Habari za Punde

Bi. Omolo: Maafisa Usafirishaji Epukeni Mwendokasi.

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango, Bi. Jenifa Omolo, (wa tatu kushoto), Mhasibu Mkuu wa Serikali Bw. Leonard Mkude, (wa tatu kulia), Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Utawala na Rasilimali Watu Bw. Renatus Msangira, (wa kwanza kushoto) akifuatiwa na Mwenyekiti wa Maafisa Usafirishaji Wizara ya Fedha na Mipango Bw. Emmanuel Mkumbo, wakimkabidhi zawadi yam ashine ya kufulia nguo aliyekuwa Afisa Usafirishaji (dereva) wizarani hapo Bw. Yahaya Kilima, (wa kwanza kulia), aliyestaafu baada kutimiza umri wa kustaafu utumishi wa umma, katika hafla ya kumuaga iliyoratibiwa na Maafisa Usafirishaji wa Wizara hiyo, jijini Dodoma.

Na. Saidina Msangi, WFM, Dodoma

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango Bi. Jenifa Omolo, amewaasa Maafisa Usafirishaji Wizarani hapo kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu na kuepuka kuendesha vyombo vya moto kwa mwendokasi ili kuepusha ajali.

Alitoa rai hiyo wakati wa hafla ya kumuaga aliyekuwa Afisa Usafirishaji Wizarani hapo Bw. Yahaya Kilima, ambaye amestaafu baada ya kutimiza umri wa kustaafu utumishi wa umma, jijini Dodoma.

Alisema kuwa hakuna sababu ya kuendesha magari kwa kasi wakati wa safari na viongozi wao na maafisa wengine badala yake waenedshe mwendo wa wastani ili kuepuka ajali zinazosababishwa na mwendokasi Pamoja na uzembe mwingine barabarani.

‘’Hakuna tunachokimbilia, epukeni mwendokasi lakini pia zingatieni maadili ya utumishi wa umma kwa kuhakikisha kuwa mnatunza siri za Serikali ambazo mnakutana nazo au kuzisikia kutokana na aina ya kazi zenu mnazofanya,’’ alisema Bi. Omolo.

Aidha, aliwaasa Maafisa Usafirishaji wanaoendelea na Utumishi wa Umma kuanza maandalizi ya kustaafu utumishi wa umma mapema ikiwemo kuwa na makazi ya kudumu lakini pia kumtanguliza Mungu katika mipango yao ili iweze kuwa na mafanikio.

Aliwaasa kutenga muda wa kushiriki katika shughuli za kijamii pamoja na kuishi vizuri na ndugu pamoja na jamii kwa ujumla ili wakati wa kustaafu unapowadia waweze kupokelewa vizuri na jamii zao.

Bi. Omolo alimpongeza Bw. Yahaya Kilima, kwa utumishi wake bora wakati wa kutekeleza majukumu yake akiwa kazini na kumtakia kila la heri anapoanza maisha mapya nje ya utumishi wa umma.

Naye Mhasibu Mkuu wa Serikali Wizara ya Fedha na Mipango Bw. Leonard Mkude, alimpongeza Bw. Yahaya Kilima, ambaye alikuwa akimuendesha kabla ya kustaafu, kwa uadilifu wake wakati wa utumishi wa umma na kumpongeza kwa kustaafu, na kumtakia kila la heri katika maisha mapya ya uraiani.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.