima na ili  kuondoa tatizo la foleni kwenye Matawi ya Zanzibar; 

iv. Kuanzisha kituo maalum cha huduma kwa wateja  kitakachofanya kazi masaa 24 kwa lengo la kupokea  na kufanyia kazi changamoto za wateja kwa wakati na  haraka; 

v. Kufungua vituo (maduka) ya kubadilisha fedha, bureau  de change katika maeneo ya Paje, Nungwi, Airport Dar  es Salaam na Unguja (Terminal III);  

vi. Kuweka mashine sita za kutolea fedha katika maeneo  ya Gombani, Konde, Mtambile, Amani, Maungani na 

OR-Fedha na Mipango 22 

Kinyasini; na 

vii. Kutoa huduma kwa kadi za malipo (Master card). F.6 Shirika la Bima la Zanzibar - ZIC 

42.0 Mheshimiwa Spika, Shirika la Bima kwa mwaka fedha 2021/22  linatarajia kukusanya jumla ya TZS 31.00 bilioni kutoka katika  vianzio vyake vya mapato kwa kutekeleza mikakati ifuatayo: 

i. Kutoa taaluma kwa Wananchi na taasisi mbalimbali  juu ya suala la kujiwekea kinga mali zao kwa lengo  la kuongeza idadi ya wateja wapya wa biashara  zisizokuwa za magari katika mtandao wake. 

ii. Kuzidisha mashirikiano na mawakala na madalali  wanaofanya biashara ya bima kwa niaba ya Shirika. iii. Shirika kwa kushirikiana na mawakala na madalali  

kutumia kikamilifu mfumo mpya wa Teknolojia “Smart  Policy System” kwa kutoa huduma bora zaidi kwa  Wananchi. 

iv. Kuendelea kuwapatia Wafanyakazi mafunzo mbalimbali  ya kuwajengea uwezo na kuboresha utendaji wa kazi  zao. 

43.0 Mheshimiwa Spika, kwa upande wa matumizi, Shirika kwa  mwaka wa fedha 2021/22 limepanga kutumia jumla ya TZS  15.50 bilioni ikijumuisha matumizi yafuatayo: 

i. Matumizi kwa kazi za kawaida za Shirika ni TZS 9.80 bilioni; ii. Matumizi kwa kazi za maendeleo ni TZS 5.70 bilioni  ikijumuisha gharama za ujenzi wa jengo la Shirika Pemba

OR-Fedha na Mipango 23 

G. MWELEKEO WA BAJETI YA OFISI YA RAIS, FEDHA NA MIPANGO  KWA MWAKA 2021-2022 

G.1 Vipaumbele vya Ofisi ya Rais Fedha na Mipango 

44.0 Mheshimiwa Spika, Baada ya kutathmini miongozo  inayotolewa na viongozi wa nchi yetu ikiwemo Dira 2050,  Ilani ya Uchaguzi wa CCM ya mwaka 2025 na Hotuba ya  Mheshimiwa Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi  aliyoitoa katika uzinduzi wa Baraza la kumi la Wawakilishi  aliyoitowa Barazani siku ya tarehe 11/11/2020 na kuzingatia  mwenendo wa hali ya Uchumi wa nchi yetu pamoja  na mwenendo wa hali ya Uchumi wa Dunia. Baada ya  kuyazingatia yote hayo Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango  imejipanga kutekeleza vipaumbele vifuatavyo:  

i. Kusimamia ukusanyaji wa Mapato ya Serikali ya TZS 1.78  trilioni; 

ii. Kuunda na Kusimamia Mifumo ya kielektroniki  itakayorahisisha ukusanyaji wa Mapato, Bajeti na  Matumizi ya Serikali; 

iii. Kuanzisha kitengo maalum cha kuchambua taarifa  za kibiashara (Business Inteligence Unit) ili kuweza  kuzitambua taarifa hizo na kupata taarifa sahihi katika  utozaji kodi ya Serikali; 

iv. Kuimarisha kitengo cha Ufuatiliaji na tathmini ili kuweza  kufuatilia utekelezaji wa miradi na shughuli za Serikali na  kuweza kutoa tathmini halisi za utekelezaji;  

v. Kutayarisha Mkakati wa Mawasiliano wa Mpango wa  Maendeleo wa Muda wa Kati wa Zanzibar 2021-2025; vi. Kutafsiri Dira ya Maendeleo ya Zanzibar 2050 na  Mpango wa Maendeleo wa Muda wa kati kwa Lugha  nyepesi za Kiswahili na Kiingereza; 

vii. Kusimamia Utekelezaji wa Mfumo wa Kielektroniki wa  Taarifa za Ufuatiliaji na Tathmini kwa ngazi zote; na

OR-Fedha na Mipango 24 

viii. Kuandaa Sensa ya Watu na Makaazi 2022. 

G.2 Makadirio ya Mapato ya Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango 

45.0 Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2021/2022, Ofisi ya Rais,  Fedha na Mipango inakadiriwa kukusanya jumla ya TZS  1.78 trilioni. Makusanyo hayo ni ongezeko la asilimia 15  ikilinganishwa na makadirio ya kukusanya TZS 1.549 trilioni  yaliyopangwa kukusanywa kwa mwaka 2020/202. 

G.3 Makadirio ya Matumizi ya Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango 

46.0 Mheshimiwa Spika, Kwa mwaka wa Fedha 2021/2022 Ofisi ya  Rais Fedha na Mipango inakadiriwa kutumia TZS 402.13 bilioni  kwa mafungu yanayosimamiwa na Ofisi ya Rais, Fedha na  Mipango na uchambuzi wake ni kama ifuatavyo: 

i. Fungu F01 limekadiriwa kutumia TZS 170.00 bilioni; ii. Fungu F02 limekadiriwa kutumia TZS 208.99 bilioni na iii. Fungu F03 limekadiriwa kutumia TZS 23.15 bilioni.  

47.0 Mheshimiwa Spika, naomba sasa uniruhusu kuwasilisha  uchambuzi wa matumizi ya Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango  kwa kuzingatia programu kama ifuatavyo: 

a. Matumizi kwa fungu F01 yanakadiriwa kufikia TZS 170.00  bilioni ambazo zinatarajiwa kutumika katika utekelezaji  wa programu kuu tatu (3) zifuatazo: 

i. Programu ya Usimamizi wa Fedha za Umma na  Bajeti inakadiriwa kutumia TZS 65.06 bilioni; 

ii. Programu ya Usimamizi wa Mali za Umma  inakadiriwa kutumia TZS 83.81bilioni; na 

iii. Programu ya Utumishi na Uendeshaji wa Ofisi ya  Rais, Fedha na Mipango inakadiriwa kutumia TZS  21.14 bilioni.  

b. Matumizi kwa fungu F02 yanakadiriwa kufikia TZS  208.98 bilioni ambayo yanategemewa kulipia viinua 

OR-Fedha na Mipango 25 

mgongo vya wastaafu, Pencheni, kulipia madeni ya  Serikali pamoja na kulipia huduma nyengine za Serikali  zinazolipwa kwa kupitia Mfuko Mkuu. 

c. Matumizi ya fungu F03-Tume ya Mipango yanakadiriwa  kufikia TZS 23.15 bilioni ambazo zinatarajiwa kutumika ili  kutekeleza shughuli za Programu kuu zifuatazo: 

i. Programu ya Uratibu Mipango ya Kitaifa na  Maendeleo ya Watendakazi inakadiriwa kutumia  TZS 4.85 bilioni; 

ii. Programu ya Usimamizi wa Uchumi Mkuu, Tafiti na  Takwimu inakadiriwa kutumia TZS 14.58 bilioni; na 

iii. Programu ya Uendeshaji wa shughuli za Tume ya  Mipango inakadiriwa kutumia TZS 3.72 bilioni. 

48.0 Mheshimiwa Spika, pamoja na programu kuu nilizoziwasilisha  Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango itatekeleza programu ndogo  kumi na tisa (19) ambazo uchambuzi wake umewasilishwa  katika rasimu ya Mswada wa Makadirio ya Mapato na  Matumizi ya kazi za kawaida na kazi za maendeleo kwa  mwaka 2021/2022 ukurasa F01-i hadi F03-11 “volume 2”.  

G.4 Matumizi ya miradi ya maendeleo inayotekelezwa na Ofisi  ya Rais, Fedha na Mipango kwa mwaka 2021/2022 

49.0 Mheshimiwa Spika, pamoja na utekelezaji wa shughuli  za kazi za kawaida, Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango kwa  mwaka 2021/2022 itatekeleza miradi saba (7) ya maendeleo  ambayo inakadiriwa kutumia TZS 99.09 bilioni. 

H. SHUKRANI 

50.0 Mheshimiwa Spika, Matayarisho ya bajeti yamehusisha  wadau wengi, wakiwemo watendaji wa Ofisi yangu na  taasisi mbali mbali ambao tumeshirikiana kukamilisha suala  hili. 

OR-Fedha na Mipango 26 

51.0 Mheshimiwa Spika, kwa misingi hiyo naomba kutoa shukrani  zangu kama ifuatavyo: kwanza nianze kuwashukuru sana  Watendaji wakuu wa Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango  wakiongozwa na Katibu Mkuu Dkt. Juma Malik Akil, Katibu  Mtendaji wa Tume ya Mipango Nd. Mwita Mgeni Mwita, Naibu  Katibu Mkuu Fedha na Mipango, Ndugu Khamis Suleiman  Mwalim na Naibu Katibu Mkuu Mifumo, Ndugu Rashid Said  Rashid pamoja na Wakuu wa Taasisi, Idara na wafanyakazi  wote wa Ofisi hii kwa mashirikiano wanayonipatia ambayo  yanakuza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu ya Ofisi  hii. Aidha, nawashukuru sana Washirika wa Maendeleo  wakiwemo: Benki ya maendeleo ya Afrika (ADB), Benki ya  Dunia, IMF-Kanda ya Afrika Mashariki, Serikali ya Jamhuri ya  China, Serikali ya Norway, IFAD na wengine wengi. 

52.0 Mheshimiwa Spika, kwa namna ya pekee nawashukuru sana  wananchi wote wa Zanzibar kwa umoja na mashirikiano yao  ambayo yamekuza utulivu na kupelekea nchi yetu kuwa  ni nchi ya amani. Mheshimiwa Spika, mwisho lakini sio kwa  umuhimu naomba tena nichukue nafasi hii kwa wananchi wa  jimbo la Magomeni ambao walinichagua kuwa muwakilishi  wao, nawashukuru pia kwa ustahamilivu wao ambao hunipa  fursa ya kuendelea na majukumu mengine ya Serikali yetu. 

I. HITIMISHO 

53.0 Mheshimiwa Spika, Baada ya maelezo niliyoyatowa sasa  naomba Baraza lako tukufu kuridhia maombi ya Ofisi ya Rais,  Fedha na Mipango kukusanya mapato ya TZS 1.78 trilioni kwa  mwaka 2021/2022. Aidha, naliomba Barara lako kuidhinisha  matumizi ya TZS 402.13 bilioni ili Ofisi iweze kutekeleza shughuli  zilizopangwa kwa mwaka 2021/2022.  

54.0 Mheshimiwa Spika, Maelezo na shughuli zitakazotekelezwa  kwa mwaka 2021/2022 yanapatika katika kitabu cha pili 

OR-Fedha na Mipango 27 

(volume 2) cha Mswada wa Makadirio ya Mapato na  Matumizi ya Fedha kwa Bajeti inayotumia programu (PBB)  kwa mwaka wa Fedha 2021/2022-2023/2024 katika ukurasa  wa F01-i hadi F03-11. 

55.0 Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja. 

JAMAL KASSIM ALI 

WAZIRI WA NCHI, 

OFISI YA RAIS, FEDHA NA MIPANGO, 

ZANZIBAR.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.