Habari za Punde

Dunia imekabiliwa na changamoto kubwa ya kutojitosheleza kwa mahitaji ya chakula kutokana na ongezeko la idadi ya watu na mabadiliko ya tabia nchi

 

Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Othman Masoud Othman, akisoma hotuba wakati wa ufunguzi wa semina ya kuwajengea  uelewa viongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wakiwemo Mawaziri, Naibu Mawaziri  na Makatibu Wakuu wa SMZ, kuhusu matumizi ya Baiteknoloji ya Kisasa. Kushoto kwa Makamu ni waziri katika Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Mhe. Harous Said Suleiman na  Katibu Mkuu Kiongozi  ndugu Zena Ahmed Said.  Katika Semina hiyo Mhe. Othman alimuwakilisha Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Mwenyi imefanyika Ukumbi wa Sheikh Idrisa Abdulwakili  Kikwajuni mjini Zanzibar leo Tarehe 27.12.2022.

Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Othman Masoud Othman, katikati akifafanua jambo wakati wa semina ya kuwajengea  uelewa viongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wakiwemo Mawaziri, Naibu Mawaziri  na Makatibu Wakuu wa SMZ, kuhusu matumizi ya Baiteknoloji ya Kisasa. Kulia kwa Makamu ni waziri katika Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Mhe. Harous Said Suleiman na Kushoto ni Katibu Mkuu Kiongozi Zena Ahmed Said.  Katika Semina hiyo Mhe. Othman alimuwakilisha Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Mwenyi imefanyika Ukumbi wa Sheikh Idrisa Abdulwakili  Kikwajuni mjini Zanzibar leo Tarehe 27.12.2022.

 Picha na Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Kitengo cha Habari.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mpinduzi Mhe. Dk. Hussein Mwinyi, amesema kwamba dunia imekabiliwa na changamoto kubwa ya kutojitosheleza kwa mahitaji ya chakula kutokana na ongezeko la idadi ya watu na mabadiliko ya tabia nchi ambayo yanaathiri uzalishaji.

Mhe. Rais Mwinyi ameyasema hayo katika hotuba iliyosamwa kwa niaba yake na Makamu wa  Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Othman Masoud Othman, alipomuwakilisha Rais katika ufunguzi wa semina ya kuwajengea uwelewa kwa viongozi wa serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuhusu matumizi ya Bioteknolojia ya kisasa huko katika ukumbi wa sheikh Idrisa Abduliwakili Kikwajuni Mjini Zanzibar.

Aidha  Dk. Mwinyi amesema kwamba idadi ya watu Barani Afrika ikiwemo Tanzania na Zanzibar inategemewa kuongezeka maradufu ifikapo 2050 na kwamba hali hiyo itasababisha usalama wa chakula kuwa na changamoto kubwa iwapo hatua sahihi hazitachukuliwa  mapema ili kuzuia hali hiyo isiwe janga.

Hivyo Mhe. Rais amesema kwamba matumizi ya biteknoloji ya kisasa ni elimu inayowezesha kufanyika mabadiliko ya vijinasaba (DNA) kwa kuvumbua mambo mbali mbali katika nyanja za Afya , Uchumi wa bluu, Kilimo , Ufugaji , Mazingira na bidhaa za viwandani.

Aidha Dk. Mwinyi amefahamisha kwamba Biteknolojia ya kisasa iwapo itatumika kwa usahihi na ufanisi inaweza kuchangia katika kuleta maendeleo  endelevu ya kiuchumi na kijamii kwa haraka kama ilivyofanyika katika upatikanaji wa chanjo ya maradhi ya Uviko 19 iliyopatikana kwa muda mfupi sana.

Sambamba na hayo Mhe. Mwinyi amesema kwamba katika Nyanja ya afya biteknoliji ya kisasa pia inatumika katika kuzalisha dawa na chanjo mbali mbali , kutambua magonjwa na kutengeneza vyakula vyenye virutubisho ili kukabiliana na matatizo ya utapia mlo.

Mbali na hayo pia Rais Mwinyi amesema kwamba teknolojia  ya kisasa inaweza kutumika katika kusafisha mazingira hasa katika kuondoa mabaki ya sumu  zinazotokana na taka za viwandani  na kupunguza matumizi ya viuwatilifu  na hivyo kuchangia katika kutunza hifadhi ya mazingira pamoja na afya za binaadamu na wanyama.

Aidha amesema kwamba teknolojia hii ni muhimu katika maendeleo ya sekta ya viwanda kwa uzalishaji wa bidhaa kama za nishati mbadala ya biogesi, kutengeneza vyakula vya mifugo dawa za kusafishia vipodozi  vya binaadamu .

    Akiwasililisha mada kuhusu   Bioteknolojia ya Kisasa, Matumizi, Fursa, Faida na changamoto zake Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Dk. Aly Mahadhy, amesema kwamba kuwepo kasi ya ongezoke la idadi ya watu, mabadiliko ya tabia nchi na ardhi kuliwa na bahari  kutasababisha kukosekana kwa eneo la kilimo na hivyo kusababisha uhaba mkubwa wa chakula.

Aidha amefahamisha kwamba kuwepo kwa magonjwa ya mazao ya kilimo kama vile mpunga , muhogo na migomba ambacho ni chakula muhimu kwa wananchi kunahitajika juhudi kubwa za kiutafiti ili kuweza kuzalisha mbegu mbadala na vifaa tiba na chanjo za magonjwa mbali mbali kupitia teknolojia ya kisasa ili kukabiliana na hali hiyo.

Mapema Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Kwaza wa Rais Zanzibar Dk. Omar Dadi Shajak, amesema kwamba mafunzo hayo ni muhimu katika kufanya tathmini ya masuala yanayohusu matumizi ya teknolojia ya kisasa na kusaidia Zanzibar  katika uandaaji wa sera na sheria ili kuweka muongozo sahihi wa matumizi ya teknolojia ya kisasa.

Semina hiyo ya siku moja imeandaliwa kwa pamoja na Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Tume ya Mipango na kudhaminiwa na Tume ya Sayansi na Teknolojia ya Tanzania Bara na kuwashirikisha  Mawaziri , Naibu Mawaziri , Makatibu Wakuu pamoja na Manaibu Katibu wakuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Imetolewa na ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Kupitia Kitengo chake cha habari leo tarehe 27.12.2022.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.