Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhajj Dk.Hussein Mwinyi Amujumuika na Wananchi wa Mkoa wa Kusini Katika Dua ya Kuwaombea Kumuombea na Kuiombea Nchi Amani Iliyofanyika Msikiti wa Ijuma Mtegani Makunduchi

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk.Hussein Ali Mwinyi akiweka ubani kwa ajili ya kuwarehemu Wazee,Viongozi na kuwaombea dua Viongozi Wakuu na kuiombea Nchi Amani, iliyofanyika katika Msikiti Mkuu wa Ijumaa Mtegani Makunduchi Mkoa wa Kusini Unguja, iliyofanyika leo 16-12-2023 na (kushoto kwa Rais) Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh Saleh Omar Kabi na Kadhi Mkuu wa Zanzibar Sheikh. Hassan Othman Ngwali
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhajj Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza na kuwasalimia Wananchi wa Mkoa wa Kusini Unguja baada ya kumalizika kwa Dua Maalum iliyoandaliwa na Mkoa kwa ajili ya kuwaombea Viongozi Wakuu na kuiombea Nchi Amani, dua hiyo iliyofanyika katika Msikiti Mkuu wa Ijumaa Mtegani Makunduchi Mkoa wa Kusini Unguja
WANANCHI wa Mkoa wa Kusini Unguja wakimsikiliza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhajj Dk.Hussein Ali Mwinyi (hayupo pichani) akizungumza na kuwasalimia Wananchi baada ya kumalizika kwa Dua maalum iliyoandaliwa kuwaombea Viongozi Wakuu na kuiombea Nchi Amani, iliyofanyika katika Msikiti Mkuu wa Ijumaa Mtegani Makunduchi 
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhajj Dk.Hussein Ali Mwinyi akijumuika na Viongozi na Wananchi wa Mkoa wa Kusini Unguja katika kuitikia dua ikisomwa na Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh.Saleh Omar Kabi (kushoto kwa Rais) na (kulia kwa Rais) Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Katiba,Sheria,Utumishi na Utawala Bora Zanzibar Mhe. Haroun Ali Suleiman, baada ya kumalizika kwa dua maalum ya kuwaombea Viongozi Wakuu na kuiombea Nchi Amani, iliyofanyika katika Msikiti Mkuu wa Ijumaa Mtegani Makunduchi Mkoa wa Kusini Unguja.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Al hajj Dk. Hussein Ali Mwinyi, amewashukuru Waumini wa dini ya Kiislam wa Mkoa wa Kusini Unguja, kwa nia yao njema ya kumuombea dua na kuliombea dua taifa.

Amesema, utamaduni wa kuiombea dua nchi na viongozi lazima uendelezwe na udumishwe hasa wakati huu ambao dunia imegubikwa na mabalaa mengi yenye athari mbaya.

Al hajj Dk. Mwinyi ameyasema hayo kwenye dua maalum iliyoandaliwa na Wazee na viongozi wa Mkoa wa Kusini Unguja, kwa kumuombea dua yeye na taifa kwa kipindi chote cha uongozi wake. Dua hiyo imefanyika msikiti wa Ijumaa, Makunduchi Wilaya ya Kusini, Mkoa wa Kusini Unguja.

Alisema, hakuna jambo jema kwa wakati uliopo zaidi ya kumuomba Mwenyezi Mungu aiepushe nchi na mabala ya vita, mabadiliko ya taiba nchi na mazingira ikiwemo upepo mkali na mafuriko.

Akizungumzia suala la amani, utulivu na mshikamano wa nchi na watu wake, Al Hajj Dk. Mwinyi alisema amani na utulivu wa nchi ndio kila kitu kwa mustakbali mwema wa maendeleo endelevu na ustawi wa taifa na uchumi wake.

Akitolea mfano mataifa ya Urusi, Ukraine, Sriya, Iraq na nchi nyngine duniani zilizogubikwa na vita pamoja na mataifa yaliyoathiriwana ukame ikiwemo Pakistani, Al hajj Dk. Mwinyi alisema dunia imekua kama Kijiji, inashuhudiwa mabalaa mengi ya vita na majanga ya kimaumbile yanavyoiathiri, hali ilizusha taharuki na uchumi wa dunia kutetereka, ikiwemo kupanda kwa gharama za maisha na uchumi wa dunia.

Al hajj Dk. Mwinyi aliongeza hali hiyo pia imeathiri sana mataifa yanayoendelea ikiwemo Tanzania na Zanzibar kwa ujumla, hivyo alilisitiza utamaduni wa kuendelea na kudumisha suala la kuiombea dua nchi na viongozi wake.

“Tunawajibu wa kuendelea kumuomba Mwenyezi Mungu atuepushe na mabalaa mbalimbali, mabalaa ya vita na matatizo ya kimaumble, mabadiliko ya mazingira ikiwemo upepo mkali na mafuriko” aliomba Al hajj Dk. Mwinyi.

Akizungumzia maendeleo makubwa yaliyofikia na awamu ya nane ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Al hajj Dk. Mwinyi alieleza kuwa imeendelea kufanya mengi makubwa ikiwemo kufanikisha miradi mingi ya maendelo na kuimarisha miundombinu ya mawasiliano zikiwemo barabara za kisasa zenye viwango vya hali ya juu, ujenzi na uimarishwaji wa huduma za elimu, afya, miradi mingi ya maji kwa kujengwa skuli na hospitali za kisasa zenye hadhi za hali ya juu.

Pia, aliahidi kuendelea kupeleka miradi mikubwa ya maendeleo mkoani humo na maeneo mengine ya nchi.

Akizungumza kwenye dua hiyo, Waziri Nchi Ofisi ya Rais Katiba, Sheria, Utumishi na Utawala Bora, Mhe. Haroun Ali Suleiman aliwasihi wananchi wa Zanzibar kuendelea kumuombea dua Al hajj Dk. Mwinyi kwa maendeleo makubwa anayoyafanya nchini.

Akitoa neno la shuqrani kwa niaba ya masheikh na wazee wa Makunduchi, Shekh Muadhini Jongo ameshukuru Al hajj Dk. Mwinyi kwa kuridhia kufika Makunduchi kujumuika nao kwenye dua hiyo pamoja na kuwashukuru Waislam wote walioshirikiana kuifanikisha.

Dua hiyo, pia ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa dini wakiongozwa na Mufti Mkuu wa Zanzibar, Sheik Saleh Omar Kaab pamoja na viongozi wa Chama na Serikali.

Pia, Al hajj Dk. Mwinyi alizuru makaburi ya  aliekua Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Awamu ya nne, Marehemu Sheikh Iddrisa Abdul Wakili na Kaburi la Sheikh Hassan bin Ameir, aliekua mwanazuoni mkubwa Zanzibar.

IDARA YA MAWASILIANO IKULU, ZANZIBAR.

 
 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.