Habari za Punde

Rais Dkt. Magufuli Anataka Wachimbaji Kunufaika na Rasilimali ya Madini --BITEKO

Waziri wa Madini Doto Biteko akitazama machimbo ya Madini ya Bati (Tin) alipofanya ziara yake ya kikazi wilayani Kyerwa Mkoa wa Kagera
 Waziri wa Madini Doto Biteko akikagua vifaa vinavyotumika kuyeyushia Madini ya Bati mara baada ya kufanya ziara yake ya kikazi wilayani Kyerwa Mkoa wa Kagera.
WAZIRI wa Madini Doto Biteko kushoto akisalimiana na mchimbaji mdogo wa madini ya bati (TIN) katika soko la madini Kyerwa mara baada ya kumaliza mkutano nao



Na Tito Mselem Kagera
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli anataka wachimbaji wote wa madini nchini wafaidike na madini ambayo Mwenyezi Mungu amewabariki kuwanayo katika maeneo yao.
Hayo yamesemwa na Waziri wa Madini, Doto Biteko, alipokuwa kwenye ziara yake ya kikazi wilayani Kyerwa Mkoa wa Kagera ambapo alizungumza na wachimbaji pamoja na wafanyabiashara wa  Madini ya Bati (Tin).
Waziri Biteko alisema, anachokitaka Rais Dkt. John Pombe Magufuli ni kuona wachimbaji wote wa madini nchini wanafaidika na madini yaliyopo kwenye maeneo yao, hii ndiyo awamu ya wachimmbaji kutajirika.
“Wote ni mashahidi kwa muda mrefu madini yetu yalikuwa yanatoroshwa, lakini Mheshimiwa Rais akasema hapana tuanzishe masoko, leo wote tunaona mafanikio makubwa yanayotokana na masoko hayo,” alisema Waziri Biteko.
Tanzania hatukuwahi kuwa na Cheti cha Uhalisia wa Madini ya Bati lakini Rais akasema hapana tutafute Cheti cha Uhalisia lakini tunashukuru Mungu Cheti cha Uhalisia tumekipata, Biteko aliongeza.
Aidha, Waziri Biteko amewaruhusu wafanyabiashara wa Madini ya Bati kuyasafirisha madini yaliyoongezwa thamani kwenda kuuzwa nje ya nchi ili yauzwe kwa bei nzuri na wachimbaji kufaidika.
Pamoja na mambo mengine Waziri Biteko, amewataka wachimbaji wa Madini ya Bati kurejea kazini na kuachana na vitendo vya kutorosha madini hayo na badala  yake wayapeleke sokoni.
Pia, Waziri Biteko amewataka wachimbaji hao kupendana, kuthaminiana na kuachana na mambo ya majungu ili kujikita katika kuongeza tija kwenye shughuli yao ya uchimbaji madini.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kyerwa Rashidi Mwaimu alimpongeza Waziri wa Madini, kwa kazi nzuri anazozifanya na kuwataka wachimbaji wa Madini ya Tin kutumia fursa hiyo kueleza changamoto zao mbele ya Waziri.

Nae, Mwenyekiti wa wachimbaji wadogo wa Madini ya Tin wilayani Kyerwa Osward Inyasi, kwa niaba ya wachimbaji wenzake alieleza kuwa wachimbaji wa madini ya Tin bado wanashida ya wanunuzi wa madini yao kwani hadi sasa wana zaidi ya tani 20 zimewekwa stoo baada ya kukosa wanunuzi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.